Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia.
Mheshimiwa Spika, leo Bunge hili linakutana kwa pamoja kuamua kusitisha au kusaini Mkataba wa EPA. Lakini juzi wakati tunapata semina juu ya mkataba huu baadhi ya Wabunge tuliomba tuletewe watu wengine ambao waliufikisha mkataba huu mahali hapa ili waje kueleza uzuri wa mkataba huu. Ni bahati mbaya sana kwamba kilio hicho hakikusikilizwa.
Mheshimiwa Spika, mpaka hapa tulipofika, mambo yote haya yamefanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Leo hii kutuambia kwamba huu mkataba ni wa ajabu, ni mbaya, ni mchafu, ni wa kikatili na hili lenyewe nalo ni la ajabu. Ndiyo maana tunasema kwamba baadhi ya watu wanaposema kwamba Chama cha Mapinduzi kimechoka, kimezeeka, wanasema kwa sababu ya mambo kama haya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, inawezekana kabisa kwamba mkataba huu ukawa ni mbaya, lakini kuna faida kubwa kwenye mkataba huu ambazo hazijaelezwa na watoa mada. Kwa mfano, mkataba huu unatupa sisi kama nchi upendeleo maalum wa kupeleka bidhaa katika nchi za Ulaya bila kulipa kodi. Jambo hili halielezwi mahali popote na watu waliotoa mada. Binafsi inawezekana tukawa na maoni yanayokinzana, na ndiyo mjadala. Hoja ya msingi hapa ni nani aliyefikisha mkataba huu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mkataba huu ulijadiliwa katika Kikao cha Baraza la Mawaziri cha Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kabla mkataba kuingia kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki, ulipitia kwenye Kikao cha Makatibu Wakuu, baada ya Kikao cha Makatibu Wakuu mkataba uliingia kwenye Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Huu mkataba kabla ya kwenda katika Baraza la Afrika Mashariki ulipitia katika Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sasa watu wanakuja hapa leo kusema mkataba mbaya, mchafu kana kwamba nchi hii ndiyo kwanza inaanza upya, si sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni muhimu sana kwamba Bunge hili likaelezwa taarifa sahihi kutoka pande zote mbili. Upande unaopinga mkataba na upande unaotaka mkataba ili maamuzi sahihi yafanyike kwa manufaa ya Taifa letu. Tusifanye mambo ya ushabiki hapa. Tulipitisha miswada na sheria mbalimbali hapa za kuuza mabenki yetu, tukauza mashamba, tukabinafsisha lakini hao hao waliobinafsisha wamerudi wamesema uamuzi ule haukuwa sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni lazima na ni muhimu sana kabla ya Bunge lako Tukufu halijaingizwa katika mgogoro huu, wapatikane watu wa upande wa pili, wakaeleza uzuri wa mkataba huu ili Bunge hili liweze kuamua kwa maslahi ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Bunge limeelezwa kwamba nchi za Afrika Mashariki ikiwemo Kenya na Rwanda, taarifa zinasema hata Rwanda wameshasaini mkataba huu. Sasa kama sisi tuko kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kenya na Rwanda wameshasaini mkataba, sisi ndani ya Jumuiya hiyo tunabaki wapi kama kisiwa? Nchi za SADC ambazo zimeshasaini sehemu ya mkataba huu na sisi tumo katika Jumuiya ya SADC kama washirika wa biashara, tunakuwa wapi kama nchi hii? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jambo muhimu sana kwamba kabla ya uamuzi wa kufunga, kusaini au kutokusaini kwa mkataba, ni muhimu kwa maoni yangu kwamba huu mkataba haiwezekani wote huu kama ulivyo ukawa mbaya, haiwezekani. Haiwezekani kwamba dudu lote hili likawa baya kwa sababu watu wetu, wazalendo kabisa walitumwa kutoka Serikalini kwenda kushiriki kwenye vikao vya majadiliano hadi wakatengeneza kitu hiki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Bunge hili lingetoka na Azimio kwamba kabla ya mkataba huu kusainiwa vile vifungu ambavyo ni vibaya viondolewe tukajadiliane, vile vifungu ambavyo havifai viondolewe tukajadiliane, si kusema kitu chote hiki ni kibaya, tutaonekana watu wa ajabu duniani, yaani hata sisi kupeleka bidhaa zetu nje likawa jambo baya? Kwa nini tumejiunga na AGOA? Kwa nini kila mwaka tunapeleka maafisa kwenye mikutano ya AGOA? Ni kwasababu kuna vitu vizuri vimo humu ndani ya mkataba. Hivyo vitu vizuri hivyo, tuiagize Serikali ikafanye majadilinao upya ili vile vizuri tuvichukue na vibaya tuvitupe, si kusema kila kitu kibaya, haiwezekani. Haiwezekani kwamba vitu vyote vilivyomo humu vikawa vitu vibaya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo rai yangu ni kwamba Serikali ambayo iliingia mkataba huu, watalam ambao walishiriki mkataba huu, Baraza la Mawaziri ambalo limeshiriki mkataba huu mpaka kutufikisha nchi mahali kwenye njia panda, Mabunge ya nchi za wenzetu yamesharidhia, sisi tukiwa tuko nyuma hawa watu waliotumwa kwenda kusaini mkataba huu ni lazima wawajibike.
Waliokwenda kufanya mazungumzo ya mkataba huu, kama mkataba huu ni mchafu ni lazima wawajibike. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo hili lisichukuliwe kwa ushabiki. Sote hapa tunaweza tukawa Wazalendo, na hakuna mtu asiependa nchi yake lakini ni lazima tupime uzuri na ubaya.
Mheshimiwa Spika, siungi mkono hoja.