Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ya leo na ninakushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Kabla sijasema lolote basi, niunge mkono hoja hii kabla sijasahau. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1973 Wabunge wenye akili timamu, wenye uwezo walikaa pale Karimjee wakaamua kwamba Makao Makuu ya nchi hii yaje Dodoma na tangu kipindi hicho Marais waliopita wamefanya kazi kubwa, Rais wa Awamu ya Kwanza amefanya kazi kubwa, Rais wa Awamu ya Pili amefanya kazi kubwa, Rais wa Awamu ya tatu amefanya kazi kubwa, Rais wa Awamu ya Nne amefanya kazi kubwa na Rais wa Awamu ya Tano ameamua kutekeleza yale ambayo yaliamuliwa mwaka 1973.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania kwa ujumla pamoja na sisi wananchi wa Dodoma tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa maamuzi haya. Wametekeleza dhamira ya wananchi kwa sababu ukitoka hapa Dodoma mpaka Kagera unafika siku hiyo, ukitoka hapa mpaka Songea unafika siku hiyo, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa dhamira hii ambayo wameamua kuhamia Dodoma kwa awamu na sisi tunawaunga mkono na mimi niwaombe Waheshimiwa Wabunge ambao wana uwezo wa kujenga mahoteli, wana uwezo wa kujenga viwanda, wana uwezo wa kufanya miradi mbalimbali tunawakaribisha Dodoma. Kuna ardhi ya kutosha, barabara zinapitika, ukitaka kwenda Singida utakwenda kwa lami, Iringa utakwenda kwa lami, Arusha utakwenda kwa lami na Dar es Salaam utakwenda kwa lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona nianzie hilo kwamba tunaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano, lakini niombe kwa Serikali hii kwamba CDA waliopewa mamlaka ya kustawisha mji huu hawana fedha, wanatakiwa kujenga barabara, wanatakiwa kupima viwanja, wanatakiwa kuhakikisha kwamba squatter hakuna hapa, wanatakiwa kuhakikisha kwamba hakuna foleni kama Dar es Salaam lakini hawana fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu ambao umeletwa sikuona kama CDA wametengewa fedha yoyote kwa ajili ya kupanga Mji wa Dodoma. Nimeangalia katika kitabu chako ukurasa wa 51 kanda maalum ya kiuchumi sikuona kama Dodoma imewekwa katika kanda maalum kiuchumi. Kwa sababu watakaojenga viwanda katika Mkoa wa Dodoma watataka ardhi, lakini ardhi hii wanaipataje kama wenye ardhi hawatalipwa fidia, watapataje ardhi kama nyumba za wanakijiji hazitalipiwa fidia. Kwa hiyo, kuna haja ya kuweka Dodoma katika kanda maalum ya kiuchumi ili Serikali itakapoamua sasa kuhamia na wafanyabiashara mbalimbali watakapoamu kuijenga Dodoma basi iwepo fedha kwa ajili ya kutenga maeneo, iwepo fedha kwa ajili ya huduma mbalimbali, huduma ya maji taka, huduma ya maji, barabara, upimaji wa ardhi na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie sasa Mpango ambao uko mbele yetu. Nimeona kwenye Mpango maeneo mbalimbali yameainishwa na nimeona mazao ambayo yameainishwa ambayo yamepewa kipaumbele, lakini naona haitioshi. Hata mipango iliyowekwa kwa ajili ya miwa, tumbaku, mpunga, lakini bado mazao kama mbaazi, chai, korosho, bado mazao mengi ambayo nilitegemea kwamba Serikali itaonesha mkazo maana asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima. Lakini kama asilimia kubwa hii ya Watanzania hawatawekewa mkakati maalum hakika hatutafaulu kwa haya ambayo tunayategemea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahamasisha kujenga viwanda, lakini viwanda hivi ambavyo tunahamasisha kujenga tunategemea malighafi itoke ndani ya nchi yetu, lakini viwanda vingi ninavyoona vitakuwa vya mazao sio vya mazao ya mpunga tu au mazao ya chai au mazao ya korosho tu, lakini mazao yako mengi, lakini Tanzania wananchi walio wengi wanategemea mvua. Sasa katika karne hii ya tabia nchi inayobadilika kila siku ifike wakati kwamba tusitegemee mvua, lazima tuhakikishe kwamba kilimo cha umwagiliaji kinapewa kipaumbele katika mikoa yetu bila kujali mkoa huu una mvua au mkoa huu hauna mvua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea maeneo kama yale ya Rubada, maeneo ambayo Serikali ilitoa kwa ajili ya kilimo ili kuiwezesha nchi kuwa na mazao ya kutosha. Kule Kasulu kuna shamba kubwa karibu ya eka 10,000 au 5,000 wale wanaotoka Kasulu wanajua tungeweza kuendeleza yale mashamba na tukayagawa kwa wananchi au Serikali ikaona namna ya kuendeleza yale mashamba, ili tunaposema kwamba nchi iwe ya viwanda basi malighafi ipatikane nchini na Watanzania wafaidi kuwa na viwanda katika nchi yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Kilimo haina mtaji wa kutosha kutoa pembejeo au kuwapa wananchi pembejeo, lakini wako wananchi wengi ambao wangependa kulima, wangependa kukopa pembejeo, wangependa kukopa matrekta, lakini benki haina fedha. Na benki ina kituo kimoja tu, kituo kiko Dar es Salaam, ukimwambia mkulima wa Kagera, atoke Kagera, Mara, Kigoma kwa ajili ya kwenda kutafuta mkopo Benki ya Kilimo Dar es Salaam, hakika ni kazi kubwa na anapokwenda Dar es Salaam hana hakika kama atapata huo mkopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali yangu sikivu iangalie namna ya kuendeleza kilimo cha umwagiliaji, lakini ione namna ya kuwawezesha wakulima kusogeza huduma ya benki karibu nao. Nishauri pia kwamba miradi ile ambayo ilikwishaanza sasa ndio ikamilishwe kabla hatujaanza miradi mipya, kwa sababu tunapojirundikia miradi mingi wakati fedha hatuna za kutosha tunajikuta miradi mingi imekwama. Kwa hiyo, kuna haja ya kumaliza miradi ile ambayo tulishaanza, lakini tukatoa vipaumbele kwa miradi ambayo tunaona inaweza ikaisaidia nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia kwamba lazima tujue tunapotaka kuwa na viwanda umeme tunatoa wapi? Je, umeme upo wa kutosha nchini? Ifike sasa habari ya Mchuchuma na Liganga utoe megawatt 600 zile ambazo zimepangwa, lakini tunaweza tukapata wawekezaji wengi tusiwe na maji, tusiwe na umeme wa kutosha kwa hiyo, hata kuhamasisha kwamba, wajenge viwanda itakuwa ni kazi. Watajenga viwanda, lakini watakosa maji, watakosa umeme; kwa hiyo, mambo muhimu katika kuwawezesha hawa wawekezaji ni jambo muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini reli ya kati, ili kuhifadhi barabara zetu lazima tuwe na reli ya kati inayofanya kazi vizuri . (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema nimeshangazwa na maneno ambayo nimeyasikia kwa baadhi ya Wabunge. Kazi yetu Wabunge ni kuishauri Serikali, lakini Mbunge unaposimama na kusema matusi sidhani kama Waziri wa Fedha anaweza akaandika matusi hayo yanayosemwa. Unaposema maneno ya kejeli sidhani kama Waziri anaweza akaandika maneno ya kejeli katika kitabu chake cha Mpango. Kwa hiyo, kwa sababu kazi yetu ni kuishauri Serikali tusimame tuishauri Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakumbuka kuanzia mwezi wa nne mpaka mwezi wa sita Bunge lilikaa hapa kujadili Bajeti ya Serikali, lakini wapo wengine ambao waliweka plaster kwenye midomo yao, waliishauri Serikali wakati gani? Leo watu wanasimama wanasema tulishauri Serikali kipindi cha bajeti! Tulishauri Serikali hawakusikia! Mimi sikuwaona walioishauri Serikali zaidi ya Wabunge wa CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba tukubaliane na haya ambayo yapo kwa sababu bajeti hii ilijadiliwa na upande mmoja na tukakubaliana kwamba, haya ni sawa. Na leo watu wanachangia baada ya kuona bajeti iliyopitishwa na Wabunge wa CCM ni sawa. Ninaomba kazi yetu Wabunge ni kuishauri Serikali, tuishauri Serikali, tuache lawama, tuishauri Serikali tuache matusi, tuache kubeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwamba watu wanajua na tumeona katika Majimbo yetu baada ya kusema kwamba elimu ni bure, maeneo mengine darasa la kwanza waliandikishwa watoto 100, maeneo mengine watoto 200. Kwa hiyo, huwezi kusimama ukadharau hili kwa sababu wako wananchi ambao hawakuweza kuandikisha watoto kwa sababu ya michango ya shule. Tunakotoka wananchi wanashukuru kwamba sasa watoto wanasoma kwa sababu wanalipiwa michango na Serikali. Na ninashangaa kwamba wengine walisema vyama vyao vilisema kwamba wangelipa ada mpaka university, sasa tunalipa mpaka form four wanabeza, akutukanaye hakuchagulii tusi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wako ambao hawaangalii mbele, wanaangalia nyuma siku zote. Zamani watu walibeza wakasema Mheshimiwa Kikwete anachekacheka, Mheshimiwa Kikwete hawezi, leo wanasimama wanamsifu Mheshimiwa Kikwete. Hakika nadhani tuyatafakari na kuchambua yale ambayo tunaona yatalisaidia Taifa letu, tuyaweke yatusaidie katika kuendeleza nchi hii. Tunajua hali ya kodi katika nchi yetu, tunajua Wabunge wamesema, Serikali imesikia, Mawaziri wamesikia, Waziri Mkuu tunaye kwenye Bunge letu amesikia.
Mheshimiwa Waziri…
MWENYEKITI: Ahsante.