Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa uhai kuwemo katika Bunge hili kuwawakilisha wananchi wa Jimbo la Kyerwa. Nichukue nafasi hii kipekee kukupongeza kwa kazi nzuri unayoifanya kwa ujasiri ambao umeuonesha kama mwanamke. Kwa kweli tunakupongeza na tunakuombea Mungu akupe nguvu, akupe afya na azidi kukuinua kila siku akupandishe juu zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kipekee kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi nzuri ambayo anaifanya ya kukusanya mapato. Kwa kweli kwa kipindi kifupi ameonesha kazi nzuri ambayo Wizara ya Fedha imeifanya na dhamira ya Serikali yetu kukusanya mapato. Kwa kweli nampongeza na nimtie moyo katika hili asitegemee atapendwa. Mtu yeyote ambaye anakusanya mapato, anakusanya kodi hapendwi.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Mheshimiwa Waziri asije akategemea atapongezwa, atabeba lawama nyingi sana. Hata hivyo, katika hili wale wanaoitakia mema nchi yetu ni vizuri tukaungana naye hata sisi Wabunge tukaendelea kuwahimiza wananchi wetu namna ya kuchangia Taifa letu kwa kukusanya kodi kutoka kwa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wengi sio walipa kodi na sisi Wabunge ambao tumepitia bajeti hii tunahitaji kuwapa elimu, tunaona mambo mazuri ambayo Serikali imeyapanga. Sisi tuwahimize wananchi wetu ili waweze kushiriki, kuendeleza uchumi wa Taifa letu kwa kulipa kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuongelea mikoa maskini. Kwa kweli ni jambo ambalo linasikitisha, nimekuwa nikifuatilia sana hii mikoa maskini ni mikoa ipi? Kwa mfano Mikoa kama ya Kagera na Kigoma, ni mikoa ambayo ina uzalishaji mkubwa. Kwa mfano, kama kule kwetu Kyerwa, sisi tuna uwezo wa kulima mara tatu kwa mwaka, kila zao kule linastawi, ni kwa nini tumekuwa maskini? Hili ni jambo ambalo ni la kujiuliza na nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha anapokuja hapa atueleze ni namna gani wamejipanga kuinua hii mikoa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukija kuangalia hii mikoa ambayo ni maskini ni mikoa ambayo ni kama Serikali imeitenga, Serikali haiihudumii, haiwezekani Mkoa kama wa Kagera ambao tuna kila kitu, tuna zao la kahawa ambalo ni zao kubwa leo tunaitwa mkoa maskini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejaza tozo kibao, leo Waziri wa Fedha hajatuambia hizo tozo wameziondoa halafu bado anatangaza hii ni mikoa maskini, hili halikubaliki. Kitu kinachofanywa na Serikali mimi nashangaa! Badala ya kuondoa hizi kodi, walichofanya wamejaza askari kila mpaka ili wakulima wasipeleke kahawa Uganda.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hamuwezi kuondoa hizi tozo zote waruhusuni wananchi wakauze kahawa wanakotaka. Lazima tujenge mazingira ambayo ni mazuri kwa wananchi wetu. Lazima tujiulize kwa nini hawa watu wanakwenda kuuza kahawa Uganda na sisi tutafute jibu ambalo litawasadia wananchi wetu wauze kahawa nchini kwetu, siyo tunajaza maaskari kila kona ili wazuie kahawa zisiende, hawa wananchi tutaendelea kuwafanya wawe maskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukija kuangalia mikoa hii, Mkoa wa Kagera sisi tuko nyuma, tuna maji mengi, tuna vyanzo vingi vya maji, lakini hatuna maji safi na salama. Ni mikoa ambayo imenyimwa miradi mikubwa ya maji. Ukija kwenye umeme kwetu Kyerwa miaka 50 ya uhuru sasa hivi ndipo tunaanza kuona umeme, umeme wenyewe uliokuja unawaka masaa mawili, huyu mwananchi tutamwendelezaje? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitegemea nione kwenye bajeti mikoa hii ambayo ni maskini ndiko tuweke miradi mikubwa. Mikoa hii ambayo ni maskini ndiyo imenyimwa barabara, hilo halikubaliki, kwa nini hii mikoa inatengwa kwani sisi sio sehemu ya Watanzania? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Mheshimiwa Waziri, hili waliangalie, lakini mikoa hii ambayo ni maskini huduma za afya ni duni, huyu mwananchi afya yake haiko vizuri ataweza kuzalisha vipi? Mtu anakwenda kuchota maji anakwenda kuanzia asubuhi mpaka saa tano, huyu mwananchi unategemea ataweza kuinuka? Haya mambo lazima tuyaangalie. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, nimwombe Waziri haya mambo ya kupeleka miradi wale walionacho wanazidi kuongezewa, sio sawa. Lazima tuangalie namna tutakavyowainua hao wananchi wetu ambao wana kipato cha chini. Katika hii mikoa, kwa mfano kama Kagera, tukiweka miundombinu vizuri, tukaweka mazingira mazuri tunaweza tukaliingizia Taifa mapato makubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwahiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri hili aliangalie na atuambie anapokuja hapa, suala la kahawa, sasa hivi ni kipindi cha msimu, wananchi wanahitaji kusikia kauli ya Rais aliyoitoa kwenye kampeni; akasema hizi tozo zote ataziondoa. Tunataka tusikie bei nzuri vinginevyo waacheni wananchi wakauze kahawa wanakotaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la bodaboda. Hawa Vijana wetu wanafanya kazi kwenye mazingira magumu. Leo tunawabebesha na kuwaongezea mzigo tena badala ya kuwaandalia kwanza mazingira ambayo ni mazuri waweze kufanya shughuli zao vizuri ndipo tutawaongezea kodi.
Unawawekea kodi wakati bado wako kwenye mazingira ambayo ni magumu, hili sio sawa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie vyanzo vingine ambavyo tunaweza kupata mapato, tuwawekee mazingira mazuri wananchi wetu ndipo twende tukawakamue. Wewe ng‟ombe hujamlisha halafu unaenda kumkamua atapata maziwa wapi? Mheshimiwa Waziri lazima aliangalie jambo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ni suala la Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Nasema hili jambo inawezekana ni mtego ambao aidha wamemtega Mheshimiwa Waziri ili kuzuia juhudi za Mheshimiwa Rais wetu za kutaka kuwabana mafisadi ndiyo maana mmepunguza pesa. Rais wetu ana nia nzuri ndiyo maana anasema mahakama tayari inakwenda kuanza, TAKUKURU wameipa pesa, lakini hili jicho ambalo linaona huyu mwizi limlete mahakamani wamelinyima pesa, hili jambo sio sawa. Vinginevyo Mheshimiwa Waziri, aidha waliomshauri wamemshauri vibaya ili wasimamishe juhudi za Rais wetu za kupeleka mafisadi mahakamani, lazima aongezewe pesa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo Mheshimiwa Waziri wamemshauri, hizi Sh. 50 za kuongeza kwenye mafuta, watu wanahitaji maji, hata kwake Kigoma anajua watu wanahitaji maji, watu wanahitaji zahanati, kwa nini anakuwa mgumu kuongeza hizi pesa? Hata Kamati ya Bajeti imeshauri kwa nini hakusikia? Hili ni jambo ambalo ni zuri. Sisi Wabunge leo tuko tayari, tunasema tukatwe hizo pesa wananchi wetu wapate maji, wananchi wetu wapate zahanati. Naomba alifikirie, vinginevyo Waheshimiwa Wabunge tusimame hapa tusiipitishe hii bajeti. Tunahitaji maji, tunahitaji zahanati, hali ni mbaya ndugu zangu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nitaunga mkono hoja pale ambapo atapitisha mambo muhimu. Ahsante kwa kunisikiliza.