Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nami nikushukuru kwa kunipa fursa niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mbele yetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kutuletea hoja hii sasa pamoja na kwamba, kama walivyosema wachangiaji wengine wanaona imechelewa kidogo. Naomba niseme mapema kabisa kwamba naunga mkono hoja hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee kidogo hotuba fupi ya Kambi Rasmi ya Upinzani iliyowasilishwa hapa na huyu msanii kutoka Mbeya, hotuba ambayo ilikuwa ya mzaha tu, tusiendeleze mambo kama haya katika Bunge hili Tukufu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama wewe haupo Bungeni unaitwaje kuja kuwasilisha maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani? You should be here to stand up to be counted. Sasa tukianza kupiga kura tutamtuma Askari kwenda kuhesabu kura zao kule nje au tuwaite kuja kupiga kura kwa kitu ambacho hawajashiriki?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba tu kwamba tufuate Kanuni zetu bila wasiwasi wowote. Kwanza umewahi kusikia wapi mtu ambaye hakumaliza shule leo anadiriki eti kutilia shaka uelewa wa Daktari wa Falsafa mwenye Shahada na Stashahada sita? Haya yanatokea tu kwenye nchi ambazo zina underdeveloped economies. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Pilato aliwahi kusema wenye busara husema wanapokuwa na kitu cha kusema. Wapumbavu husema ilimradi waseme chochote. Sasa kwa msingi huo naomba sasa niseme kwa kuwa nina kitu cha kusema kuhusu hoja hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa miaka mingi nafikiri sasa ni miaka 11 nchi yetu haikuweza kuridhia Mkataba huu. Je, ni hasara au faida gani tumepata? Naona ni hasara tu kwa kutokuridhia, ninaziona ni hasara. Hasara kubwa kupita zote ni image, sura ya Tanzania machoni mwa Jumuiya ya Kimataifa, kuwa ya kutiliwa mashaka mashaka tu. Sasa leo ambapo biashara ya madawa ya kulevya duniani imeshamiri sana. Ndiyo sababu kwa kutokusaini vitu kama hivi, kutoridhia Watanzania tukisafiri nje ni watu wa kutiliwa mashaka kweli kweli! Tunapekuliwa bila huruma. Unamwona mwenzako kutoka nchi nyingine anapita tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tusisahau mwaka 2013, hivi majuzi, binti yetu mmoja amekwenda kwenye michezo Brazil, namkumbuka kwa jina moja tu la Sara. Alikutwa na dalili kwa mbali tu kwamba kulikuwa na dalili za nguvu kuongezeka, lakini anatoka Tanzania ambayo haijaridhia mikataba kama hii, kafungiwa miaka miwili. Kwa hiyo, kutoridhia kumetuathiri kwa kiasi. Tutoke huko sasa tuingie katika kuridhia, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuridhiwa kwa mkataba huu hakutuongezei tu heshima katika Jumuiya ya Kimataifa, lakini inatupa fursa ya kushiriki katika uendeshaji wa michezo duniani. Kwa sababu, sasa hivi hata tukitakiwa kupimwa Watanzania inabidi matokeo yetu tupeleke Kenya. Lakini hapa watatuletea vifaa. Kutakuwa na faida ya vijana ya wetu, wataalam wetu nao kupata mafunzo, kuendesha vifaa hivyo na vile vile ku-interact na wenzao Kimataifa kuweza kupata ujuzi zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukiwa humu ndani nasi ni sehemu ya Jumuiya ya Kimataifa ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya kwa upande wa michezo. Tunaweza kuwa na fursa kuwaeleza wenzetu tofauti kati ya bangi na mlenda, tofauti kati ya bangi na matembele. Maana ni kama yule binti wetu aliyekamatwa huko Brazil, siyo ajabu alikuwa amekula ugali hapa wa muhogo pamoja na matembele yakaonekana kama yameongeza nguvu, lakini wenzetu kama Kenya wanatumia mirungi na ni zao la biashara, lakini sijaona kama wanatingishwa sana, ingawa kwa kweli sasa hivi ndiyo wameanza kutingishwa kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kutoridhiwa kwa mkataba huu bado tuna changamoto kubwa kama ambayo nimeisema hasa kudhibiti madawa tunayoyalima hapa ndani, bangi. Nafikiri kuna umuhimu Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wakae na Wizara ya Katiba na Sheria vilevile Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tuangalie ni jinsi gani tunaweza kuboresha udhibiti wa dawa kama bangi zinazolimwa nchini na kutumiwa na vijana wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna tatizo hapa, mmea kama mirungi, kwa wenzetu wa Kenya ambao ni sehemu ya Afrika ya Mashariki lile ni zao biashara na juzi wote tumeona Serikali imeongeza ten million US Dollars kuwasaidia wakulima kuhamasisha zao hilo. Sasa na mipaka yetu kama Afrika Mashariki ni very porous, mirungi inaingia kwa wingi sana hapa. Sasa inabidi tukae chini, tuiangalie hiyo hali tunaidhibiti vipi mirungi ambayo inatokea Kenya ambako wenzetu ni zao la biashara, lakini sisi hapa tumeharamisha kwa muda mrefu sana na tusirudi nyuma katika hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu nimegongewa kengele ya kwanza, naomba tu niseme kwamba Azimio hili limekuja katika muda mzuri sasa na naliunga mkono kwa asilimia mia moja. Ahsante sana.