Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niungane na wenzangu kukupongeza, kwa kutumia sheria, kanuni na taratibu za kuendeshea Bunge, na unaona amani ilovyorudi humu ndani. Ni mategemeo yangu kwamba wenzetu waliotoka humu ndani watakuja kukuona na mfikie muafaka warudi huku Bungeni turudishe heshima ya Bunge letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda vilevile kuungana na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote kwa kuja na mpango mzuri wa kutekeleza Mpango wa Awamu ya Pili wa Miaka Mitano, na bajeti ya kutekeleza mpango huo. Ninawapongeza kwa sababu, kwa kweli wameonesha kwamba kuna maendeleo ambayo tutayapata, lakini nina yafuatayo ambayo ningependa kusema.
Mheshimiwa Naibu Spika, msingi wa mpango wa miaka mitano wa pili ni viwanda na tuna bahati sana Mheshimiwa Rais mwenyewe amelisimamia hili, na amelielekeza Taifa hili kwamba hakuna sekta nyingine ambayo itapeleka nchi hii kuondoa umaskini na kutupeleka kwenye kipato cha uchumi wa kati. Ninampongeza, ninamshukuru na nina uhakika Bunge hili litamuunga mkono kuona kwamba viwanda vinasimamiwa na tutahamasisha uanzishaji wa viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa Waziri aone kwamba hamna namna ambavyo uchumi wa viwanda utanufaisha wananchi walio wengi Watanzania bila ya kupitia sekta ya kilimo. Ninaomba tusiiseme kisiasa, tuongee kwa vitendo. Pia ningeomba kwamba namna moja ya kuhakikisha kwamba viwanda vinakuwa ni kufanya kwamba kilimo kinakuwa cha kisasa. Azimio la Maputo tumeliridhia hapa lililosema kwamba tuitengee sekta ya kilimo asilimia kumi ya bajeti. Mwaka huu tumetenga asilimia 4.6; ninaomba kadri tunavyokwenda Mheshimiwa Waziri aone hili linafanyika ili tujielekeze kwenye vitendo zaidi ya kusema tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili ni kwamba kilimo hakitakuwa cha kisasa kama zana, kama mbegu, kama viuatilifu havitatiliwa mkazo. Watu wangu wa Hanang na Wilaya ingine wangependa kuona matrekta yanamwagwa kama namna ya kuboresha tija katika kilimo. Wangependa kuona mbegu zinapatikana kwa wakati na vilevile mbegu bora zinapatikana na mbolea nayo inapatikana. Ningependa kusema kwamba viwanda ambavyo vitapeleka nchi hii mbele na vitasambaza mapato kwa wananchi ni viwanda vya kusindika mazao ya kilimo, viwanda vya kusaidia tija kwenye kilimo kama viwanda vya mbolea na vilevile kuona kwamba masoko yanapatikana kwa kuhakikisha kwamba (a),(b), (c), (d) zinazotakiwa kwenye soko zinatiliwa mkazo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la kusisitiza ni Benki ya Maendeleo ya Kilimo, bila Benki ya Maendeleo ya Kilimo wananchi hawawezi kupata fedha za kuweza kuboresha kilimo. Ninaomba sana kila mwaka kama Serikali ilivyoahidi iweze kutoa zile fedha ambazo zitaimarisha benki hiyo. Kubwa zaidi ambalo lazima tulikumbuke ni kwamba bila ushirika imara, bila ushirika usioibia watu, kilimo hakitaendelea. Kwa hiyo, naomba sana tuone kwamba hayo mambo yametekelezwa ili kilimo kiwe cha kisasa kiwe bora kiweze kutoa malighafi na soko kwa viwanda ambavyo tunataka kuvianzisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 80 ya Watanzania wanategemea kilimo, kama unataka maendeleo ya watu kama Waziri alivyoandika kwenye mpango wa maendeleo, hamna namna ya kuleta mapinduzi ya viwanda kama kilimo hakitapewa uzito unaosaidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuliongolea ni kuhusu maji, ningependa kuungana na Wabunge wote kwamba tumeahidi kutua ndoo ya maji kutoka kwa wanawake wa Tanzania wakiwemo wale wa Hanang na hatuwezi kufanya hivyo bila ya kuwa na mpango madhubuti. Ninampongeza Waziri kwa sababu mwaka jana fedha zilizotengewa Wizara ya Maji ilikuwa shilingi bilioni mia nne na kitu, lakini mwaka huu tumefika bilioni 900 hata hivyo hazitoshi. Kwa hiyo ninaomba suala la kukata shilingi 50 kwa kila lita ya dizeli na petroli tuitilie mkazo jamani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, najua bei ya petroli ilivyokuwa juu mfumuko wa bei ulikuwa asilimia 6.2 leo mfumuko wa bei ni asilimia 5 .9 tofauti ni nini? na sidhani kama ni mafuta yameleta. Kwa hiyo, naomba hili tulitilie mkazo na Waheshimiwa Wabunge tunaishauri Serikali yetu kwa jambo jema, wakati huu ambako bei ya mafuta iko chini ndiyo wakati wa kuchukua fursa baadaye yakipanda hatuwezi kulifanya hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niongelee suala la logistic center ya Dar es Salaam. Naomba ni-declare interest logistic center ilianza wakati mimi nikiwa Waziri wa Viwanda na baadaye Waziri wa Uwekezaji. Tumetaka logistic center ili Dar es Salaam iwe Hongkong ya Afrika. Nawaambieni kwamba Dar es Salaam ina hinterland kubwa na hiyo hinterland ikitumika vizuri italeta manufaa makubwa. Naomba niwaondolee hofu, kufikiria kwamba bidhaa kutoka nje itafanya viwanda visianze, nataka niwaambie kwamba hilo siyo kweli. Kwa sababu bidhaa zitakazoletwa Dar es Salaam zikionekana zinanunuliwa Congo, Rwanda na kwingineko wawekezaji watakuja kuwekeza kwenye viwanda hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo logistic center ni mahali pa ku-test demand au mahitaji ya bidhaa ili kuwavutia wawekezaji wa viwandani. Kwa hivyo, tukitaka tujue bidhaa ambazo zitauzika haraka, na vipi viwanda ambavyo vitatengeneza bidhaa hizo ni lazima tuhakikishe kwamba logistic center ya Dar es Salaam inaanza. Ninataka niongelee vilevile kuhusu jamani mwaka jana Bunge lilitengewa hela nyingi shilingi bilioni zaidi ya 100 mwaka huu tumetengewa shilingi bilioni 99. Ninaomba sana kuona kwamba bajeti ya Bunge, ndiyo inayotuwezesha kutembelea miradi na oversight inayotakiwa. Kwa hivyo, kama zinatosha lakini tuhakikishe kwamba wajibu wetu wa kuwa Wabunge, unatekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningetaka kulizungumzia ni kwamba ningependa kusema kwamba takwimu za umaskini vina vigezo vyake, mkiwa mnabadilisha vigezo kila wakati, tutakuwa tunabadili mikoa ambayo ni ya umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakumbuka Mkoa wa Manyara ulitoka Arusha kwa sababu ulikuwa unaonekana kama umeendelea kutokana na Arusha na tukataka tugawanyike ili umaskini wetu uonekane. Mkoa wa Manyara ndiyo una Wahadzabe, Mkoa wa Manyara ndiyo una Wabarbaig wanaotembea nchi nzima. Mkoa wa Manyara ni moja ya Mikoa ambayo ni maskini na haina vyanzo vingi vya kuondoa umaskini. Ninaomba tuangalie vigezo hivyo, kama Pwani ilivyolalamika tuone kama kweli vigezo hivyo vinatufikisha kujua Mikoa ipi kweli ambayo ni maskini na tuchukue hatua ambazo zinatakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nirudie tena, naomba sana Bunge hili na Mheshimiwa Waziri tunamsihi aone umuhimu wa kuongeza shilingi 50 kwa kila lita ya petroli na dizeli kwa ajili ya maji na Wabunge tunalisema hili kwa ajili ya ushirikiano na Serikali siyo tunataka tupingane na Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno haya, naomba uvute uzi, uendelee kusimamia Sheria, uendelee kusimamia Kanuni za Bunge hili, uendelee kuona utaratibu unaleta heshima ndani ya Bunge hili na tunawasihi wale wenzetu ambao hawaoni umuhimu huo, hatimaye waone hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru na ninampongeza tena Mheshimiwa Waziri.