Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika mijadala hii miwili iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC kwa hiyo, nitajielekeza zaidi na Kamati hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya jambo kubwa sana wakati tukipitia hesabu za Serikali za Mitaa lililokuwa likijitokeza lilikuwa ni upungufu wa watumishi. Lakini nitajikita zaidi kwenye upungufu wa watumishi kwenye shule za sekondari, shule zetu za sekondari zina shida kubwa sana ya walimu wa sayansi. Katika Halmashauri zote ambazo tuliangalia vitabu vyake kila Halmashauri ilionyesha ina shida kubwa sana ya walimu wa sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke tumetumia nguvu nyingi sana kujenga maabara, lakini sasa lipo tatizo la walimu wa sayansi. Niiombe na niishauri Serikali kwa kadri nionavyo mimi na nguvu tunazozitumia kupata walimu wa sanyansi bado ni kidogo mno, hitaji la walimu wa sanyansi ni kubwa, walimu waliopo ni wachache sana na jitihada tunazoziweka ni ndogo mno ili kupata walimu wa sanyansi. Katika suala la walimu wa sanyansi tatizo kubwa ambalo limetufikisha hapa ni wana sanyansi wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema wana sayansi wenyewe, ukichukua mwanafunzi anayeingia kidato cha kwanza hajui chemistry ni nini hajui biology ni nini hajui physics ni nini. Lakini mwalimu anayeingia darasani anaanza kumfundisha na kumwambia haya masomo ni magumu sana. Sasa kitendo hicho moja kwa moja kinapelekea mwanafunzi aanze kujenga hisia kwamba masomo haya ni magumu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana sisi kama Wabunge, niiombe Serikali tutumie muda mwingi kuongea na wanasanyansi na waweze kuongea na wanafunzi kwamba sayansi sio ngumu na tangu hapo sayansi wala sio ngumu. Kwa sababu ugumu wa sayansi unakuja pale tu ambapo sayansi haina hadithi nyingi, ikiwa ni suala la formula ni formula, ikiwa ni Archimedes Principle ni Archimedes Principle, hakuna maelezo mengi wala nini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe sana tujitahidi sana na kama Serikali inaona inafaa ni bora ikaanzisha shule maalum za sayansi kwa maana ya kwamba tukianza na shule za sekondari specially school for science kwa hiyo pale tutajenga misingi mizuri, wanafunzi wale wataingia pale wakiwa wanajua kwamba wao ni wana sanyansi, huko mbele watatawanyika watapatikana madaktari, ma-engineer, walimu. Kwa hiyo tutakuwa tayari tumejenga msingi mzuri wa sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwendo tunaonenda nao sasa na upungufu wa walimu wa sayansi ambao upo, kwa kweli kuja kukamilisha na kuweza kumudu kuwa na walimu wa sayansi wa kutosha ni kama ni ndoto. Naomba sana Serikali ilione jambo hili ni gumu na ilione kwamba hili linatakiwa lifanyiwe kazi haraka sana ili tuweze kupata walimu wa kutosha wa sayansi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine kwenye suala la maabara, tulipokuwa tukipitia hesabu hizi na wenzangu wameseme uchochoro mkubwa wa fedha za Halmashauri umekwenda kwenye maabara, kila Halmashauri ilifika pale ikaeleza kwamba fedha imepelekwa kwenye maabara lilikuwa ni agizo la Serikali. Agizo la Serikali ni muhimu, kiongozi mkuu wa Serikali lazima aagize, asipoagiza huyo atakuwa ni kiongozi wa namna gani? Hoja inakuja watendaji hawa wanajua miiko? Kwa sababu pamoja na hayo maagizo wenyewe wamekurupuka tu wametumia mpaka fedha za kununulia dawa, wamechukua mpaka fedha ambazo zilikuwa za miradi ya maendeleo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana, sasa tufanye zoezi la muhimu la kupitia maabara hizi tujiridhishe kwamba viwango vya fedha vilivyoenda kwenye hizo maabara ni sawa sawa na ubora uliopo kwenye hizo maabara? Kwa sababu fedha yote katika Halmashauri wanasema imeenda kwenye maabara, kwa hiyo, ni vizuri tukaangalia sasa thamani ya fedha kwenye ujenzi wa hizo maabara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala la uwezeshaji wa vijana na akina mama. Lipo tamko ambalo linasemwa kwamba ni asilimia tano kwa akina mama na asilimia tano kwa vijana kutoka Halmashauri zetu. Lakini kama kweli tunataka kutatua tatizo la ajira kwa vijana wetu na kuwapa akinamama mitaji ya kujiendeleza kibiashara, naona asilimia hizo tunazozitaja hazitoshi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu moja, asilimia hiyo haipo kisheria, lakini pili makusanyo ni kidogo sana. Jambo lingine Halmashauri zina majukumu mengi kweli kweli ambayo yanawabana hawa wanashindwa kuyatekeleza, sasa kuja kumpa kijana ambaye yupo mtaani kumuita kumwambia kuna asilimia tano yako hapa na wewe kama Halmashauri una shida ya fedha inakuwa ngumu sana. Ndio maana tunaona Halmashauri zote hakuna Halmashauri hata moja ambayo imemudu kutoa hizo fedha kwa asilimia 100 kwa miaka yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iangalie utaratibu huu ikiwezekana ubadilishwe, uwekwe utaratibu mwingine ambao utaenda kwa uwiano mzuri na tutahakikisha kwamba vijana wetu na akina mama wanapata hizi fedha kwa utaratibu mzuri, vinginenyo tutakuwa tunatumia nguvu nyingi sana kuelekeza kwamba ni asilimia tano kwa akina mama na asilimia tano kwa vijana wakati kumbe uwezo wa Halmashauri ni chini sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunavyofahamu shughuli za Halmashauri ni nyingi sana sisi kama Wabunge tukija hapa Bungeni tukitoa maombi kwa Serikali kwamba kwenye Halmashauri yangu kuna shida hii, kuna shida hii Serikali inatujibu kwamba lazima iwe kwenye bajeti. Ukienda kwenye bajeti kuongea na watendaji pale Halmashauri jamani tuliingize hili na wao wanakujibu wanakuambia ukomo wa bajeti. Sasa hebu angalia mkanganyiko huu jinsi ulivyokaa ndio ufikie mahali useme kwamba asilimia kumi ikatolewe kwa vijana na akina mama haiwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana sasa Serikali ione hilo na ijaribu kuangalia kwamba tunafanya nini ili tuwe na utaratibu unaofanana kwa nchi nzima unaowezesha kutoa fedha kwa ajili ya vijana na kwa ajili ya akina mama, lakini hizi asilimia imeonyesha ni zoezi lililoshindikana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa nilizungumzie ni suala la asilimia 30 ya makusanyo ya ardhi ambayo Halmashauri mbalimbali zimekuwa zikikusanya na zinapeleka Wizara ya Ardhi. Wizara ya Ardhi hairudishi zile fedha kule Halmashauri na hairudishi kwa sababu inasema hawajaomba. Hivi jamani kuna sababu ya kuomba kwanini tunaweka bureucracy katika hili, wewe mwenyewe Wizara ya Ardhi ume-declare kwamba 30 percent itarudi council warudishie wape na maelekezo fedha yenu hii nataka mfanye hiki na hiki, kama kuna utaratibu wa kukagua kakague. Wizara ya Ardhi imerundika fedha zote kwake, hairudishi Halmashauri inasema hawajaomba na tunataka fedha hizi zikirudi zirudi kwenye maendeleo ya ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kweli Wizara ipo serious na inataka fedha zirudi kwenye maendeleo ya ardhi kwa nini isirudishe fedha na ikatoa na maelekezo halafu ikayasimamia maelekezo yake Halmashauri zikapata fedha. Kwa hiyo, unakuja kuona kwamba Halmashauri zinakusanya hii fedha na wakati mwingine Wakurugenzi wanajitoa, wanatoa mpaka matangazo lipia kiwanja chako kwa gharama za Halmashauri tukitegemea kwamba 30 percent itarudi lakini ardhi hairudishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niiombe Serikali irekebishe utaratibu huo badala ya kukusanya na kurudisha ibakize ile asilimia 30 kule kwenye Halmashauri ili zibakiwe na ile fedha kwa ajili ya maendeleo ya ardhi. Kama kuna maelekezo wanataka watu wa ardhi wayafanye wayatoe, wawape watu wa Halmashauri ili kusudi watekeleze huo mpango ambao Wizara inaona unatakiwa utekelezwe na Halmashauri kutokana na hilo fungu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni suala la East African Meat. Katika Jiji la Dar es Salaam walianzisha mradi wa kiwanda cha nyama pale Ukonga, lakini jambo la kusikitisha ni kwamba Halmashauri ya Kinondoni, Ilala na Temeke walichanga fedha pamoja na Jiji lenyewe kwa ajili ya kuanzisha huu mradi ya East African Meat, wakaweka na utaratibu wakaajiri na wataalam mchango ule kama mtaji walianza kulipana mishahara siku ile fedha ilipoisha na kampuni iliishia pale pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli huu ni utaratibu mbaya sana kwa watumishi wa umma kwamba Halmashauri zimechanga fedha, halafu mmeanzisha kampuni, fedha mliyoichanga kama mtaji mmelipana mshahara na maduhuli, safari na vikao vya bodi na nini halafu fedha imeisha kampuni imeishia pale.
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sasa Serikali iangalie suala hili, moja katika suala hili la East African Meat kuna suala la kiwanja kilichopo pale Gongo la Mboto. Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam inaanza kuonyesha kwamba kile kiwanja ni mali yake. Ninaishauri Serikali kile kiwanja sio mali ya Jiji kile kiwanja ni cha manispaa zote za Dar es Salaam. Kwa hiyo, Serikali ione na iweze kusaidia kuhakikisha kwamba katika mali kidogo iliyobaki ambayo ni kiwanja kilichopo Gongo la Mboto Halmashauri zote za Dar es Salaam zinanufaika nazo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikirudi tena kwenye suala la elimu naomba niseme jambo moja. Sasa hivi tumehangaika na maabara na madawati, lakini katika nchi yetu kuna kitu kigumu sana kinakuja kinaitwa elimu msingi na hii tumeshaanza kuitekeleza. Elimu msingi hii italeta ugumu zaidi kuliko wa maabara, kuliko wa madawati, kwa sababu itakapofika mwaka 2021 vijana walioko darasa la pili sasa watakuwa wamefikia kuingia kidato cha kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wataingia kidato cha kwanza wakiwa darasa la sita, watamaliza darasa la sita wataingia kidato cha kwanza. Kwa hiyo na hawa walioko darasa la tatu sasa na wenyewe watakuwa wanaingia kidato cha kwanza. Imani tunayojipa kama nchi ni kwamba tumefikisha zaidi ya asilimia 75 watoto wetu wanaenda sekondari. Lakini tukumbuke kwamba wapo asilimia 75 lakini wana uwezo kiasi gani? Wanatembea umbali gani? Sasa tunataka tupeleke asilimia 100.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali hebu tuunde Kamati za Wilaya za kulisimamia zoezi hili kusudi kila Wilaya iwe na mtazamo wa kuona jambo hili tutalikabili vipi litakapofika kuna shida kubwa ya madarasa, itatokea shida ya nyumba za walimu, itatokea shida ya mahali pa kuishi wanafunzi kwa hiyo lazima tuone. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke watoto hawa ni wa Watanzania wote unapomfikisha mwanangu darasa la sita halafu unamwambia anaenda form one umenielimisha kiasi gani mimi kama mwananchi? Ni vizuri elimu kwa wananchi ikaenda ya kutosha ili kusudi wajue kabisa kwamba vijana walioko darasa la pili sasa wataishia darasa la sita baada ya hapo wataingia kidato cha kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo maelezo haya yaende sambamba hata kwenye taasisi zisizo za Serikali zinazotoa elimu, matokeo yake tutakaa kimya itafika siku ya siku wale vijana wameshatekeleza huo mtaala mpya wa elimu wanaingia kidato cha kwanza kila mtu anashangaa. Wote tutakuwa tunashangaa kama vile tulivyokuwa tunashangaa kwamba kwanini shule zetu hazina madawati.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hili tunalifahamu na watu wote sisi ni waelewa hebu tulifanyie kazi likae vizuri kusudi fanya maandalizi ya kutosha tukijua kabisa kwamba sasa ifikapo mwaka 2021 vijana wote walioko shule ya msingi watakwenda sekondari, lakini watakuwa wanaingia sekondari wakiwa wamekomea darasa la sita. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba niseme nashukuru sana kunipa nafasi na naunga mkono hoja asante.