Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Ummy Ally Mwalimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa, lakini kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuleta hoja hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa maoni na ushauri. Katika hatua hii napenda kusema kuwa tumepokea maoni yenu na ushauri wenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya, masuala makubwa ambayo yamejitokeza katika michango na maoni ya Waheshimiwa Wabunge, kwanza ni suala la miundombinu ya utoaji wa huduma za afya na ni suala linalohusu ujenzi wa zahanati, vituo vya afya, hospitali za wilaya, hospitali za mikoa kwa mikoa ile mitano mipya, lakini pia na hospitali za kanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kulikuwepo na suala la rasilimali watu na hili linahusika kwa kiasi fulani na uhaba wa madaktari, wahudumu, wauguzi na wafanyakazi wengine katika sekta ya afya. Lilikuwepo pia suala la upatikanaji wa dawa, vifaa, vifaa tiba na kwa upande wa sekta ya maendeleo jamii, jinsia na watoto, masuala makubwa matatu ambayo yamejitokeza katika mjadala huu ni suala la kuwawezesha wanawake kiuchumi. Pia suala la elimu kwa watoto wa kike na suala la mainstream gender katika mipango yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nataka kuwathibitishia Waheshimiwa Wabunge wote kwamba katika suala la miundombinu ya huduma ya afya, tutajenga zahanati katika kila kijiji kama tulivyoahidi, tutaonesha katika bajeti yetu, ni zahanati ngapi tutajenga katika mwaka wa fedha 2016/2017; tutaonyesha ni vituo vya afya vingapi vitajengwa na Hospitali za Wilaya ngapi zitajengwa. Tutashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI kuhakikisha kwamba 2020 tunaporudi kuomba kura, Watanzania watatupa kura kwa sababu ya ahadi ya kuboresha miundombinu ya vituo vya afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la rasilimali watu juzi niliongea. Tunao uhaba wa wafanyakazi especially madaktari katika vituo vyetu vya afya kuanzia ngazi zote, uhaba ni karibu 52%. Kwa hiyo, bajeti inayokuja ya mwaka 2016/2017, tutajikita katika kuajiri watumishi wapya wa sekta ya afya, Mmadaktari, wauguzi na wakunga lakini pia tutaweka kipaumbele katika ile Mikoa tisa kama nilivyosema ambayo ina uhaba mkubwa ikiwemo Katavi, Geita, Simiyu, Tabora na Njombe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo tutalipa kipaumbele ni kuhakikisha kwamba tunatoa motisha kwa Madaktari kukubali kufanya kazi vijijini. Kwa hiyo, tutahakikisha tunajenga nyumba za madaktari, lakini pia tunataka sasa hivi daktari yeyote ambaye anataka kuongeza ujuzi kwa kutumia fedha za Serikali tutampa mkataba, ata-sign mkataba kwamba atakaporudi atakwenda kufanya kazi Katavi kwa miaka mitatu kabla hajaamua kuondoka katika Serikali, hili linawezekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la vifo vya akinamama wajawazito. Mimi ni mwanamke na nimepewa jukumu hili, nakubali ni changamoto kuona wanawake karibu 7,900 wanafariki kila mwaka kwa sababu tu wanatimiza haki yao ya uzazi. Kila saa moja tulilokaa hapa mwanamke mmoja wa Tanzania anafariki kwa sababu tu anatimiza haki yake ya msingi ya kuzaa. Nimedhamiria, tumedhamiria Wizarani hili suala tutalipa kipaumbele kuhakikisha vituo vya afya vyote vinakuwa na vifaa vya kufanyia upasuaji mdogo, maana wanawake wengi wanakufa kwa sababu wanakosa upasuaji, lakini suala la damu salama, suala pia la kuhakikisha kuna ambulance ili wanawake waweze kukimbizwa pale ambapo watapata matatizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie suala moja ambalo kwa kweli Mheshimiwa Edward Mwalongo amelizungumzia, vikwazo vya mtoto wa kike katika kupata elimu. Kwa mamlaka niliyopewa namtangaza Mheshimiwa Edward Mwalongo, Mbunge wa Njombe Mjini kuwa shujaa, champion wa haki ya mtoto wa kike kupata elimu kwa mwaka 2016. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tutampa tuzo rasmi ya Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii. Kwa mara ya kwanza katika Bunge hili, mwanaume anasimama, anatetea haki ya zana za kujistiri kwa mtoto wa kike. Hili jambo tumelisema, lakini limesemwa na mwanaume kwa kweli tumepata nguvu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Elimu mwanamke, Mheshimiwa Waziri anayehusika na Utumishi ni mwanamke, Mheshimiwa Jenista na mimi, tutalipigania kuhakikisha watoto wa kike wanapata taulo ili waweze kupata haki yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu.