Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika mjadala wa Taarifa ya Kamati yangu kwa mwaka 2016. Michango mbalimbali mizuri imetolewa na naitaka Serikali sasa kujipanga na kuona namna bora ya kurekebisha kasoro nyingi zilizoainishwa na Waheshimiwa Wabunge ili kupunguza matumizi mabaya ya fedha za umma na kuongeza ari ya uwajibikaji katika Halmashauri nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na jumla ya wachangiaji 46 ambao wamechangia kwa hoja mbalimbali za Kamati yangu; kati yao 39 wakichangia kwa maneno na saba wakichangia kwa maandishi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia katika maeneo yaliyogusia matumizi yasiyozingatia Sheria ya Manunuzi ya Umma, upelekaji usioridhisha wa fedha kwenye Halmashauri kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, asilimia kumi ya mapato kutochangiwa katika Mfuko wa Wanawake na Vijana, Halmashauri kutopeleka asilimia 20 ya ruzuku kutoka Serikali Kuu katika Serikali za Mitaa na Vijiji na Marekebisho ya Sheria ya Manunuzi ya Umma kwa kuwa sheria hii inakinzana na hali halisi ya bei za bidhaa katika soko na mwisho uwezo mdogo wa kiutendaji wa baadhi ya Wakurugenzi wa Halmashauri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie uwezekano wa kutumia chuo cha mafunzo ya Serikali za Mitaa Hombolo kutoa mafunzo kwa Wakurugenzi wapya wa Halmashauri kama ilivyoshauriwa na Mheshimiwa Issa Mangungu, Mheshimiwa Godfrey Mgimwa na Mheshimiwa Abdallah Chikota. Pia Ndugu yangu Mheshimiwa Silinde alisema na kupendekeza kwamba ni vizuri sasa Serikali iangalie uwezekano wa kuwatumia watumishi wanaotokana na Watumishi wa Serikali ili iwe motisha chanya kwa wale Wakuu wa Idara katika utendaji wa kazi, maana kwa hali iliyopo sasa watumishi wengi katika Halmashauri ile ari ya kufanya kazi imeshuka sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, idadi kubwa ya Waheshimiwa Wabunge ilikuwa inaitaka Serikali itenge bajeti ya kutosha kwa Bunge ili Wabunge waweze kutekeleza majukumu yao kwa kuisimamia Serikali hususan kufanya ukaguzi wa miradi ya maendeleo badala ya kufanya vikao na mahojiano ya ana kwa ana na Menejimenti za Halmashauri hapa Dodoma. Kimsingi ukaguzi ni moja kati ya shughuli muhimu katika kuhakikisha kuwa kuna nidhamu katika matumizi ya fedha za umma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wamechangia hoja ya ufinyu wa bajeti ya Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi unaosababisha ofisi hii muhimu kushindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu. Hili limezungumzwa na ndugu yangu Mheshimiwa Khatibu na kusema kwamba Serikali inazibana Kamati za usimamizi wa fedha za Serikali, lakini inaibana Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi. Kwa hiyo, mimi situmii ile terminology nyingine aliyotumia Mheshimiwa Khatibu, ila niseme tu kwamba Serikali ilegeze kubana ili basi mambo yaweze kwenda sawasawa. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati za usimamizi wa fedha zinatekeleza majukumu yake kwa kutumia taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, lakini kutokana na ufinyu wa bajeti, mwaka huu CAG ameshindwa kutembelea baadhi ya Halmashauri kufanya ukaguzi na uthibitisho wa majibu ya hoja mbalimbali za ukaguzi. Ufinyu huu wa bajeti usipotatuliwa katika bajeti zinazokuja, kuna hatari ya CAG kushindwa kufanya ukaguzi kabisa na hivyo Kamati hazitaweza kuendelea na majukumu yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na michango mizuri inayohusu usimamizi mbaya wa mikataba na utekelezaji wa miradi ya maendeleo uliobainishwa na Kamati. Naamini kwamba Serikali imeliona hilo na italifanyia kazi hasa kuboresha usimamizi wa mikataba kwa kuwa miradi mingi ya maji katika mwaka wa fedha 2013/2014 na mwaka wa fedha 2014/2015 haikutekelezwa kikamilifu kwa sababu mikataba mingi ilivunjika kabla ya miradi kukamilika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Leah Komanya, Mheshimiwa Martin Msuha, Mheshimiwa Richard Mbogo kwa kutoa maelezo mazuri juu ya mfumo wa fedha wa EPICOR. Mfumo huu niseme wazi umegharimu Serikali fedha nyingi katika kuziunganisha Halmashauri nchini, lakini utendaji kazi wake hauna tija. Baadhi ya taarifa kwa mfano, taarifa za mali za Halmashauri zinaandaliwa nje ya mfumo. Ifikie wakati Serikali ione kuwa mfumo huu una changamoto nyingi na hivyo haufai kwa mazingira ya sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa sasa kupata taarifa za Halmashauri ni mgumu kwa kuwa vitabu vinavyowasilishwa huwa vikubwa mno na mapitio yake huwa magumu mno. Dunia ya sasa inaelekea katika mfumo wa nyaraka laini (electronic filing system). Hili limezungumzwa sana na Mheshimiwa Conchesta Rwamlaza kwamba Kamati inakutana na malundo ya vitabu ambavyo kuvifanyia upembuzi inakuwa ngumu sana. Hivyo Serikali iangalie uwezekano wa kuanzisha mfumo huu kwa Halmashauri nchini. Hii itapunguza hatari ya gharama za kudurufu vitabu hivi ambavyo ni vikubwa na mzigo mkubwa kwa Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mjadala baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walishauri Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani kuwa huru na kuwa kipangiwe bajeti ya kutosha ili kiweze kusimamia mwenendo wa fedha za Halmashauri. Wazo hili ni zuri kwa kuwa hata Kamati yangu ilibaini tatizo hili. Serikali iendelee kusisitiza kuangalia namna bora ya utendaji kazi wa kitengo hiki ili kulinda fedha za umma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Pauline Gekul alifafanua kwa undani namna bora ya Mfuko wa Wanawake na Vijana ambavyo unawabagua wazee ambao nao kimsingi wanayo mahitaji ya fedha kwa ajili ya mahitaji ya biashara ndogo ndogo na shughuli nyingine. Kamati iliona hilo na nichukue tena fursa hii kusisitiza uundwaji wa Sheria ya Mfuko huu ili kuongeza tija, ikiwa ni pamoja na kuangalia changamoto ambazo Kamati imeziainisha katika taarifa yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea pia mchango wa Mheshimiwa Zitto Zuberi Kabwe kwa maandishi kuhusu suala la Mfuko wa Wanawake na Vijana. Nakubaliana na wazo lake la kuangalia uwezekano wa Serikali kutumia mfumo wa hifadhi ya jamii ili kuhakikisha usalama wa fedha za umma. Kimsingi ushauri wake ni mzuri kwa kuwa una faida za ziada kwa wanavikundi; kama vile utaratibu wa kujiwekea akiba, kupata fao la Bima ya Afya na kupata fursa ya huduma ya SACCOS ili kupanua wigo wa biashara zao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, limekuwepo suala la Serikali kuchukua vyanzo vya mapato vya Halmashauri kama vile ushuru wa ardhi na ushuru wa nyumba. Waheshimiwa Wabunge wengi waliochangia wamelalamikia suala hili la Serikali kukusanya ushuru wa ardhi na kutopeleka asilimia 30 katika Halmashauri kama ilivyokubaliwa. Niseme wazi, ushuru huu umefikia wakati kwamba Serikali lazima irudishe katika Halmashauri ili kuongeza wigo wa mapato na kuzipunguzia utegemezi wa ruzuku kutoka Serikali Kuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wengi waliochangia taarifa yetu, wameshauri Halmashauri kufuata utaratibu katika kutekeleza maagizo kutoka Serikalini. Suala la ujenzi wa maabara limegharimu miradi mingi na Kamati ilibaini kuwa ni moja kati ya sehemu zenye walakini mkubwa katika matumizi ya fedha za Serikali. Sasa lipo suala la utengenezaji wa madawati ambalo pia ni agizo kutoka Serikali Kuu. Naendelea kusisitiza kuwa Halmashauri zifuate sheria, kanuni na taratibu za fedha katika kutekeleza maagizo yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nawashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika taarifa yetu na Kamati inataka Serikali kuleta majibu kwa maandishi juu ya utekelezaji wa yale yote ambayo Kamati tumeyaazimia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho basi niombe sasa Bunge lako Tukufu lipokee na kukubali taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa pamoja na mapendekezo yote yaliyomo katika taarifa hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.