Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kwa kweli kukupongeza wewe kwa ujasiri mwingi ambao umeuonesha ndani ya Bunge hili na kwa vyovyote vile sisi Wabunge wenzako tupo pamoja na wewe na tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu uwe na afya njema, uitende kazi hii ya Watanzania kwa moyo mkunjufu na hongera sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi hii ya kuweza kushiriki katika kuichangia bajeti ya Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, bajeti ya kwanza katika kipindi cha miaka mitano ya uhai wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii imejikita katika mambo mengi ya msingi yakiwemo masuala ya maji, barabara, umeme na mazingira pamoja na uboreshaji wa Reli ya Kati; na kwa hakika suala zima la madini nalo limewekwa kipaumbele ili kuhakikisha kwamba kwa kweli Taifa letu linanufaika kutokana na maliasili tulizonazo ambazo Mwenyezi Mungu ametujalia.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wetu wa Geita ni Mkoa mpya, mkoa huu unatarajia kwa kweli uungaji mkono wa Serikali ili uweze kwenda kwa sababu ni miongoni mwa mikoa mipya minne au mitano sasa ambayo imeanzishwa na Serikali yetu kwa ajili ya kusogeza huduma kwa wananchi. Kwa maana hiyo, mikoa hii inahitaji kwa vyovyote vile uangalizi mzuri katika utekelezaji wa bajeti hizi ambazo zinakuwa zinaandaliwa kila mwaka ili kusudi ikiwezekana mikoa hii iweze kupiga hatua, iende sambamba na maeneo mengine ambayo yametangulia katika kupiga hatua za kimaendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Geita ipo karibu na Ziwa Victoria ambalo ni ziwa kubwa katika Afrika na ni la pili katika ulimwengu huu, kwa maana hiyo linayo maji ya kutosha; na sisi wana Geita tunamshukuru Mungu kwa kutujalia kuzaliwa katika eneo hili ambalo lina maji mengi ya kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, naiomba Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kama ilivyoweza kuwa na ujasiri mwingi wa kuweza kupeleka maji haya Ziwa Victoria kutoka Mwanza mpaka Kahama na Shinyanga na hatimaye kuyapeleka katika Mkoa wa Tabora. Naomba sasa kwa vyovyote vile Serikali yetu ijitahidi sasa kutuletea maji katika Wilaya yetu ya Mbogwe pamoja na Mkoa wetu wa Geita ili tuweze kufikia hatua ambayo kwa kweli itakuwa ni njema hasa kuwa na maji safi na salama ya kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua maji ni uhai. Ukiwa na maji safi na salama una uhakika wa kuwa na maisha mazuri kwa sababu magonjwa mbalimbali ambayo yanaangamiza maisha ya mwanadamu yanatokana na maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwa mfano typhoid, kipindupindu ambacho kimekuwa kikiwasibu Watanzania katika maeneo mbalimbali kinatokana na miundombinu mibovu ya maji. Wakati mwingine maji yanapokuwa hayawezi kupatikana wananchi wanapata shida namna ya kuweza kuyafanya mazingira ya makazi yao yawe salama, kwa maana ya kwamba maji ndiyo yanayoweza kuwasaidia wakati wa kusafisha mazingira yao. Wakati mwingine iwe ni katika kusafisha nyumba, viwandani au kusafisha mahali popote pale; na wakati mwingine hata katika kilimo cha umwagiliaji maji yanasaidia. Katika kuhakikisha kwamba mazingira yanakwenda sawasawa maji ni muhimu na ni uhai.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo,niombe tu kwamba Serikali yetu inapopata nafasi, kwenye maeneo yote ambayo kwa kweli tumejaliwa kuwa na maziwa; kwa mfano Ziwa Tanganyika, Ziwa Rukwa na Ziwa Nyasa, Serikali yetu ifanye kila linalowezekana pale ambapo rasilimali zinapatikana kuhakikisha kwamba, wananchi hawa wanapewa maji ya kutosha. Ili Tanzania ya viwanda iweze kupatikana ni lazima kwa kweli suala zima la maji lipewe kipaumbele cha kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi katika kuuliza swali niliuliza suala la kuwepo kwa mapori ya akiba katika nchi yetu hii. Mapori haya kimsingi bado sijaelewa vizuri, kwamba hivi Serikali ilipoyatenga mapori haya kuwa ya akiba ni kwa ajili ya baadaye kuyafanya yawe national parks au baadae yaje yawe maskani ya wananchi au makazi? Kama yametarajiwa kuja kuwa ni maeneo ya kuwa national parks na maeneo ya kuweza kuwafanya wanyama waendelee kudumu ni kwa vipi mapori haya yenyewe hayawezi kutengwa angalau sehemu fulani ikawa na eneo ambalo limehifadhiwa kwa ajili ya wanyama hawa wa kuzaliana ili waweze kupitisha kizazi hata kizazi na hatimaye waongezeke? Isije ikatokea kwamba baadaye hawa wanyama wakaisha tukaanza na sisi kuwa tunakwenda kufanya utalii katika nchi nyingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, inashangaza sana kuona kwamba wakati mwingine katika maeneo yetu kwa sasa kama pori la Kigosi Moyowosi kimsingi hayatunufaishi kwa vyovyote vile. Pori la Kigosi Moyowosi linafanyiwa ujangili, tembo wanauawa na hakuna habari ya asilimia 25 ambayo tulitakiwa tuwe tunapewa kama mchango kutokana na uwindaji. Shughuli hii kwa kweli haina maslahi kwetu na kwa maana hiyo ndiyo maana unaweze ukakuta watu wanaamua kuhamishia mifugo humo ndani angalau waweze kulisha mifugo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali, kama kweli ina nia njema ya kuweza kutusaidia, basi mapori haya iyaboreshe, iyawekee miundombinu na iyatangaze ulimwenguni huko ili kusudi watu waje kufanya utalii na hatimaye maeneo yetu ya Wilaya ya Mbogwe pamoja na Mkoa wa Geita basi yaweze kunufaika katika suala zima la utalii. Tunayo mapori mengine ya Kimisi, Burigi katika Kanda ya Ziwa, hayana mchango wowote hayaonyeshwi katika Serikali hii kwamba kuna mpango wa kuweza kuyaendeleza mapori haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali kwa kweli ijiangalie, katika mpango wake wa maendeleo unapokuja mbele huko tuone kwamba utalii uliokuwa umewekwa katika kanda ya Kaskazini basi uhamishiwe katika kanda ya ziwa kwa sababu tunalo pori lenye kilomita za mraba elfu 21, ni eneo kubwa hili, kama Serikali haiwezi kulijenga vizuri na kulifanyia miundombinu ya uendelezaji hatimaye watu watahamia katika mapori haya na mwisho lengo la kuyatenga haya mapori lisije kupatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, niseme tu kwamba kwa kweli suala la kiinua mgongo cha Wabunge waliangalie kwa jicho la pili kwa sababu sheria yenyewe iliyopo hapa ya viongozi wa kisiasa inatoa nafuu (msamaha) katika suala hili. Kwa hiyo, niombe tu kwamba, kwa sababu sheria ipo na iheshimiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme tena juu suala zima la kilimo. Kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa hili, naomba Serikali kwa kweli iangalie namna ambavyo mazao kama pamba…
Ohh! Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja.