Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru kwa kunipa fursa hii kuweza kuzungumza machache mbele ya hoja hii iliyoko mbele yetu. Pili, nasema kwamba naunga mkono hoja hii kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, toka mjadala huu ulipoanza, Wabunge wote hasa Wabunge wa Kanda ya Ziwa walikuwa wanasimama mbele yetu na kila mmoja kwa hisia tofauti, kwa ukali na kwa uchungu sana wanazungumzia kuhusu reli ya kati. (Makofi)
Mimi Mwenyewe kama Waziri imenigusa sana na inaniuma sana jinsi gani ambavyo tunasimamia mpango wa ujenzi wa reli ya kati. Serikali vilevile inaliona kwamba hili ni jambo muhimu na tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba tutajenga reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mtandao wa reli ya kati unaotarajiwa kujengwa kwa kiwango cha standard gauge utakuwa na kilometa 2,560. Mtandao huu utajumuisha reli kati ya Dar es Salaam - Tabora - Isaka, reli kati ya Tabora - Kigoma kilometa 411; reli kati ya Uvinza - Msongati, kilometa 200; reli kati ya Isaka - Mwanza, kilometa 249; reli kati ya Kaliua - Mpanda - Kalema, kilometa 360; na reli kati ya Isaka - Keiza, kilometa 381; pia itakwenda reli kati ya Keiza - Rusumo na mwisho tumalizia kuunganisha na wenzetu wa Kigali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli kati ya Tabora - Kigoma, kilometa 411, zilifanyiwa feasibility study mwaka 2015 mwezi Februari na sasa hivi zimekamilika. Reli kati ya Kaliua - Mpanda vilevile zimefanyiwa feasibility study katika kipindi hicho. Reli kati ya Isaka - Mwanza, kilometa 249 zilifanyiwa feasibility study na kampuni ya Denmark na kazi ilikamilika mwezi Mei mwaka 2015.
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli kati ya Mpanda - Kalema na Uvinza - Msongati inafanyiwa feasibility study na kampuni ya HP-Gulf ya Ujerumani. Kazi hiyo ilianza mwezi Machi, 2015 na ikamalizika mwezi Desemba, 2015.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali iko katika mpango wa kutafuta pesa kwa ajili ya ujenzi wa reli ya kati katika kiwango cha standard gauge ambapo reli hiyo kama nilivyosema itaunganisha matawi niliyoyataja hapo juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na maoni kwamba tutumie Mfuko wa Reli kwa ajili ya kujenga reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge. Kwa taarifa tu, Mfuko wa Reli kwa mwaka tunapata shilingi bilioni 50. Ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge, kwa kilometa 2,561 itagharimu takribani dola za Kimarekani bilioni 7.5, sawa na shilingi trilioni 15. Hii inaweza kupungua ama inaongezeka, itategemea kama tutaamua tutajenga tuta jipya, pesa itakuja hii na tukiamua kuchanganya reli baina ya meter gage na standard gauge inaweza kushuka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kutumia Mfuko huu wa Reli, itachukua muda mrefu si chini ya miaka 300 kwa shilingi bilioni 50 ndiyo tuweze kupata trilioni 15. Kwa hivyo, Serikali sasa inaweka kipaumbele chake cha kwanza katika kujenga reli ya kati kupitia utaratibu wa ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu mwingine utakaoweza kutumika ni utaratibu wa ushirikiano baina ya nchi na nchi yaani Bilateral agreement ili kupata mkopo wenye masharti nafuu kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huu. Serikali imeona mradi huu ni muhimu na tutasimamia kwa nguvu zetu zote ili tuhakikishe kwamba reli hiyo ambayo ina manufaa makubwa sana kwa nchi yetu hasa upande wa Congo kule na upande wa Burundi iweze kujengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.