Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Mpanda Vijijini kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kukichagua Chama cha Mapinduzi. Na mimi kama mwakilishi wao nawaahidi nitawafanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kuchangia Mpango huu kwenye suala zima la miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya Serikali ni kuhakikisha mikoa yote inaunganishwa na barabara zote zinajengwa kwa kiwango cha lami. Bahati mbaya sana mikoa ya pembezoni imeachwa bila kuunganishwa ukiwemo mkoa wa Katavi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa ya Katavi, Kigoma na Tabora ni Mikoa ambayo ilisahaulika kimaendeleo. Katika Mpango huu ambao Serikali imeuleta, tunaomba rasilimali za nchi hii zigawanywe kwa uwiano ulio sawa. Inafanya wananchi wa maeneo mengine katika nchi yetu wanaonekana kama watumwa wakiwa Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iangalie kwa makini zaidi, tusielekeze kila siku Mikoa ya Kanda ya Kaskazini ndiko ambako wanaelekeza Serikali kupeleka huduma za kijamii. Tunahitaji maeneo ambayo yalisahaulika nayo yaangaliwe na kuwekwa kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali iharakishe kujenga miundombinu ya barabara. Barabara ya Sumbawanga kuja Mpanda ikamilike, barabara ya kwenda Kigoma kutoka Mpanda ikamilishwe na barabara ya kutoka Mpanda kwenda Tabora ikamilishwe. Vilevile bado barabara zile za Mkoa wa Tabora kwenda Kigoma nazo zikamilishwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyozungumza leo hii, Mkoa wa Katavi umekaa kisiwani. Barabara ya kutoka Mpanda kwenda Tabora haipitiki. Nasikitika tu kwamba hata leo Serikali ilipokuwa inatoa kauli, uwezekano wa kupita barabara ile ya kutoka Sikonge kuja Wilaya ya Mlele, haupo. Bahati mbaya Serikali imesahau maeneo hayo. Naomba miundombinu iangaliwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwenye suala la miundombinu ni ujenzi wa reli. Reli tunayoihitaji Watanzania ni reli ya kutoka Dar es Salaam kuja Tabora; reli ya kutoka Tabora kwenda Mwanza; reli ya kutoka Tabora kwenda Kigoma. Vilevile tawi la reli la kutoka Uvinza kwenda Msongati na tunahitaji reli ya kutoka Tabora kwenda Kaliua - Mpanda – Karema. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo sababu za msingi ambazo tunaomba Serikali iangalie. Nchi ya Congo inajenga reli kutoka Lubumbashi kuja Kalemie kwa lengo la kutaka kuunganisha reli inayotoka Karema kwenda Tabora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Wakongo wameona kuna umuhimu bidhaa zao zipitie kwenye nchi yetu, sisi ambao tuna umuhimu wa kutumia Bandari ya Karema na kuifanya Bandari ya Dar es Salaam ipokee mzigo mkubwa, ni kwanini tuwe na vikwazo vya kusuasua tusijenge reli hii na kutoa maamuzi? Naomba Serikali iliangalie hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la kilimo. Watanzania walio wengi wanafanya kazi na wengi wanajishughulisha na shughuli za kilimo. Naiomba Serikali, ni lazima ifike mahali iangalie umuhimu wa kuboresha kilimo. Ili kilimo kiweze kuwa na maboresho, kwanza iangalie gharama za pembejeo. Pembejeo nyingi zinazoletwa kwa ajili ya shughuli za kilimo ni za bei ya ghali. Tena inafikia mahali Jimboni kwangu, bei za pembejeo zenye ruzuku ya Serikali ni za ghali kuliko bei za soko.
Sasa inafanya kilimo hiki kisiweze kwenda. Naomba iangalie umuhimu wa kuboresha shughuli za masoko ili tuweze kusaidia mazao ya kibiashara. Ni lazima Serikali ifike mahali iwe na kitengo maalum cha kutafuta masoko ili kuyasaidia mazao ambayo yanalimwa na Watanzania walio wengi.
Jimboni kwangu kunalimwa zao la tumbaku. Tumbaku sasa hivi ni zao ambalo kwa wananchi ni kama utumwa, kwa sababu masoko yake ni ya shida. Naiomba Serikali iangalie umuhimu sasa wa kujenga kiwanda ambacho kitasindika mazao ya zao hili la tumbaku sambamba na mazao ya korosho, kahawa na mengineyo yale ya kibiashara ambayo yatakuza uchumi kwa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine nilikuwa napenda kuishauri Serikali iwekeze kwenye shughuli nzima ya uvuvi na ufugaji. Ili wavuvi waweze kuwa na mazao mazuri yenye tija, ni lazima Serikali iangalie masoko na kuwapa huduma wavuvi ambao wanavua kwenye eneo la Ziwa Tanganyika ambako kunahitaji miundombinu ya umeme ili wananchi wanaofanya shughuli kwenye mwambao wa Ziwa Tanganyika waweze kunufaika na kuona umuhimu wa kuwekeza kwenye suala zima la uvuvi. Tunahitaji Serikali ijenge viwanda vidogo vidogo vitakavyowasadia wananchi hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naiomba Serikali iangalie suala zima la huduma ya maji. Ili Watanzania waweze kufanya shughuli za kiuchumi vizuri, ni vyema Serikali ikasaidia kuwekeza miundombinu ya maji kwenye maeneo mengi, hasa vijijini. Naiomba Serikali, kwenye Jimbo langu tuna miradi ya maji ambayo haijakamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ikamilishe haraka; na ipeleke kwenye maeneo mapya ambayo tuna Watanzania walio wengi ambao wapo kule maeneo ya Mishamo, hawana huduma ya maji. Tuna Kijiji cha Kamjela, Kijiji cha Kusi, Ipwaga, Ilangu na maeneo mengineyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo mapya yanahitaji yapate huduma ya maji. Naomba Serikali iangalie maeneo yale kwani huko nyuma yalikuwa yanahudumiwa na UN, kwa sasa yapo mikononi mwa Serikali. Naomba Serikali pia iangalie eneo la migogoro ya ardhi. Tunayo maeneo mengi katika Jimbo la Mpanda Vijijini ambalo limezungukwa na mapori, ifike mahali Serikali imalize migogoro ya ardhi, hasa ile ya WMA kwenye vijiji vya Kabage, Sibwesa, Nkungwi, Kasekese na Kaseganyama. Lakini...
MWENYEKITI: Ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.