Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu wa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya mwanzo kuchangia hoja hii. Kwanza niseme kwamba, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC na kwa sababu hiyo mengi nitakayozungumza yatahusu maoni na mapendekezo ya Kamati yangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kusema tu kwamba, matatizo mengi ambayo tumeyaona katika ukaguzi yanafanana kwa halmashauri zote. Nipende kuzungumza zaidi maeneo yanayohusu fedha za Serikali ambazo zinapelekwa katika Halmashauri zetu. Karibu halmashauri zote nchini, zinakabiliwa na tatizo la kutopata fedha za maendeleo kutoka Hazina kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo hili ni kubwa kiasi kwamba, karibu katika halmashauri zote, kuna miradi ya maendeleo au haijakamilika au iko nusunusu na kwa kweli karibu halmashauri zote zina madeni yanayotokana na wakandarasi kutolipwa fedha zao kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kucheleweshwa kwa fedha hizi kwenda kwenye halmashauri, hakuna sababu yoyote ambayo katika ukaguzi tumeambiwa, ambayo Hazina wanazieleza halmashauri na ndiyo maana tungependa kusikia kama Bunge, Waziri wa Fedha atuambie tatizo linaloikumba Hazina kutopeleka fedha kwa wakati kwenye halmashauri ni nini? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ndani ya Halmashauri kuna matatizo makubwa sana ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo. Tatizo la maji ambalo Wabunge wote tunalizungumza, kiini chake ni kwamba, baadhi ya miradi inayosimamiwa na Halmashauri haitekelezeki kwa sababu ya madeni. Siyo hilo tu, tatizo ambalo tunalipata la ukarabati wa miundombinu ya elimu, ukarabati wa barabara na kadhalika linatokana na shida hii hii ya Hazina kutopeleka fedha kwa wakati. Kwa hiyo ili kuzisaidia halmashauri zetu, ni lazima utaratibu uangaliwe wa kusaidia hizi halmashauri ziweze kutekeleza bajeti zake kwa Hazina kupeleka fedha kwa wakati katika halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lingine ambalo ni kubwa na linakabili halmashauri zote ni Maafisa Masuuli kuhamisha fedha za miradi ya halmashauri bila kufuata taratibu za fedha. Tatizo hili ni kubwa zaidi, kw sababu maagizo ya Viongozi Wakuu na Viongozi wa Mikoa na Wilaya yanakwenda kwa Wakurugenzi wakati kukiwa hakuna fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hili naomba nilieleze, halmashauri nyingi zimekuja mbele yetu, zimekumbana na tatizo hili, lakini ukiwauliza watakwambia tulikuwa tunatekeleza agizo la Rais kutengeneza madawati. Tumehamisha, tulikuwa tunatekeleza agizo la Rais, kujenga maabara. Maagizo haya yamesababisha uchochoro mkubwa sana wa wizi wa fedha za umma. Kwa sababu sasa fedha zinahamishwa bila utaratibu, bila kibali, bila maombi maalum, lakini ikuliza unaambiwa tulikuwa tunatekeleza maagizo ya kiongozi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa maagizo ya Mheshimiwa Rais, inavyoelekea na Marais wengine huko Mikoani, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na wenyewe wameingia katika utaratibu huu huu wa kutoa maagizo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo linalokumbwa zaidi na uchotaji wa fedha hizi ni asilimia 10, fedha zinazopaswa zitengwe kutokana na own source ya Halmashauri kwa vijana na akinamama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, agizo hili la kutenga asilimia 10 kwa ajili ya akinamama na vijana ni agizo zuri na lengo lake lilikuwa ni kuwasaidia akinamama na vijana kuweza kujiajiri. Vijana wengi wanaotoka vijijini kuja mijini wanakuja kwa sababu katika vijiji hawana kitu cha kufanya, wanajua kwamba, kule mijni ndiyo kuna kila kitu. Sasa kila Afisa Masuuli anayeulizwa ni kwamba, fedha za Mfuko huu wa Vijana na Akinamama zimekwenda kujenga maabara, zimekwenda kutengeneza madawati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kushangaza ziko Halmashauri ambazo zimetekeleza agizo hili bila kutumia fedha hizi. Kuna Halmashauri ambazo Wakurugenzi wake wamewahamasisha wananchi wamechanga kuku, mazao, wametekeleza agizo hili. Zile halmashauri ambazo Wakuu wake wamekaa hawatafakari, hawafanyi utaratibu wa ubunifu wa namna ya kutekeleza agizo hili ndiyo kwa kiasi kikubwa akinamama na vijana wa maeneo hayo, fedha zao zimechukuliwa kwa ajili ya kutekeleza haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kuna halmashauri nyingi ni maskini kwa maana zile fedha zenyewe haziwatoshi kwa ajili ya utekelezaji wa miradi yao ya maendeleo na kwa sababu fedha kutoka Hazina haziji wanaingia kwenye ushawishi wa kutumia hizi fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana tukasema lazima tuangalie utaratibu mwingine wa namna ambavyo fedha hizi vitawafikia akinamama na vijana kwa sababu lengo la kuwafikia akinamama na vijana bado lipo na litaendelea kuwepo na tunasema lazima miradi hii iboreshwe ili vijana wapate namna ambavyo wanaweza kujiajiri. Kwa sababu tunavyoona ni kwamba, uwezo wa Serikali hata na wa sekta binafsi kuwaajiri vijana wote na akinamama wote ni mgumu. Kwa hiyo, kama Serikali itaimarisha huu Mfuko kwa ajili ya kuwawezesha hawa vijana ni jambo jema, tena ni jema kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo fedha zinatumika vibaya ni ile asilimia 20, ambayo inatokana na kufutwa kwa vile vyanzo vya mapato ambavyo halmashauri zote zilikuwa zinatumia. Fedha hizi zinatoka Hazina moja kwa moja zinakwenda halmashauri ili halmashauri izitumie kwa ajili ya kupeleka kwenye kata na kwenye vijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri nyingi fedha hizi haziendi vijijini na wote tunafahamu jinsi ambavyo Viongozi wetu wa Vijiji, Viongozi wetu wa Kata wanavyofanya kazi katika mazingira magumu. Sasa hata hizi fedha ambazo Serikali kwa makusudi mazima iliamua ili kuwasaidia hawa ili kuweza kufanya kazi vizuri hazifiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hii asilimia 20 hakuna utetezi, vitabu vyote tulivyokagua, Hazina wanapeleka hizi fedha, lakini hizi fedha zikifika kwa Wakurugenzi wanazitumia jinsi ambavyo wao wanaona inafaa. Ndiyo maana kama umesikia hotuba yetu tumependekeza kwamba, Serikali itafute njia nyingine ya kupeleka hizi fedha zisipitie kwa Wakurugenzi ikiwezekana ziende moja kwa moja kwenye kata au ziende moja kwa moja kwenye vijiji, kama vile fedha kwa ajili ya elimu zinavyokwenda kwenye shule zinazohusika moja kwa moja.Vinginevyo, hili tatizo litaendelea kusumbua na wananchi hawatapata faida na hizi fedha hata kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine la mwisho, ambalo ningependa kulizungumza, ni kuhusu Sheria ya Manunuzi. Hili tumelipigia kelele katika Bunge lililopita na hata katika Bunge hili tumeendelea kulizungumza, ni vizuri Sheria ya Manunuzi ikaletwa kufanyiwa mapitio. Kwa sababu mpaka dakika hii kuna vifaa ambavyo vinaweza vikanunuliwa kwa bei ya soko lakini kwa sababu tu kwamba mkandarasi ametafutwa, bei ya vile vifaa inabadilika inakuwa mara mbili au mara tatu ya bei ya vifaa ambavyo viko sokoni, kwa hiyo, eneo hili linaziumiza halmashauri. Fedha ambazo zingeweza zikafanya kazi kiwango cha kuridhisha zinapunguzwa kutokana na matumizi mabaya ya Sheria ya Manunuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni ushauri wa Kamati kwamba, kwa sababu eneo hili litaendelea kusumbua, ni vizuri Sheria ya Manunuzi ikaangaliwa ili vile vifaa ambavyo vinaweza vikanunuliwa kwa bei ya soko, sheria ielekeze ili kupunguza mianya ya wizi inayotokana na matumizi mabaya ya hii sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa ni pendekezo; tumeongea na Wakurugenzi wetu na tulichogundua ni kwamba Wakurugenzi wengi sasa hivi ambao tunaongea nao, hawa wapya, maana huu ukaguzi ni ukaguzi uliotokana na hesabu za 2012/2013 – 2013/2014, sasa tutakwenda kwenye ukaguzi wa mwaka 2014/2015 na 2015/2016, ni vyema TAMISEMI ikaangalia uwezekano wa kukaa na hawa Wakurugenzi kuwapa kama semina hivi. Hili tumelisema sana, naomba lisibezwe, Wakurugenzi wengi tuliokaa nao uwezo wao ni mdogo sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunashauri kwa nia nzuri, uteuzi umeshafanyika, sisi hatuna mamlaka ya kuwaondoa lakini tunawashauri, hawahawa mliowateua kama mnaona wanafaa vizuri, lakini tafuteni namna ya kuwapa semina, namna ya kuwaongoza ili waweze kujua namna ya kutenda kazi, kwa sababu Wakurugenzi wengine hata taratibu za namna ya kuendesha Serikali hawajui, kwa hiyo ni kwa nia nzuri tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vinginevyo, ukaguzi unaokuja tunakwenda kuona hoja nyingi zaidi za ukaguzi kwa sababu ndogo tu kwamba, Wakurugenzi hawana uwezo wa kusimamia halmashauri a, wengine wako rigid hawataki kusikiliza ushauri kutoka kwa wakuu wa idara waliowakuta pale, wengine wanafikiri wanajua zaidi kuliko wale waliowakuta, wengine walikuwa wanaendesha NGOs zao huko sasa wamekuja kwenye utumishi wa Serikali wanafikiri uendeshaji wa halmashauri ni sawasawa na uendeshaji wa NGOs zao kumbe ni vitu viwili tofauti. Kwa hiyo, sisi tunawashauri kwa nia njema kabisa ni vizuri TAMISEMI wafanye semina ya hawa Wakurugenzi waweze kuongezewa uwezo wa kufanya kazi zao vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja zilizotolewa na Kamati zetu za Fedha.