Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nachukua nafasi hii kukushukuru kunipa nafasi tena ili na mimi niweze kutoa mawazo yangu juu ya Wizara hii ya Fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaendelea nataka mimi pia kama ambavyo amezungumza mzungumzaji aliyepita, nikutie moyo kwamba kazi unayofanya ni njema, hauna sababu za kunyong‟onyea au kujisikia upweke, sisi tupo. Wote tumetumwa na wananchi ili kuja kuwasemea hapa Bungeni. Kwa hiyo, timiza wajibu wako kama ambavyo inakupasa kufanya na sisi tutakuwa pamoja na wewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nijielekeze sasa kwenye kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri lakini nianze na ukurasa ule wa 40, Msajili wa Hazina. Msajili wa Hazina anayo kazi kubwa ya kusimamia rasilimali za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali kwa ujumla. Kazi yake hii ni kubwa na muhimu sana kwa Taifa, inabeba vitu vingi, mashirika na taasisi za Serikali uangalizi wake uko chini yake. Nilikuwa najaribu kujiuliza, je, huyu mtu ana wafanyakazi wa kutosha? Tena wawe wa kada mbalimbali kwa sababu, mashirika na taasisi hizi za Serikali ni nyingi lakini pia zina sekta mbalimbali tofauti-tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najaribu kuangalia bajeti yake aliyowekewa na kulinganisha na ukubwa wa kazi ambayo amepewa, naona kama haitoshelezi. Mwanzoni niliona kama ni kubwa, iko shilingi 160,181,000,000 nikaona kama ni kubwa lakini nilipoingia kwa undani nikakuta ndani yake shilingi milioni kama 150 hivi ni kama social responsibilities kwa mashirika yaliyo chini ya huyu Msajili wa Hazina. Nikaona ukiondoa pesa za maendeleo anabaki na hela kidogo sana za uendeshaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu hii imepewa kazi kubwa sana. Mheshimiwa Rais alipokuwa akihutubia Bunge hili alisema kuna mashirika ya umma yaliyouzwa ambayo tathmini yake inabidi ifanyike, mengine yarudishwe, mengine yaangaliwe kama yalipouzwa yanaendelea kufanya shughuli zile ambazo zilikuwa zimekusudiwa au la. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nimeona tu mashirika ambayo wameandika Kiswahili cha kileo, uperembaji ni kama 55 tu lakini pia hatujaona kwa kina kwamba haya 55 ndiyo yanayofanya kazi, ndiyo yaliyofilisika, ndiyo yaliyobadilisha matumizi au yana hali gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, nilipokuwa najaribu kuangalia bajeti nikaona kwa sababu labda ya bajeti kuwa ndogo ndiyo maana Msajili wa Hazina hajaweza kufanya kazi yake ipasavyo kuweza kutupa taarifa zilizo kamili kama wananchi ili tuweze kufahamu. Kwa sababu kama ni ahadi ya Rais kwamba mashirika haya ya umma mengine yatarudishwa Serikali au yataangaliwa yauzwe upya au mengine yatafanyiwa mpango mwingine, tungetakiwa sisi kama wananchi kujua hatua iliyofikiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Waziri anapohitimisha Wizara yake hii pengine tutapenda kujua kuna hali gani ya mashirika na mali za Serikali chini ya Msajili wa Hazina.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni ufuatiliaji na tathmini. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri pia nilipokuwa najaribu kuangalia ufuatiliaji na tathimini haujapewa uzito ule unaostahili. Asilimia 40 ya bajeti ya nchi yetu mwaka tunaouendea itakuwa ni bajeti ya maendeleo. Kama hatuna mkakati na mpango unaoeleweka juu ya ufuatiliaji na tathmini tunaweza kujikuta tuna miradi ambayo iko chini ya kiwango, haiko sawa na thamani ya fedha iliyopangiwa au haijakamilika sawasawa. Kwa hiyo, kipengele hiki cha ufuatiliaji na tathmini ni muhimu sana kikieleweka kwamba kipo na kwamba kinafanyiwa kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri zetu huko tulikotoka miradi mingi inayotoka Serikali Kuu haina fedha ya ufuatilliaji na tathmini. Kwa hiyo, wanapoagizwa kufuatilia miradi hii ili waweze kutoa taarifa Serikalini wanashindwa kufanya hivyo kwa sababu hakuna bajeti mahsusi kwa ajili ya jambo hili kwa hiyo wanahangaika wanabaki tu sasa kujikusanyakusanya wenyewe kwa fedha yao lakini wana malalamiko makubwa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anapokuwa anahitimisha pia ajaribu kuangalia suala la ufuatiliaji na tathmini liwekewe uzito unastahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni uwezo wa mashirika chini ya Wizara hii, yapo mashirika chini ya Wizara hii lakini nizungumzie tu shirika moja la TTCL. TTCL bado inaendelea kupata ruzuku ya Serikali. Najiuliza TTCL ni Kampuni ya Simu kama ambavyo makampuni mengine ya simu yalivyo, inashindwaje kuingia kwenye ushindani kama yanavyoshindana makapuni mengine na yenyewe ikatupatia faida kama Shirika letu la Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukijaribu kuangalia taarifa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri unaona kabisa kwamba TTCL bado haijasimama pamoja na kutiwa nguvu na vitu vingine.
Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri anaposimama hapa kujibu hoja atuelezee mashirika yaliyo chini ya Wizara hii hasa yale ambayo ni mzigo kuna sababu gani ya kuendelea nayo? Kwa nini mengine tusiyaache tukaendelea na mashirika ambayo yanaweza yakatoa faida kwa Serikali?
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho kimezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengine ni Sheria ya Manunizi. Kweli kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri hajataja kitu chochote lakini sheria hii pia ilipigiwa kelele kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais alipokuwa anafungua Bunge hili. Tulitegemea kwamba tungepata majawabu kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kwamba hatua tulizonazo ni zipi sasa kuhusianana na sheria hii. Tunapeleka fedha nyingi kuanzia mwakani kwenye Halmashauri na sehemu zingine lakini Sheria ya Manunuzi imebaki ile ile inayotunyonya, ile ile inayolalamikiwa. Kwa hiyo, tungependa Mheshimiwa Waziri atueleze Sheria hii ya Manunuzi italetwa lini hapa Bungeni ili tuweze kuirekebisha na miradi itakayofanyika ifanyike kweli kuonesha value for money ambayo imetumika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze la mwisho juu ya Benki ya Wakulima ambayo imeundwa hivi karibuni. Benki hii imepewa shilingi 60,000,000,000 lakini bado wanalalamia wakati kuna benki nyingine wamepewa kama shilingi 20,000,000,000. Mfano TIB Corporate hata kwenye hotuba ya Waziri amesema hawa watu wameweza kuvuta amana zingine sasa hii TADB yenyewe imeshindwaje kuvuta amana zingine na inashindwaje hata kufika tu maeneo ambayo wakulima wapo? Kwa sababu ukijaribu kuangalia benki hii bado iko Dar es Salaam kama walivyozungumza wazungumzaji wengine, naona kama hatutaweka nguvu inayoeleweka mwelekeo wake hii pia inaweza ikawa benki tu ambayo ina jina la Benki ya Wakulima lakini wakulima haiwasaidii. (Makofi)
Kwa hiyo, naomba sana tuwasaidie wafanyakazi walioko kwenye benki hii ili kuweza kufikia maeneo yetu ya vijijini ili wawaguse wakulima kama lilivyo jina la benki yao. Vinginevyo tutakuwa tuna Benki ya Wakullima kama tulivyokuwa na Benki ya Wakulima Vijijini CRDB au TRDB zamani lakini isiweze kuwasaidia wakulima wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, yangu yalikuwa ni hayo lakini Mheshimiwa Waziri atakaposimama kuhitimisha hoja yake basi naamini tutapata majibu na majawabu ya hoja hizi nilizozungumza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja.