Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ambayo iko mbele yetu na ni-declare interest na mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), nikiwa kama Makamu Mwenyekiti wa Kamati.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kabla sijaanza kutoa michango yangu nilitaka tuweke record sawa na hasa kuhusu taarifa yetu. Kilichosisitizwa kwenye taarifa yetu ni mafunzo kwa Wakurugenzi wapya. Taarifa yetu imeweka wazi kabisa kwamba hatuna maswali, hatuhoji uteuzi wa watu mbalimbali kutoka kwenye kada mbalimbali kwenda kwenye Ukurugenzi lakini watu hawa sasa wanatakiwa wapate mafunzo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, alivyofanya Mheshimiwa Rais kuchukua breed nyingine kutoka nje kupeleka kwenye utumishi wa umma na hasa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ni kitu ambacho ni kizuri na kinaweza kuleta matunda ambayo tunayatarajia. Kuna watu ambao wametoka kwenye private sector wakaenda kwenye mashirika yetu, kwa mfano Mkurugenzi wa Shirika letu la Nyumba, Ndugu Mchechu, anafanya vizuri, lakini ametoka kwenye private sector.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakurugenzi waliokuja mbele yetu wakati tunafanya mahojiano, wapo Wakurugenzi ambao wamefanya vizuri kabisa niwataje baadhi tu, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kiteto alifanya vizuri na alikuwa na miezi miwili tu ofisini; Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ileje, Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Mkurugenzi wa Tandahimba, lakini na Mheshimiwa Heche pale atakuwa shahidi, Mkurugenzi wa Tarime na yeye ni kijana mdogo, lakini ni mchapakazi vizuri na alionesha uwezo mkubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hii haikwepi jukumu la TAMISEMI kuwapeleka vyuoni hawa Wakurugenzi. Ukurugenzi ni kazi kubwa, kwenye council kuna idara na vitengo visivyopungua 15. Mkurugenzi huyu inabidi awe mganga, Mkurugenzi huyu ajue masuala ya elimu, Mkurugenzi huyu anatakiwa ajue masuala ya manunuzi, Mkurugenzi huyu anatakiwa ajue masuala ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni vema Wakurugenzi hawa pamoja na kubana matumizi, tuwaandalie programu maalum ili tuwapeleke kwenye Chuo chetu cha Hombolo wakapitishwe kwenye taratibu za kawaida tu. Kwanza waifahamu sheria ambayo imeanzisha Mamlaka ya Serikali za Mitaa, ile Sura ya 288, Sura ya 289, lakini na Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Sura ya 290, ili zikawasaidie katika kutekeleza majukumu yao, hicho ni kitu cha msingi sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna kitu hapa kimezungumzwa kuhusu mahusiano ya Wakurugenzi na Wakuu wa Wilaya. Kwenye mafunzo hayo wapitishwe kwenye Sheria ile ya Regional Administration Act ambayo wataona mahusiano kati ya Serikali Kuu na Serikali ya Mitaa. Kwa hiyo, naomba sana TAMISEMI pamoja na kubana matumizi mafunzo haya ni muhimu kwa Wakurugenzi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili ambayo napenda nichangie ni kuhusu udhaifu wa mfumo wa udhibiti wa ndani. Haya yote ambayo tumeyaongea hapa yangeweza kudhibitiwa kama tungekuwa na mifumo imara ya udhibiti wa ndani na hapa naomba niseme tu kwamba Ofisi ya Internal Auditor General ilifanya kazi sana miaka mitatu, minne iliyopita chini ya uongozi wa Ndugu Mtonga. Aliandaa mafunzo kwa Wakaguzi wa Ndani ili wakasimike mifumo ya udhibiti wa ndani kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme tu kwamba, mafunzo yale hayakuleta tija ambayo tulitarajia kwa sababu mafunzo yale yalilenga kwamba Wakaguzi wa Ndani wakirudi kwanza watengeneze kitu ambacho kinaitwa Risk Management Policy kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, watengeneze Risk Framework, lakini vilevile watengeneze Risk Register ambazo watakuwa wanazi-update kila mwaka kuangalia ni maeneo gani yana vihatarishi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa na haya yanaweza yakafanyika vizuri chini ya Internal Auditor.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitofautiane na wale ambao wanasema kwamba Internal Auditor anatakiwa ahamishwe, hapana. Internal Auditor ni jicho la karibu la Mkurugenzi Mtendaji. Ndugu zangu mimi nilikuwa mtumishi wa umma nilifanya kazi hiyo ya Ukurugenzi, Mkurugenzi ambaye anataka aone matokeo katika council yake mtu wake wa karibu ni Internal Auditor. Kuna Idara 15 kwa hiyo, atamsaidia Mkurugenzi katika Idara zake 15, Risk Department ni hi hapa kwa hiyo, Internal Auditor ni mtu wa karibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkurugenzi ambaye anataka matokeo atamuwezesha huyu Internal Auditor, atampa usafiri Internal Auditor kwa sababu hata Mkurugenzi akisafiri anajua kwamba kuna jicho lake la karibu ambalo ni Mkaguzi wa Ndani, lakini si vinginevyo kwa sababu watu wanafikiri kwamba kuwepo kwake huyu basi anaweza aka-collude na Mkurugenzi, hapana, Mkurugenzi ambaye anataka matokeo katika Halmashauri yake atamtumia vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba, TAMISEMI mlikuwa na utaratibu wa kuwezesha hivi vietengo, mlinunua magari, lakini magari yale yameenda kwenye Halmashauri chache. Kuna Mamlaka ya Serikali za Mitaa tumeongeza Halmashauri mpya, hawana yale magari hebu wezesheni kwenye zile Halmashauri mpya wapate magari kwenye vitengo hivi ili viweze kuwasaidia hawa Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala langu la pili ambalo nataka nichangie ni kuhusu udhaifu katika mikataba. Sehemu nyingine ambayo ina udhaifu katika Mamlaka yetu ya Serikali za Mitaa na CAG ameonesha wazi ni udhaifu wa kwanza uingiaji wa mikataba yenyewe katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, lakini pili na usimamizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana ulifanyika ukaguzi na CAG ametuonesha kwenye taarifa yake kwamba kwenye mikataba ya kukusanya fedha, kwanza Halmashauri hazifanyi assessment ya vyanzo vya mapato, yaani wanaingia mikataba na Mawakala wa Kukusanya Mapato bila kuangalia chanzo hiki kitapata Shilingi ngapi, na Halmashauri inategemea takwimu kutoka kwa Wakala. Hiyo ni taarifa mbaya sana kwa sababu Wakala anatafuta faida lazima atadanganya kwa hiyo, ni vizuri Halmashauri zifanye assessment ya chanzo cha mapato kabla ya kuingia mkataba na Wakala.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapo kwenye Taarifa ya CAG inaonesha kabisa kwamba kwenye Halmashauri 76 kuna fedha bilioni 5.3 Mawakala hawakuwasilisha, waliingia mikataba, lakini kwa sababu ya usimamizi mbovu wa mikataba fedha hizo wameondoka nazo Mawakala, Halmashauri hawakuzipata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine ambayo nilitaka nichangie kwenye hiyo hiyo mikataba, mimi naona TAMISEMI sasa mikataba kama hii ambayo inaonekana kwamba Halmashauri sasa imezidiwa hebu tuingilie kati mapema. Kwa mfano mkataba ule wa Oysterbay Villa na Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni, mkataba ambao hauna tija. Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni ina apartments 17 wamepewa, lakini hadi leo hawajapangisha na hawapati zile fedha. TAMISEMI mnatakiwa muingilie kati ili chanzo kile kisaidie kupata mapato ya Kinondoni kwa sababu, Kinondoni kama mmiliki amezuiliwa kuingia kwenye ule mradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mkataba mwingine ambao tuliona kwamba nao una mashaka ambao wenzangu mmeshasema ni ule wa UDA ambapo Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam ilipeleka barua kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Sasa tunaomba ule ushauri ambao ameutoa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ufanyiwe kazi ili zile fedha ambazo ziko benki zaidi ya bilioni tano zitumike kwa maendeleo ya wananchi wa Jiji la Dar es Salaam. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ni usimamizi wa matumizi ya fedha. Hapa naomba TAMISEMI ilivalie njuga suala hili kwa sababu Mamlaka ya Serikali za Mitaa imeonekana tena kuanza udhaifu wa kuanza hoja ambazo huko nyuma zilikuwa zimeshafutwa. Kuna hoja hapa kwenye taarifa ya mwaka 2014/2015 kwamba Halmashauri za Wilaya zimefanya malipo ya bilioni 10 na milioni 31 bila kuwa na viambatisho muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi hoja ni za kizembe, hizi hoja sasa tuna Mfumo wa EPICOR kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kwa nini hoja kama hizi ziendelee kuwepo? Kwa hiyo, naomba TAMISEMI muingilie kati ili uzembe kama huu usiendelee kutokea na watumishi ambao wanafanya uzembe huu wachukuliwe hatua mara moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile naomba sasa ule Mfumo wa EPICOR usimikwe katika halmashauri zote. Kuna halmashauri mpya ambazo mfumo wa EPICOR haujasimikwa bado. Kwa hiyo naomba TAMISEMI ihakikishe kwamba, inatenga fungu la kutosha, ili halmashauri zote sasa ziweze kufunga mifumo hii ya EPICOR ili na wao waweze kufanya hesabu zao kupitia mfumo huu badala ya kutumia mifumo ya kizamani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kuhusu uteuzi wa Wakuu wa Idara. Wakuu wa Idara kwa sheria iliyopo wanateuliwa na Mkurugenzi wa Halmashauri, lakini kuna mchakato, lazima waende kwenye vetting. Kwa hiyo, naomba mamlaka zinazohusika ziongeze uharaka katika mchakato huu, ili tusiwe na makaimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na ninashukuru kwa kunipa nafasi.