Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante sana kwa kunipa fursa ili niweze kuchangia katika hotuba iliyoko mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa kabisa ambacho nilitaka kuongelea ni kuhusiana na watu kukaimu kwenye Halmashauri zilizo nyingi ikiwemo Halmashauri yetu ya Wilaya ya Geita na mfano kwa sababu niko kwenye Halmashauri tangu miaka mitano iliyopita kwa hiyo ninaelewa hali halisi katika Halmashauri pengine na Halmashauri nyingine pia tatizo lipo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo sasa niombe tu Serikali suala hili iweze kuwachukulia kwa uzito sana, unakuta kwamba vijiji vingi kwa mfano katika jimbo langu kule wengi yani watendaji wa kata wanakaimu, sasa mtu anapokaimu atawezaje kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi? (Makofi)
Kwa hiyo nitumie fursa hii kuiomba Serikali ihakikishe iangalie namna kwenye vijiji ambako ndiko ambako tunapeleka shughuli za utekelezaji wa majukumu ya Halmashauri kwa sababu miradi yote inatekelezwa kwenye vijiji au kwenye kata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Serikali iangalie utaratibu mzuri kuona kwamba watu wanaokaimu basi waajiri moja kwa moja ili watu waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa. Wakifanya hivyo pengine itapunguzwa hata matumizi mabaya ya fedha ya Serikali, maana sasa kama mtu anakaimu anakuwa hana pia hata na uchungu maana hana uhakika na ile ajira yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ninaiunga mkono kabisa Kamati ambayo imelizungumzia kwamba watu wengi wanaokaimu katika ngazi ya Halmashauri, lakini vilevile kwenye kata na vijiji hili suala liangaliwe kwa umakini ili Serikali ione kwamba ni jambo la msingi kabisa kwamba watu wanapata, wanapewa fursa kama ni kukaimu basi iwe ni kwa muda mfupi baada ya hapo wapewe ajira za kudumu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, ni ile asilimia kumi ya mfuko kwa ajili ya wanawake pamoja na vijana. Katika Halmashauri zilizo nyingi jambo hili halitekelezeki, unakuta kwamba Halmashauri hizi zinafanya shughuli mbalimbali za maendeleo lakini wanapopata mapato yao hawawezi kutenga hizi fedha asilimia kumi kwa ajili ya akina mama pamoja na vijana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe kwamba basi suala hili pia litiliwe mkazo kuwepo na usimamizi muhimu ili kuona kwamba sera na taratibu na sheria za nchi zinafanyiwa kazi na zinatekelezwa kulingana na inavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuhusu udhibiti katika usimamizi wa mambo ya udhibiti wa ndani. Ina maana kwamba kama hatutaimarisha usimamizi wa ndani ina maana kwamba katika Halmashauri miradi mingi itakuwa inatekelezwa pengine chini ya viwango, lakini tukiimarisha udhibiti wa ndani hasa kwenye Halmashauri zetu mimi nina uhakika kwamba hata zile changamoto ndogo ndogo za fedha za miradi pengine kutekelezwa chini ya kiwango tutaweza kupunguza changamoto hii. (Makofi)
Mheshimiwa naibu Spika, kwa hiyo nitumie fursa hii kuiomba Serikali iweze kuimarisha kabisa vizuri tuweke wasimamizi ambao watakuwa na maslahi kwa ajili ya wananchi kuweza kuona kwamba kweli wanasimamia na kukagua, lakini pia kuishauri Serikali kupitia Halmashauri kuona kwamba kuna umuhimu mkubwa wa kuweza kufanya shughuli za maendeleo kulingana na fedha ambazo zinatengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna suala lingine la ruzuku kutokupelekwa. Ni kweli kwamba kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita kulikuwa na changamoto kubwa sana kwamba fedha tulikuwa tunatenga ndani ya Bunge, lakini mwaka unapita zilizokuwa zimepelekwa ni kiasi kidogo pengine chini ya asilimia 100 kwa hiyo zinakuwa chini pengine asilimia 60 au asilimia 50 jambo ambalo lilikuwa linapunguza pia utekelezaji wa miradi mbali mbali ya maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitumie fursa hii kuiomba Serikali iangalie sasa katika mwaka huu, hii ni awamu mpya na nimeona jinsi ambavyo tayari wamekwisha kuanza kufanya utekelezaji katika miradi mbalimbali kwa mfano kupeleka elimu bure kule wanapeleka zile fedha kila mwezi vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe basi hata katika bajeti ya mwaka huu tumetenga asilimia 40 ya bajeti iende kwenye shughuli za maendeleo. Serikali ihakikishe inatekeleza suala hili, hata mwisho wa mwaka tutaweza kuona jinsi ambavyo miradi mbalimbali ya maendeleo imetekelezeka kule vijijini kwa sababu Serikali imeweza kutekeleza wajibu wake hasa Wizara ya Fedha ambayo inahitajika kuweza kufanya utaratibu huu vizuri zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona jinsi ambavyo kuna mifano ya baadhi ya nchi ambao bajeti ya maendeleo ni zaidi ya asilimia 50, kwa mfano tu hata wenzetu hapa Kenya bajeti ya maendeleo inakuwa ni zaidi ya asilimia 50 na bajeti kubwa wanategemea mapato ya ndani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuishauri Serikali pia iangalie namna bora kwamba tuimarishe ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kuwezesha angalau asilimia 50 ya fedha za ndani ziwe zinapelekwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi. Tunashuhudia kabisa kwamba fedha nyingi za makusanyo zinatumika kwa ajili ya kulipa mishahara tu na gharama aina mbalimbali. Lakini kumbe Serikali iangalie utaratibu mzuri angalau yale makusanyo tukiweza yani angalau zaidi ya asilimia 50 zikaenda kwenye maendeleo, wananchi wetu wataweza kunufaika zaidi hasa walioko vijijini ambao wanazo changamoto nyingi sana katika huduma za jamii kwa mfano afya, elimu na masuala mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto hizi niungane tu pamoja na Kamati ambazo zimewasilisha hoja hii kuona kwamba Serikali lazima katika masuala haya yote iangalie namna ya kuyatafutia ufumbuzi ili wananchi waweze kunufaika na rasilimali ambazo Mungu ametujalia katika Taifa letu la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wote ni mashahidi nchi ya Tanzania tumejaliwa kuwa na rasilimali mbalimbali, madini pamoja na mazingira mazuri ambapo yanaruhusu watalii kuja katika nchi hii. Kusema ukweli tukijipanga katika ukusanyaji wa kodi tayari imekwisha kuanza taunaona impact tayari tunaona jinsi ambavyo Serikali inakusanya kodi vizuri kabisa naunga mkono kabisa ukusanyaji wa kodi na niendelee kusisitiza kabisa kwamba tujipange zaidi kwa sababu badi kuna watu pia ambao wanaendelea kukwepa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nichukue fursa hii kuiomba Serikali iendelee kuongeza ili makusanyo yawe makubwa zaidi kwa sababu kulingana na rasilimali ambazo Mungu ametujalia katika nchi yetu ya Tanzania. Kupitia mapato hayo nina uhakika nchi yetu sasa tutaweza kupata manufaa makubwa hasa katika wananchi wetu ambao tunahitaji kupeleka huduma kwa wananchi ili wananchi waweze kunufaika na huduma hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi walio wengi vijijini wana changamoto kubwa ya maisha yao. Vilevile tunashukuru kwa ajili ya TASAF ambayo imeanza kupeleka huduma kwa wananchi. Lakini niombe sasa pia kupitia TASAF tuangalie wale wahitaji kabisa, kwa mfano, wanawake walio wengi vijijini ambao wanalea watoto yatima lakini vilevile wana maisha magumu, kwa hiyo, tuangalie pia hizi fedha zinapokwenda za TASAF tuangalie kweli wale wenye uhitaji hasa walioko katika mazingira magumu zaidi vijijini.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nitumie sasa fursa hii kushukuru sana na kuomba Serikali iweze kuyazingatia yale ambayo Kamati imeweza kuyasemea ili kwamba basi wakishayafanyia kazi ninauhakika kwamba suala la maendeleo katika Taifa letu yataweza kuonekana.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.