Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na mimi naunga mkono hoja ya Dkt. Mpango. Mimi nina maeneo matatu nataka nijielekeze, la kwanza ni kutoa ufafanuzi kuhusu landing fees kwenye viwanja vyetu vya ndege, la pili nitajielekeza kwenye bandari ya Dar es salaam na tatu nitajielekeza kwenye ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya Wabunge wamezungumza kwamba landing fees ya viwanja vyetu vya ndege iko juu sana, lakini ukweli wenyewe ni kwamba landing fees ya viwanja vya ndege vyetu vya Tanzania iko chini ukilinganisha na ya viwanja vyote katika region yetu. Hapa Dar es Salaam sasa hivi au Tanzania landing fees inakuwa ni kati ya dola tano mpaka dola tatu kwa ndege yenye uzito wa kilogramu 1,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Kenya hasa kiwanja cha Nairobi, Mombasa na Moi, wao kwa ndege yenye uzito wa kilogramu moja mpaka kilogramu 1,500 wanachaji dola 10. Kwa upande wa South Africa hasa kiwanja cha Johannesburg, Capetown na Durban kwa ndege yenye uzito wa kilogramu 1,000 wanachaji dola 7.52. Kwa upande wa Msumbiji viwanja vya Maputo, Bella na Nampula wanachaji dola 11.5. Kwa hiyo, viwanja vyetu hapa landing fees ni ya chini kabisa huwezi ukalinganisha na viwanja vyoyote katika nchi zetu za jirani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa ambayo sasa hivi Serikali inafanya ni ujenzi wa viwanja vyetu, sasa hivi tunajenga jengo la terminal three pale uwanja wa Dar es Salaam, tunajenga jengo la abiria huko Mbeya, tunajenga uwanja wa Mwanza na wiki inayokuja tutafungua tender au tutapata mkandarasi kwa ajili ya kiwanja cha Sumbawanga, Shinyanga, pia tutajenga jengo la abiria kwa ajili ya uwanja wa Kigoma na Tabora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko mbioni sasa kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Musoma, Iringa, pamoja na Songea. Tunaamini kazi yote hii tunayoifanya tuna hakika kwamba viwanja vyetu hivi vitachangia sana na nchi yetu itakua hub kwa ajili ya ndege kubwa za kimataifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa bandari. Ni kweli usiopingika kwamba mizigo kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam imepungua lakini siyo bandari ya Dar es Salaam tu. Kwa mfano bandari ya Durban - South Africa mizigo imepungua kwa asilimia 10, bandari ya Mombasa imepungua kwa asilimia 1.5 na bandari ya Dar es Salaam kwa ujumla imepungua kwa asilima 5.47.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sababu za msingi ambazo zilisababisha mizigo kwenye bandari ya Dar es Salaam kupungua. Ya kwanza wafanyabiashara wengi zamani walikuwa hawapendi kulipa kodi, sasa tumeendelea kuwabana na kila mtu analipa kodi na hivyo wafanyabiashara wengi sasa wamekimbia. Pili iliyosababisha hivyo ni kudorora kwa bei ya shaba duniani. Hiyo imesababisha mzigo kutoka Zambia kutokupita kwa wingi kwenye bandari ya Dar es Salaam na kusababisha mzigo wa bandari Dar es Salaam kushuka. Pia kuna matatizo kwenye uchumi wa dunia hasa China ambapo mizigo yetu mingi inatoka huko imesababisha mizigo vile vile kupungua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine kuna changamoto kwenye miundombinu ya reli ambayo haiko vizuri na hii imechangia sana katika kupungua mizigo yetu katika bandari ya Dar es Salaam kwani inachukua muda mrefu kusafirisha mizigo kutoka hapa kupeleka nchi za jirani. Pia kuna changamoto nyingine ambayo bandari yetu ya Dar es Salaam inayo. Miundombinu ya bandari ya Dar es Salaam si mizuri hasa kina cha maji, kuanzia bandari ya namba moja mpaka namba saba sasa hivi ina kina cha maji takribani mita 10 na kwa meli kubwa za kisasa inatakiwa takribani iwe na kina cha maji ambacho ni mita 14. Sasa tuna mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba tunaboresha bandari yetu ya Dar es Salaam kuhakikisha kwamba meli kubwa za kisasa zinaingia na zinaleta mizigo kwa wingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ya mwisho kuhusu reli, mchakato wa ujenzi wa reli ya kati unaenda, vizuri tumetangaza tender kwa lot ya kwanza, ambayo inatoka Dar es Salaam mpaka Morogoro, wakandarasi kama 39 mpaka sasa hivi wameomba, tunaamini tutakapofungua tender hiyo tarehe 6 Desemba watafikia wakandarasi kama 50 hivi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya pili tutaanzia Morogoro mpaka Makutopora alafu na lot ya tatu itaanzia Makutopora mpaka Tabora, lot ya nne itaanzia Tabora mpaka Isaka na lot ya tano itaanzia Isaka mpaka Mwanza ambayo kazi za tender kwa ajili ya kazi hiyo zitatangazwa wiki inayokuja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa, naunga mkono hoja asilimia mia moja.