Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie hoja iliyokuwa mbele yetu. La kwanza nijielekeze kwenye ukurasa wa 76 wa kitabu cha PAC. Kwanza nitangaze interest kuwa mimi ni Mjumbe wa PAC hasa kuhusu suala la muamala uliokwama wa shilingi bilioni 100 TAMISEMI. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hili kwa sababu ni suala mtambuka, TAMISEMI kama tunavyofahamu ni Wizara mama na inayobeba Halmashauri zetu. Tumewasikiliza Wajumbe waliotangulia wengi tulikuwa tunalalamika pesa haziji kwenye Halmashauri yetu kwa wakati, na tulikuwa tunatafuta mchawi ni nani? Katika hili ni vizuri Serikali ikachukua hatua stahiki kujua liko nini hapo Hazina, kwamba imetoa exchequer ya shilingi milioni 287 kwenda TAMISEMI, halafu wanarudisha nyuma shilingi bilioni 100 bila taarifa ya TAMISEMI wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, TAMISEMI wanaandika cheque kuwalipa wateja wao wanakwenda benki wanakuta hewa, na hili sio jambo dogo. Katika Bajeti ile ambayo ilikuwa ya shilingi milioni 287 ambayo pesa zilizoletwa hizi ni sawasawa na asilimia 47, maana yake nini? Kama asilimia 47 pesa hazikuja TAMISEMI ukizingatia hata bajeti yetu mpya ya maendeleo ni asilimia 40 hii mpya, hiyo ya zamani ilikuwa chini ya hapo. Ndiyo maana kumbe tunalalamika kwenye Halmashauri zetu pesa haziji tatizo liko huku huku kwa watoa fedha wenyewe. (Makofi)
Kwa hiyo, tunaomba sana Serikali yetu ya Awamu ya Tano, tuko pamoja kama alivyosema Mheshimiwa Rais alipokuja hapa Bunge tumsaidie na sisi Wabunge tuko tayari kumsaidia katika vita vyake vya kifisadi ili kuangalia hizi shilingi bilioni 100 ziko wapi. Kwa sababu bila kuchukua hatua stahiki mchezo huu utaendelea na hali itakuwa kama hivi, kila siku tutagombana, miradi haiendi, pesa haziji baadaye tunaweza kuweka rehani utekelezaji wetu wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni kuhusu NFRA kupata hasara ya shilingi bilioni 6.7. Hasara hii ni kubwa sana. Nakubaliana na sababu zilizotolewa na Kamati lakini kubwa ni kuchanganya biashara na siasa. Kuna watu wamesimamishwa, lakini binafsi nasema wamesimamishwa kiuonevu kwa sababu sio makosa yao. Ilipitishwa hapa kwamba uwezo wa NFRA kuhifadhi ni tani 140,000 kwa ma-godown yao yote, lakini baada ya NFRA kununua mahindi haya viongozi hawa hawa wa juu na sisi viongozi wa kisiasa kila mtu anataka mahindi yake yanunuliwe katika eneo lake na kutoa maagizo kwa viongozi wa NFRA wanunue bila kuzingatia uwezo wa kuhifadhi waliokuwa nao.
Leo mahindi yameharibika, tunawatoa kama mbuzi wa kafara wakati kimsingi siyo waliosababisha tatizo hili. Kwa sababu wasingetekeleza maagizo ya wakubwa wao waliyokuwa wanaambiwa kwamba lazima mahindi ya wakulima yanunuliwe bado wangetambuliwa tatizo lingekuwa liko pale pale. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika hili naomba Serikali ifanye uchunguzi hasa na kila mtu apate haki yake stahiki kwa sababu uwezo wa kuhifadhi ni tani 140,000 unamuambia mtu anunue tani zaidi ya 200,000, ataziweka wapi? Lazima aziweke nje na akiziweka nje mvua zikija lazima yaharibike. Sasa yakiharibika unakuja kumuadhibu wakati wewe ndiyo uliyemuelekeza kwamba anunue na hela umempelekea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hili nataka tu nilizungumze vizuri sana, Serikali siyo mnunuzi wa mahindi. Tunapowazuia wakulima wasiuze mahindi yao nje wakati tunajua uwezo wa kuzalisha mahindi Tanzania ni zaidi ya tani milioni tatu na uwezo wa Serikali kununua ni mdogo, kwenye bajeti mwaka huu tumetenga kununua tani 100,000, wewe utajihesabu ni mnunuzi? Matokeo yake wakulima wanaacha kuuza mahindi yao sehemu zenye wateja baadaye yanakosa soko, kipato cha wakulima kinaenda chini na kudhoofisha uchumi wa wakulima wetu. Kwa hiyo, naomba sana hata mwaka huu mnapokuja tena kununua hifadhi ya chakula tusije kuwazuia wakulima kuuza mahindi yao kwa wateja wengine kwa kusema Serikali itakuja wakati tunajua uwezo huo wa kununua mahindi yote ya wakulima wetu hatuna. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, niungane na maoni ya Kamati yangu hasa kuhusu suala la NSSF kwa sababu huu ni mfuko muhimu sana, ni mfuko wa wapigakura wetu, wastaafu wako huko, ni vizuri Bunge hili likaridhia Kamati hiyo ikaenda kujiridhisha na hali halisi iliyokuwepo huko NSSF. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ujumla kwa hatua stahiki ilizochukua kukabiliana na matatizo na changamoto zilizokuwepo ndani ya NSSF.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe angalizo sana hasa kwenye ule Mradi wa Dege kwa sababu ile ardhi mpaka leo bado ni ya Azimio kwa mujibu wa title, lakini pia kuna mkataba ambao NSSF umeingia na mbia wake. Kwa hiyo, suala hili siyo la kukurupuka, ni vizuri kujipa muda wa kutosha kuangalia kwa kina na kujiridhisha mikataba inasemaje ili siku za usoni tusije kuingia kwenye matatizo makubwa zaidi ikiwa tutakurupuka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia wote wanaotuhumiwa bado ni watuhumiwa tu, tusije kuwahukumu kama wakosaji wakati chombo cha kuhukumu ni mahakama. Wote tujipe subira kama Kamati yangu ilivyosema, twende huko tujiridhishe, iletwe taarifa ambayo imekamilika. Kwa sababu jambo hili bado liko kwenye uchunguzi tuviachie vyombo vingine vya uchunguzi viendeee kufanya kazi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho nataka kusema kwamba tumefanya kazi yetu katika mazingira ya kutegemea paper work na maelezo tu kutoka kwa management na Bodi tulizokutana nazo, lakini kiuhalisia PAC tumeshindwa kwenda kutembelea mradi wowote. Kama unavyofahamu siku hizi kuna watumishi hewa, wanafunzi hewa, tunaamini pia kuna miradi hewa. Kwa hiyo, ombi langu kwako kwa sababu tunakwenda kwenye mchakato wa bajeti ni vizuri bajeti ya Bunge ikaongezwa ili na bajeti ya PAC na LAAC zikaongezwa kuziwezesha kutembelea hii miradi tusije kuuziwa mbuzi kwenye gunia kwa sababu tunaweza kusema mradi fulani upo kumbe haupo. Ni vizuri tukatembelea miradi na mashirika hayo kwenda kujiridhisha zaidi. Pia tupate nafasi ya kutembelea hata makampuni au mashirika mengine ya umma yanayofanana na mifuko hii kwenda kujiridhisha kwa sababu mashirika mengi yanafanya mambo kama hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la mwisho niombe Serikali ifuatilie hii mifuko. Kwa mfano, NSSF wenyewe kama tunavyofahamu wana majengo mengi lakini cha ajabu majengo yao hawakai, wenyewe wanapanga, ni kitu cha ajabu kabisa. Wana majengo mazuri kwa nini wasikae kwenye majengo yao kuokoa fedha? Kwa hiyo, niishauri Serikali iwape mwongozo kwa sababu hivi vyombo vinasimamiwa na Benki Kuu na Mdhibiti wa Mifuko wawashauri NSSF na mifuko mingine yote warudi kwenye nyumba zao walizojenga wakae huko kuliko tafsiri ya sasa hivi inavyoonekana kwamba wanalazimika kwenda kupanga kwa sababu labda ya 10%. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye miradi ya uwekezaji, mifuko mingi kwa ujumla inawekeza….
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.