Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami ningeungana na wenzangu kuzungumza kama walivyozungumza. Hata hivyo, kwa kuwa tetemeko lililoanzia jimboni kwangu bado linatetemesha na bado linamtetemesha na Mbunge mwenyewe kwa hiyo naomba nijikite kwenye tetemeko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnavyofahamu tarehe 10/9/2016 saa tisa na dakika 27 mchana katika eneo lililo kilometa 27 Kaskazini Mashariki mwa Nsunga kulitokea tetemeko kubwa la ardhi. Eneo hilo si pengine bali ni Wilaya ya Misenyi katika Kata ya Minziro, Kitongoji cha Murungu B. Tetemeko hilo lilileta madhara makubwa na madhara hayo yameelezwa na Waheshimiwa mbalimbali waliochangia katika Bunge hili na viongozi mbalimbali walitembelea eneo hilo na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda niseme machache kwamba katika Mpango wa maendeleo tunaoupanga niungane na wale ambao wameshauri ingekuwa vizuri basi katika mpango huo tujipange pia jinsi ya kukabiliana na madhara hayo. Kwa mfano, katika Kitongoji cha Murungu pale tetemeko la ardhi lilipoanzia karibu nyumba zote zilienda chini. Kwa hiyo, matarajio ya wananchi makubwa waliyonayo ni kwamba, Serikali itaweka utaratibu mzuri na kuchukua hatua za kibajeti za kuwawezesha kuweza kujenga nyumba zao upya. Sasa linaweza kufanyika vipi, Waziri wa Fedha anafahamu Serikali inaweza ikatumia mbinu mbalimbali lakini hayo ndiyo matarajio ya wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baada ya tetemeko la ardhi kutokea lazima tujifunze. Jambo la kwanza ambalo ni muhimu tujifunze, tujipange kwa changamoto kama hizo zitakazotokea baadaye. Kwa sababu kubwa lililojitokeza ni kwamba tulikuwa hatujajipanga vizuri kwa sababu hakuna aliyejua kwamba tunaweza kupata tetemeko la ardhi, sasa limejitokea ni vizuri tujipange kwa siku zijazo likitokea tuwe tumejipanga vizuri. Inapochukua zaidi ya wiki tatu kufanya tathmini ya tetemeko la ardhi inakuwa ni majanga ndani ya majanga. Kwa sababu hata yule ambaye angependa kukusaidia haji kukusaidia kwa sababu wewe mwenyewe hujui tatizo lililokukuta ni lipi na hujui unatakiwa kufanya nini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya tetemeko la ardhi kutokea ilitolewa taarifa kwamba utaratibu wa kukusanya michango utaratibiwa, ni jambo jema. Pia utaratibu wa kutoa matamko baada ya kutokea tetemeko la ardhi na wenyewe unahitaji kuratibiwa kwa sababu kila mtu anapokuwa anasema analofikiri linaenda kwa wananchi walewale, tunapeleka taarifa za kuchanganya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kiongozi mmoja mzito baada ya tetemeko kutokea alisema kwamba wananchi wasiwe na wasiwasi watawezeshwa kupata vifaa kama cement pamoja na mabati ili waweze kujenga, wakafurahia. Baadaye likatoka tamko lingine zito kwamba hakuna atakayetoa
vifaa vya ujenzi bali wenye uwezo waanze kujenga na wananchi wakaanza kutuuliza Mheshimiwa Mbunge mnasema wenye uwezo tuanze na je, wasiokuwa na uwezo mnawafanyaje, sikuwa na majibu kwa kweli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini na mtaalam mmoja kiongozi akatoa kauli akasema tetemeko hili ni kubwa, tunafanya uchunguzi wa miamba, kwa hiyo msianze kujenga msubiri mpaka tukishajua miamba imekaaje huko chini ya ardhi. Mpaka leo nazungumza taarifa ya miamba ikoje chini ya ardhi haijatoka. Nayasema mambo haya kwa sababu tusipojipanga vizuri mbele ya safari yatatuletea matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia hata jinsi tulivyokuwa tukijitahidi kusaidia wananchi, nilienda kwa mfano upande wa Minziro kule nikakuta wananchi wengi walikuwa wanasaidiwa na wataalam wetu wa maafa kwa kupewa kitu kinaitwa sheeting. Wanasema nimefika pale nimekuta watu hawana nyumba, wataalam wanaeleza, tumetoa sheeting, sheeting ni turubai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kwenye kutembeatembea nikakuta maeneo mengine wana tents zimetengenezwa vizuri, nikawauliza nyie hizi mmetoa wapi? Wakasema jirani zetu hapa ambao ni ndugu zetu wametutolea hapa wanatusaidia kujenga na kila tent linajengwa kwa Sh. 70,000 na linakuwa limejengwa vizuri. Nikagundua kwamba wataalam wa maafa wa Tanzania wao wanachojua inapotokea maafa ni kugawa sheeting tu lakini hawachukui hatua kuangalia kidogo kwa wenzao wanafanya nini inapotokea matatizo kama yale. Si lengo langu kumlaumu mtu yeyote, lakini ni vizuri kujifunza ili siku zijazo tusirudie katika matatizo yale yale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia humu kwenye kitabu cha mapendekezo ya Mipango tunafikiri kwamba hali ya hewa itakuwa nzuri Afrika Mashariki lakini ukweli hali ya hewa si nzuri hata huko Kagera kwenyewe ninakozungumzia, kila mahali unapopita agenda kubwa ni ukame, kule Karagwe ni ukame, Misenye ni ukame na kila sehemu ni ukame. Kwa hiyo, matarajio yetu katika Mpango huu basi changamoto hizi za ukame zizingatiwe ili tuone tunaweza kufanya nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mipango yote mingi tuliyonayo katika kitabu hiki yako mambo mengi, wengi wetu huwa tunazungumzia fedha lakini tunalo tatizo lingine. Miradi mingi haitelezeki si kwa sababu ya fedha kutokuwepo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha alielewe hili, wakati mwingine fedha za kutosha zinakuwepo, lakini uwezo mdogo wa wale wataalam wetu tuliowapa majukumu kushindwa kusimamia hii miradi ni tatizo kubwa kuliko hata tatizo la ukosefu wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili nitatumia mifano miwili, kwa mfano tunao mpango wa SEDP unaeleweka Wizara husika ilitoa zaidi ya shilingi milioni 790 za kuweza kujenga nyumba za Walimu katika shule za Sekondari za Kashenye, Bwanja, Nsunga na Kakunyu. Wakandarasi wamefanya kazi yao vizuri, shilingi milioni 709 zilishatolewa, lakini juzijuzi nilikuwa kwenye ziara nimefuatilia kwenye Halmashauri yangu wakandarasi waliojenga nyumba katika sekondari nilizotaja wamelipwa tu shilingi milioni 600 zaidi ya shilingi milioni 200 hazijulikani ziko wapi, viongozi wote hawajui lakini kazi imefanyika, sasa hilo ni tatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna tatizo la mradi wa maji katika Wilaya yangu. Kwa mfano, tuna miradi ya maji mikubwa, kule Ruzinga tuna mradi mmoja wa maji wa shilingi milioni 567, Rukurungo, Igurugati shilingi milioni 400, Bugango, Kenyana, Kakunyu ni mabilioni ya fedha lakini miradi yote hii ukiitembelea unachokiona ni mabomba ambayo yanatoa hewa badala ya kutoa maji. Mabilioni ya fedha yametumika lakini hakuna maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mkutano mmoja wa hadhara mtaalam mmoja akaniambia Mheshimiwa tumepata maji mpaka mabomba yamepasuka. Nikamwambia hongera nitakuja unioneshe mabomba yalivyopasuka. Nikamuuliza mabomba mliyotumia yakapasuka yako wapi? Akasema Mheshimiwa ni haya hapa. Nikamwambia bomba hili haliwezi kupasuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mkutano tukachimba pale nikakuta bomba lililo ndani ya ardhi siyo kama lile alilonionyesha kwamba walitumia. Nikamwambia mbona bomba ni tofauti, akasema Mheshimiwa unajua sikuelewa swali ulilouliza. Kwa hiyo, umefanyaje? Akasema tumetumia mabomba yaleyale ya zamani yaliyokuwepo. Kwa maneno mengine wale wana Ruzinga hadi leo hawajapata maji na zaidi ya shilingi bilioni 2.7 zimetumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushauri wangu kwa Waziri wa Fedha na kwa Serikali ni kwamba, tatizo siyo fedha tu, tatizo pia ni kuwa na wataalam ambao uwezo wao ni mdogo. Lazima jambo hili tuliangalie, Serikali itupe wataalam wenye uwezo, kama hawajaenda shule sawasawa wapelekwe shuleni, hata kama ni kuazima popote pale tuazime tunachotaka ni utekelezaji wa yale mambo tuliyoahidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nilijibiwa hapa kwamba siku za karibuni kule Kajunguti International Airport wananchi wataanza kulipwa fidia na niliambiwa hapa kwamba kabla ya mwezi Oktoba watakuwa wamelipwa. Naomba nieleze masikitiko yangu kwamba hadi leo hii hakuna aliyelipwa hata shilingi moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.