Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili niweze kuchangia katika Mpango huu. Niseme kwamba Serikali haijajipanga, kwa sababu kwa muda mrefu tunakuwa na Mipango lakini haitekelezwi na inachosikitisha ni kwamba Waziri Mpango kama jina lake lilivyo, ndiye aliyekuwa anatuletea Mipango ya siku za nyuma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme, kwa kweli tatizo kubwa Tanzania inajulikana dunia nzima kwa mipango mizuri sana lakini haitekelezeki. Tulikuwa na mipango mpaka inachukuliwa na nchi nyingine inakwenda kutekelezeka lakini kwa kwetu ni tatizo. Vilevile tatizo kubwa ambalo naliona ni kwamba, hii Mipango haipimiki, haina viashiria ni jinsi gani inapimika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakwenda kwa mifano, ukiangalia kwenye suala la kilimo ni kwa kiasi gani wameweza kuoanisha Chuo cha Sokoine ambacho kinatoa wahitimu wa masomo mbalimbali ya kilimo na ni jinsi gani wamewahusisha na wakulima. Leo hii tukiulizwa takwimu za wakulima hapa Tanzania hatuzijui, wakulima wakubwa ni wangapi hatujui. Kwa hiyo, nadhani kuna haja ya Serikali kuchimba zaidi na kuona ni jinsi gani wanapata data za kuweza kutusaidia mipango yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mipango mingine inachekesha. Tunajua Tanzania ni nchi ambayo geographical location yake yenyewe ni uchumi wa kutosha, bandari ya Dar es Salaam ingeweza ku-serve nchi zaidi ya sita ambazo ni land locked, lakini kwa jinsi gani tunatumia bandari ya Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashindwa kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, leo tuna mpango wa kujenga Bandari ya Bagamoyo. Sasa unajiuliza hii ni mipango ya namna gani! Ukijenga Bandari ya Bagamoyo maana yake lazima ujenge na reli, kwa sababu huwezi kutoa mizigo bandarini kwa maroli, tunahitaji kuboresha bandari tulizonazo kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuboreshe Bandari ya Dar es Salaam, tuboreshe Bandari ya Mtwara na tuboreshe Bandari ya Tanga. Tukishaboresha hivi then kama tutapata pesa nyingi, ndiyo sasa tuanze mradi wa Bagamoyo. Kupanga ni kuchagua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nadhani Serikali ni lazima iweke vipaumbele vyake vizuri, kile kidogo tulichonacho tuhakikishe tunakitengeneza vizuri ili kuweza kuzalisha zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye suala la elimu na nazungumza kama Mwalimu na mdau namba moja wa elimu. Kumekuwa na pongezi nyingi sana hapa ndani za elimu bure, lakini ukisoma Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010 - 2015 na ya mwaka 2015 – 2020, katika suala la elimu anasema sasa tutafanya elimu iwe bora, ubora wa elimu. Hapo hapo unazungumzia ubora wa elimu, lakini unaongeza wanafunzi kibao, mwalimu hawezi kufundisha, darasa lililokuwa na watoto 70, leo lina watoto 200, hakuna nafasi ya mwalimu kupita kuona watoto wanasoma kitu gani!
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulisema na siku zote nasema kwamba, suala la elimu bure ilikuwa ni kwenye Ilani ya CHADEMA. Tunashukuru mmechukua, lakini tatizo mme-copy na ku-paste, bila ya kutuuliza hivi ninyi mlikuwa mtekelezeje? Kwa hiyo, hili ndilo tatizo. Hivyo, nawaombeni sana mje CHADEMA au UKAWA muulize ilikuwaje, mlikuwa mmepangaje! Msirukie rukie mambo tu. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania Education Authority (TEA), hili ni Shirika la Elimu ambalo kimsingi lingesaidia sana kuboresha elimu. Tulisema, pamoja na kwamba, tuna sheria ya kuunda hiyo taasisi ilikuwa itolewe 2% ya Bajeti ya Serikali ipewe hii Taasisi ili iweze kusaidia, lakini mpaka leo jambo hilo halijafanyika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala zima la Mpango. Mimi kama mwanamke niseme mpango huu Mheshimiwa Naibu Waziri wewe ni mwanamke, Waziri simuoni. Huu Mpango haujagusia kabisa masuala ya kijinsia kwa upana wake. Hakuna kitu chochote kimegusa jinsia, wakati tunajua Tanzania na dunia kwa ujumla, wanawake ni wengi kuliko wanaume. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tuitake Wizara ya Fedha na Mipango kuhakikisha kwamba masuala ya kijinsia yanaoanishwa katika huu Mpango. Jana alizungumza, sitaki kwenda kwa kina lakini niseme watoto wa kike wanashindwa kwenda shule. Kama kweli tunataka kuboresha elimu Mheshimiwa Waziri wa Elimu huko naye ni mwanamke anajua, watoto wa kike wanaanza wakiwa sawa au zaidi kwa idadi na watoto wa kiume wanapoanza darasa la kwanza, lakini unapofika sekondari watoto wa kike zaidi ya nusu hawapo shuleni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatokana na sababu kwamba tumeshindwa kuwasitiri watoto hawa kwa kuwapatia towel zao kila mwezi bure. Kwa sababu wenzetu Wakenya wanafanya hivyo. Kwa hiyo, nadhani hili ni suala la msingi sana kama kweli tunataka huo usawa hawa watoto wamalize darasa la saba, wafaulu wafike sekondari na huko wafaulu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la afya. Takwimu zinaonesha kuwa kila mwaka wanawake zaidi ya 8,500 wanafariki, hii ni sawa na mwanamke mmoja anafariki kila saa. Kwa hiyo naomba sana, suala la afya ni la msingi na ndiyo sababu narudia pale pale kwenye suala langu la asubuhi, kama kweli hii nchi ina kipaumbele na inapenda wananchi wake, Serikali isingethubutu kuleta magari 777 kwa ajili ya uchaguzi, yale magari ya washawasha ambayo nimezungumza asubuhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gari moja ni dola 250,000 mpaka 400,000 wakati mashine za CT-Scan na MRI bei yake ni hiyo hiyo na Hospitali ya Taifa kama Muhimbili haina, achilia mbali hospitali za mikoa. Sasa ni kwa nini hizo fedha hata kama ni mkopo zisingetumika kuleta CT-Scan katika hospitali zote za rufaa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndiyo nasema mipango yetu ndiyo hiyo mibovu namna hiyo. Saa nyingine unajiuliza hivi hawa watu wanafikiria kwa kutumia kitu gani! (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali iende ijipange vizuri, ituletee mipango yenye tija, mipango ambayo itahakikisha kwamba kweli inaleta maendeleo katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la utawala bora na niombe niungane na wenzangu wote waliozungumzia suala la Zanzibar. Uchaguzi wa marudio wa Zanzibar, utakwenda kutumia shilingi bilioni tisa kama ambavyo tumeambiwa, sijui zinatoka Zanzibar, sijui zinatoka huku, whatever the case, kama kweli tunaka kuboresha elimu, watoto wetu wanakaa chini, dawati moja ni shilingi 100,000/=, ina maana tungeweza kununua madawati... (Makofi)
MWENYEKITI: Ahsante sana.