Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia Mpango ulio mbele yetu. Namshukuru Mungu kwa neema na rehema zake kwangu na kwa nchi nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, napenda kwa unyenyekevu mkubwa kuwashukuru wananchi wa Ileje kwa kunipa ridhaa ya kuwa Mbunge wao, nawaahidi kuwa sitawaangusha na nitawatumikia kwa nguvu zangu zote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Naibu wake na Maofisa wote wa Wizara ya Fedha na Mipango kwa mwongozo mzuri na Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano na wa mwaka mmoja. Mpango uliowasilishwa ni mzuri, lakini nianze kwa kumtaka Mheshimiwa Waziri atueleze wananchi wa Ileje kuwa wao atawawezesha vipi kuingia katika uchumi wa nchi? Mpango wa Maendeleo unaotarajiwa umeweka vipaumbele muhimu vilivyomo ukurasa wa 23 hadi 25.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na viwanda; wazo la viwanda ni jema hasa ukizingatia kuwa kwa muda mrefu bidhaa zetu nyingi zimekuwa zikiuzwa ghali na kwa hivyo kuwapatia fedha kidogo sana wazalishaji. Bidhaa nyingi zimekuwa zikipotea kabla na baada ya kuvuna na hii pia husababisha upotevu wa fedha za uzalishaji, hii pia imesababisha wazalishaji kupunguza nguvu ya uzalishaji kwa sababu ya kukosa soko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika kupanga maendeleo haya ya viwanda ni lazima mambo ya msingi yatakayowezesha ujenzi na uendeshwaji wa viwanda hivyo yapewe kipaumbele hususan miundombinu ya barabara zinazopitika kwa mwaka mzima, miundombinu ya umeme wa uhakika unaopatikana mwaka mzima, upatikanaji wa maji na upatikanaji wa malighafi za kutosha. Hali ilivyo sasa hata viwanda vilivyopo vina changamoto nyingi za miundombinu tajwa hapo awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuzungumzia viwanda bila kuainisha mpango wa kuboresha kilimo, ufugaji, uvuvi na uchimbaji wa madini ya aina mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo makubwa ya uzalishaji wa kilimo ndiyo kwa kiasi kikubwa ambayo yana miundombinu mibovu sana. Nitoe mfano wa Wilaya ya Ileje, ambao tangu tupate Uhuru na tangu Jimbo lile lianzishwe miaka 40 iliyopita halijawahi kupata barabara ya lami hata moja ilihali Wilaya nyingine zote zinazoizunguka Ileje wana barabara za lami. Sasa kwa hali hii Ileje itawezaje kuvutia wawekezaji wa kilimo cha biashara, uvuvi na ufugaji ambao utaleta ujenzi wa viwanda? Naiomba Serikali iwekeze katika miundombinu ya barabara Ileje ili na sisi Wanaileje tujenge viwanda kuanzia vidogo, vya kati na vikubwa. Suala la miundombinu Ileje ni nyeti na ni la muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna umeme, barabara, masoko, kituo cha forodha, uhamiaji wakati kuna biashara kubwa sana ya mpakani na Malawi na ni njia ambayo ingekuza biashara kubwa sana na nchi jirani ya Malawi. Ileje ni Wilaya ambayo ingepata fursa sawa na Wilaya nyingine ingepiga hatua kubwa sana ya kimaendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo Ileje inahitaji ni kupimiwa ardhi ili wawekezaji waje kuwekeza. Ileje inahitaji kujengewa masoko na kituo cha mpakani kwa ajili ya kuendeleza vizuri biashara na nchi jirani za Malawi na Zambia. Ileje inahitaji taasisi za ufundi, majengo ya utawala na biashara ili Ileje isibakie kama kijiji kikubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazingatia kuboresha miundombinu yote na kuboresha kilimo, ufugaji na uvuvi, basi tuzingatie suala la kuwa wazalishaji wakubwa katika sekta hizi ni wanawake. Mpango huu uzingatie na ujielekeze katika masuala ya jinsia na makundi maalum. Tanzania ilishajiingiza katika mfumo wa gender budgeting, basi vipaumbele vyote vioneshe jinsi mipango hii inavyozingatia masuala ya kijinsia katika mikakati, katika bajeti zake ili wanawake, vijana, walemavu na wazee wawe sehemu ya Mpango huu wa Maendeleo. Nashauri Mpango huu uweke wazi mgawanyo huu ili makundi yote muhimu yashiriki kikamilifu katika maendeleo haya yanayotarajiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mpango unapaswa kuendeleza yale yote yaliyoanzishwa na Serikali kwenye kuleta usawa wa jinsia. MKUKUTA II, hasa ile cluster ya pili, Big Result Now ilizingatia usawa wa kijinsia. Je, hivi viko wapi sasa katika Mpango huu? Serikali ilikuwa imeshakuwa na mwongozo wa bajeti inayozingatia jinsia kwa Serikali za Mitaa, Serikali Kuu, Vitengo na hata BRN.
Mheshimiwa Mwenyekiti, chambuzi nyingi zilishafanywa kwenye sekta nne na kulikuwa na tamko la Serikali juu ya kila sekta kuainisha jinsi ambavyo imezingatia masuala ya kijinsia, takwimu zilitakiwa kunyumbulisha masuala ya kijinsia na labour force survey iliyofanywa ilionesha masuala ya kijinsia. Tathmini ya matumizi ya fedha za umma ilishafikiwa chini ya PER kama nyenzo ya kuhakikisha utekelezaji wa Mpango huu. Malengo ya milenia yalikwisha na sasa tuko kwenye SDGs ambavyo ni lazima ioneshe ni jinsi gani hayo yote yatashughulikiwa katika Mpango huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa takwimu kwenye maeneo yote muhimu kijinsia urekebishwe. Msingi wa usawa wa kijinsia ni muhimu kuhakikisha kundi kubwa la wanawake, vijana, walemavu, wazee na wanaoishi na VVU kuwa katika Mpango wa Maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, fursa za kuingiza masuala ya jinsia kwenye Mpango; kwenye utangulizi Serikali ingefanya marejeo kwenye Mpango wa Maendeleo kuhusu masuala ya kijinsia na miongozo tuliyojiwekea katika kuingiza jinsia katika mipango ya maendeleo.
Lengo la tano, kuwe na utambuzi zaidi wa umuhimu wa usawa wa kijinsia. BRN imeainisha kipengele cha jinsia na ufuatiliaji na kutathmini mpango mzima, Mpango unyumbulishe viashiria vyote kutumia hali ya uchumi jinsia, walemavu na wazee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumziwa idadi, ni muhimu tukazingatia kutamka kuwa mfumo una taswira hasi kwa wanawake. Idadi ya Kaya zinazoongozwa na wanawake zinaongezeka, bado hatujasimama katika nafasi nzuri sana katika masuala ya jinsia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda; je, Serikali imezingatia vipi suala la ujuzi kwa maana ya:-
(i) Elimu - usawa na jinsia, ufundi, vyuo vikuu, ajira rasmi;
(ii) Kilimo - kina sura ya mwanamke ambaye hana umiliki wa ardhi wala nyenzo za kisasa za kilimo, ufugaji, mitaji na kadhalika. Viashiria vya umaskini vina sura ya wanawake vijijini. Je, hili limezingatiwa vipi kwenye Mpango huu?
(iii) Ajira - 1.4; wanawake wasiokuwa na ajira; je, Mpango unalishughulikia vipi? BRN - sura iko kimya kuhusu masuala ya jinsia katika BRN, asilimia tano tu ya wanawake wanamiliki ardhi wakati asilimia 44 wanafanya kazi za uzalishaji;
(iv) Mikopo - wanawake wengi sana hawana fursa, mfumo wa fedha ni mfumo dume;
(v) Huduma za jamii; na
(vi) Ukatili wa kijinsia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vifo vya mama na mtoto, utapiamlo, kukosa haki zao za msingi, kukosa kujiamini na mila na desturi, ugandamizi na sheria. Kuwe na lengo mahsusi la kuzingatia masuala ya kijinsia ili kuzingatia juhudi zilizofanywa na Serikali kujielekeza katika mikakati, viashiria na rasilimali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Sura ya Tatu; mikakati yote haijanyumbulisha mtazamo wa kijinsia, kwa hiyo, lazima mikakati ioneshe jinsi wanawake, vijana, walemavu watakavyofikia malengo haya kwa kuwapa vipaumbele kwenye Mpango na kwenye bajeti tajwa. Kwenye kujenga uwezo, nini mkakati wa kuwajengea uwezo watendaji?
Mheshimiwa Mwenyekiti, follow up issues katika Wilaya ya Ileje; kwanza ni ujenzi. Barabara kuu tano zinazounganisha Ileje na Kyela inayotokea Kusumulu - Kyela kupitia Kata ya Ikinga na Malangali hadi Ileje Mjini. Barabara inayounganisha Wilaya ya Rungwe na Ileje inayotokea Mji wa KK Rungwe na Ileje, barabara inayotokea Mji wa KK na kuingia Ileje kupitia Kata za Luswisi, Lubanda, Sange na Kafule. Barabara ya kuunganisha Wilaya ya Momba na Ileje, inaanzia Mpemba na kupitia Kata ya Mbebe, Chitete, hadi Itumba. Barabara inayounganisha Wilaya ya Mbeya Vijijini na Ileje kupitia Mbalizi, kupitia Vitongoji vya Mbeya Vijijini hadi Itale, Ibaba na Kafule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia skimu za umwagiliaji; zilizopo Ileje ni Jikombe iliyopo Chitete na Ikombe iliyopo Itumba yenye banio, lakini mifereji haijachimbwa. Jikombe ilichimbwa lakini mifereji haijasajiliwa, hivyo mfereji umekuwa ukijifulia fulia. Skimu ya Sasenge imebakiza mita 2000 kumalizia usafishaji wa mfereji mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miradi ya maji; Mradi wa Ilanga, Mlale- Chitete inasemekana mingine inasubiri makabidhiano ingawa Malangali na Luswisi inahitaji marekebisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme wa REA; vijiji vilivyopata umeme ni 35 ambavyo umeme umewashwa ni vinne tu. Ileje ina Vijiji saba. Vijiji ambavyo havipo katika orodha ya kuwekewa umeme ni 25. Je, lini Vijiji vilivyopo kwenye orodha vitakamilishiwa na ambavyo havimo kwenye orodha vitajumuishwa lini?
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ardhi; Ileje imekuwa kwa muda mrefu ikikabiliwa na tatizo la watumishi katika sekta mbalimbali ikiwemo Maaafisa Tathmini (Valuers, Surveyors na Afisa Ardhi). Hii imeathiri kwa kiwango kikubwa upimaji ardhi na kutoa hati miliki kwa wananchi na wawekezaji wa viwanda, biashara na kilimo cha biashara. Hii inawanyima fursa nzuri za maendeleo wana Ileje na Taifa kwa ujumla. Lini Serikali itatupatia Wilaya ya Ileje Maafisa hawa muhimu ili kuharakisha upatikanaji wa hati hizi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kilimo, Ileje inalima kwa wingi nafaka zote unazoweza kuzifikiria, mazao ya mbegu za mafuta, matunda, mboga, pareto, kahawa, miti ya asali na pia ina fursa ya kulima cocoa, vanilla na mazao ya misitu. Kuna fursa ya ufugaji wa mifugo aina zote na nyuki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ileje inapakana na nchi jirani ya Malawi na Zambia, zaidi ya yote kwenye mpaka wa Tanzania na Malawi kuna kituo cha mpakani ambacho ni kichekesho! Askari wetu pamoja na Maafisa wa Uhamiaji wanakaa katika banda la ovyo, hakuna ofisi rasmi na isingekuwa mahusiano yetu mazuri na Malawi hawa wangeshindwa kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Uhamiaji iko katikati ya mji kwenye nyumba ya kupanga. Nafurahi kusikia kuwa, uhamiaji wana mpango wa kuja kujenga Chuo cha Uhamiaji Ileje na vilevile Kituo cha Forodha kinaenda kujengwa ili kihudumie mpaka na kuhakikisha biashara ya mpakani inafanywa kwa ufanisi zaidi kwa manufaa ya Taifa na wananchi wa Ileje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za jamii kama afya, elimu, maji na mazingira pia zizingatiwe. Kuhusu suala la Watumishi wa Umma; kuna upungufu mkubwa wa watumishi katika Idara ya Ardhi, Elimu, Afya na Mazingira. Hii imeathiri sana utendaji na ufanisi na kuzorotesha zaidi maendeleo ya Ileje. Watumishi wengi hawapendi kufanya kazi Ileje na hawaripoti kabisa na hata wakiripoti huondoka na kuacha pengo.
Kuhusu huduma za fedha, ni chache sana, Benki iko ya NMB na Tawi moja tu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha huduma za kifedha katika wilaya nzima?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hitimisho; ni dhahiri kuwa, kwa hali hii Wilaya ya Ileje itachukua miaka mingi sana kufikia uchumi wa kati kama hatua kubwa na za haraka hazitachukuliwa katika:-
(i) Ujenzi wa miundombinu.
ii) Upatikanaji wa umeme.
(iii) Upatikanaji wa maji.
(iv) Ujenzi wa shule, vyuo na taasisi za kiufundi kama uhamiaji, mamlaka ya kodi, taasisi za kifedha, taasisi za kuhudumia wanawake, vijana, wazee, walemavu na wanaoishi na VVU.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kusikia kutoka kwa Waziri, ni nini mkakati wake wa kutuhakikishia Wanaileje kuwa na sisi tutafikia katika uchumi wa kati. Naunga mkono hoja.