Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nami niungane na wenzangu wote ambao wametangulia kusema kwamba tukitaka Bunge hili liweze kutekeleza wajibu wake na kwamba kila mtu awe na nafasi, lazima kanuni zisimamiwe humu ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiangalia toka ulipoanza umekuwa ukilikazania hilo, naomba uendelee hivyo, kusitokee mtu anakukatisha tamaa kwa sababu ukikata tamaa maana yake ni kwamba uendeshaji wa Bunge hili hautakuwa na utaratibu ambao unategemewa kisheria. Nakupongeza sana, nakutia moyo na nina uhakika wale waliotaka kukutikisa au kulitikisa Bunge hili watarudi bila wewe kutikisika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu wake na watendaji wote kwa kazi nzuri ambayo tayari wameshaionesha kwa hotuba hii ambayo ni nzuri. Baada ya pongezi hizo nipende kumshukuru na kumpongeza Rais kwa kumchagua Waziri anayeongoza Wizara hii. Waziri nimefanya naye kazi, na-declare interest kwamba nilikuwa Waziri wa Uwekezaji, na nilipohamia Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango ilikuwa chini yangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo naomba niseme machache kuhusu PPP au ubia kati ya Public Sector na Private Sector. Hii ndiyo namna ya kuweza kuhimiza uwekezaji mkubwa ndani ya nchi hii. Huwezi ukaiachia sekta binafsi peke yake wala huwezi kuiachia Serikali peke yake. Tukitaka kujenga uchumi wa soko lazima Serikali na sekta binafsi washirikiane na hakuna namna ambavyo wanaweza kushirikiana ila katika ubia. Sera ipo, sheria ipo, ilifanyiwa marekebisho, kilichobaki ni utekelezaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika ubia kitu ambacho kinatakiwa ni kuona risk ambayo kila mbia anabeba. Kuna athari (risks) nyingine ambazo sekta binafsi haziwezi kubeba, pale ambapo Serikali inahitajika iingie, lakini inapotokea mtaji unapotakiwa na upo kwenye sekta binafsi, Serikali ina uwezo mkubwa wa kuzuia mambo ambayo sekta binafsi wenyewe hawawezi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo lilikuwa limeisibu PPP ni urasimu ambao haukuwa na maana, au kutokuelewa vizuri sera na sheria ile. Wizara ya Fedha na Uwekezaji ndizo zilikuwa zina sera na sheria lakini utekelezaji uko kwenye sector Ministries. Kwa mfano, Wizara ya Ujenzi inaweza ikajenga barabara nyingi sana na katika muda mfupi kama ikipata sekta binafsi ambayo inaweza ikaingia nayo ubia na kuna namna nyingi ya kuweza kuingia kwenye ubia.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka kuliongelea ni nafasi ya mabenki katika kujenga uchumi wa soko. Katika mambo ambayo yaliathiri sekta binafsi ni pale ambapo walipokuwa crowded out na Serikali yenyewe kupitia treasury bills au wakati mwingine hata bonds. Kwa sababu Serikali inapokopa kwenye mabenki, mabenki yatapendelea Serikali kwa sababu risk ya kukopesha Serikali ni ndogo sana au hakuna, kwa hiyo sekta binafsi haiwezi kupata nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Wizara ya Fedha kuamua kutoa fedha zake ambazo zinakopa, ambazo ni zake zenyewe na kuzirudisha Benki Kuu, sasa mabenki yameanza kuwahimiza watu wapeleke fedha benki. Kabla ilikuwa ni uchaguzi wao kupata fedha kutoka kwa watu binafsi, walikuwa wanategemea zile fedha za Serikali ambazo hatimaye Serikali inakopa. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo benki sasa zimeanza kuchacharika.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, najua kwamba Serikali haiwezi kuacha kukopa, lakini mjaribu ku-balance ili sekta binafsi isikose nafasi. Huwezi kuwa na uchumi wa soko kama sekta binafsi haiko active. Kwa hiyo, naomba mliangalie suala la treasury bills.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni riba. Katika uchumi wa soko huru faida haiwezi ikawa juu ya asilimia 10. Sasa kama riba ya benki inayotoza ni zaidi ya asilimia 10 maana yake yule ambaye yuko kwenye soko huru hawezi kwenda kukopa halafu apate faida ya chini. Hili ndilo limelikumba Taifa hili. Naomba muangalie suala hili la riba zinazotozwa na benki zetu. Kwa sababu mkitaka sekta binafsi ambayo ni rational ikakope benki lazima riba iwe chini ya faida ambayo inapatikana kwa sekta binafsi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia hilo, naomba niongelee VICOBA. Kuna fedha nyingi sana ndani ya VICOBA, na fedha zile haziendi benki, tujiulize kwa nini? Ni kwa sababu hakuna sera na sheria. Kuna watu ambao wamesemea hapa, naomba Benki Kuu iangalie sera ambayo itafaa VICOBA viwe rasmi na vinufaishe watu kama inavyohitajika. Vijijini kuna VICOBA vingi sana na sioni namna ambayo soko huru linaweza kwenda vijijini bila VICOBA hivi kutumika. Naomba sana tuone watu walio wengi ambao hawatataka kukopa hela nyingi lakini kwa wingi wao wakikopa kidogo kidogo italeta impact kubwa ndani ya uchumi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka kuliongea kwa ufupi ni Benki ya Kilimo. Nimesikia na Ushirika unataka kuanzisha benki na Serikali ndiyo itakayochangia benki hizo mbili. Tukianza tena kuzindua Benki ya Ushirika maana yake Benki ya Kilimo itasimama kwa sababu hatuna hela za kuchangia benki hizo zote mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Wizara na Benki Kuu kwamba tukazanie Benki ya Kilimo, hatimaye kama Benki ya Ushirika inaanza tuondokane na Benki ya Kilimo lakini hatuwezi kuwa na benki zote mbili na zianze kwa wakati mmoja. Tukiruhusu benki zote mbili zianze kwa pamoja tutatawanya nguvu zetu na hakutakuwa na impact kwenye kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima ndio watakaoikomboa nchi hii, mazao ya kilimo ndiyo yatakayokuwa malighafi ya kiwanda. Mazao ya kiwanda ndicho kitakachokuwa chakula cha wale wanaofanyakazi viwandani na kilimo ndio uti wa mgongo ambao watu wangu wanategemea. Kwa hiyo, tusipokazania benki hii, najua kwamba suala hili liko kwenye bajeti tutakayojadili, lakini kwa leo nataka nisisitize kwamba hatutakuwa tumetenda haki kwenye Benki ya Kilimo kama tutaanzisha Benki ya Ushirika wakati hii ya kilimo bado haijapewa mtaji wa kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Najua kuwa suala la sovereign ratings ni muhimu sana ili nchi hii ionekane kwamba inaweza kukopa kwenye masoko ya nje, lakini hilo tuliangalie kwa sababu kuna nchi ambazo zimefanya hivyo zikaingia kwenye matatizo. Tusiiachie nchi yetu ikaingia kwenye matatizo. Nchi hii tunapata fedha kidogo sana kwenye investment kutoka nje. Kiasi cha investment inayokuja Tanzania ni 0.03 percent, ni hela kidogo sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, jana Waziri wa Mambo ya Nje alivyokuwa anaongelea issue ya Economic Diplomacy; tunachopigania ni kwamba investments zaidi zije na share yetu ya international markets iwe kubwa; hilo ndilo matokeo mazuri ya Economic Diplomacy ambayo ni nzuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiisimamia Benki Kuu na Benki nyingine na sekta binafsi nina hakika tutapiga hatua kubwa kwenye kujenga uchumi wetu na sioni pengine ambapo kazi hii inafanyika isipokuwa kwenye Wizara yetu ya Fedha na Mipango. Nawaombea Mwenyezi Mungu awape afya njema muweze kusimamia. Waziri Mpango ana uwezo, Naibu Waziri ana uwezo, Watendaji wana uwezo, nina hakika Wizara hii itasimamia uchumi wetu vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naomba usikate tamaa. Wewe ni mtoto wetu, sisi tuko hapa kuona kwamba kazi ambazo zinanufaisha Bunge hili unaendelea kuzifanya na usitetereke sisi tuko na wewe. Ahsante sana.