Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Waziri wa Fedha na timu yake kwa kutuletea mapendekezo mazuri ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/2018. Naomba kuchangia suala zima la kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu. Naomba niishauri Serikali yangu Tukufu tufungue viwanda vidogo vidogo ambavyo malighafi zake zinapatikana hapahapa nchini hasa kwa wakulima wetu. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa tumeongeza mnyororo wa thamani katika mazao yetu pamoja na kuongeza ajira kwa wananchi wetu. Pia pembejeo zifike kwa wakati kwa wakulima wetu na pia wakulima wa mbogamboga na matunda nao wapewe pembejeo za ruzuku kwani wakulima hawa wanachangia sana Halmashauri zetu kwa kulipa ushuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali yangu Tukufu kuwe na mkakati maalum kuhusu suala zima la maji. Suala la maji lingefanywa kama suala la madawati lilivyofanywa tungemaliza tatizo la maji kabisa hapa nchini na kusahau kabisa tatizo hili la maji. Hili ni tatizo kubwa sana hapa nchini na kila Mbunge aliahidi kutatua tatizo hili. Naamini kabisa kama tatizo hili halijatatuliwa, Wabunge wengine tutashindwa hata kurudi majimboni kwetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto kubwa sana katika suala zima la huduma ya afya upande wa dawa pamoja na kutokuwa na vituo vya afya na zahanati hasa wananchi wanaoishi vijijini wana hali mbaya sana. Sisi kama Wabunge tumehamasisha suala la CHF na wanaelewa na kuchangia, lakini wanapofika hospitali wanakuta hakuna dawa zaidi ya kuambiwa wakanunue dawa katika maduka binafsi.
Mheshimiwa Naibu Spika, maliasili na utalii, naomba niishauri Serikali yangu Tukufu kuhusu suala zima la misitu yetu kuchomwa moto kila siku hali ambayo husababisha uoto wa asili kutoweka na maeneo ya misitu kubaki vichaka. Nashauri Serikali inunue ndege kwa ajili ya kuzima moto katika misitu yetu inayopata majanga ya moto hasa ikizingatiwa jiografia ya misitu mingi kuna maporomoko makubwa ambayo watu hawawezi kuzima moto unapotokea. Pia maeneo yote yaliyoungua Serikali ipande miti ili kurudisha mandhari ya msitu husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na unyanyasaji mkubwa sana hasa kwa mama ntilie, bodaboda, akinamama wanaouza mbogamboga na matunda pamoja na watu wenye ulemavu. Halmashauri zetu hasa Wakurugenzi wanawatoza ushuru watu hawa bila huruma pamoja na kuwatolea maneno yasiyofaa, kubwa zaidi kuwaongezea ushuru kila uchao. Niiombe Serikali yangu Tukufu iwaonye Wakurugenzi hawa ili wasiendelee kuwanyanyasa wapiga kura wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, sisi Wabunge tunapowaambia Wakurugenzi hawa wanatudharau na kutuita wanasiasa hatuna lolote. Kwa hiyo, niishauri Serikali yangu sisi Wabunge tunapoleta matatizo ya Wakurugenzi, tunaomba yafanyiwe kazi haraka na ikiwezekana mhusika achukuliwe hatua, zaidi ya hapo, majimbo yetu yatakuwa hatarini kuyakosa. Kibaya zaidi Wakurugenzi wengi ni wanasiasa pamoja na hayo wanarubuniwa na baadhi ya wanasiasa walioshindwa ili amharibie Mbunge ambaye yupo madarakani ashindwe au aonekane hafai.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mazao ya biashara kama pamba, kahawa, korosho, tumbaku pamoja na katani. Mazao haya yamesahaulika wakati ndiyo yanatoa pato kubwa katika Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali yangu Tukufu kuhusu TRA. Mzigo unapoingia kutoka nje huwa unatozwa ushuru/kodi, ukitoka bandarini ukifika sehemu kama Kariakoo, TRA tena wanachukua kodi, ukipakiwa kwenda mikoani TRA wanachukua kodi, mwisho wa siku biashara hii inamfikia mtumiaji kwa bei ya juu. Kwa hiyo, niishauri Serikali ipunguze mzigo huu wa kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna suala la motor vehicle licence, huwa inakatwa au inalipiwa kila mwaka lakini kuna watu wana magari ambayo yameharibika kwa muda mrefu mpaka limefikia kuchakaa mtu anaamua kuliuza kama skrepa. Cha ajabu mtu huyu anapofika TRA kwa ajili ya kuripoti ili arudishe kadi ya gari anaambiwa unadaiwa lazima ulipe, hii inasumbua sana watu wengi na ukizingatia walio wengi hawana uwezo tena. Kwa hiyo, niishauri Serikali iliangalie suala hili upya ili wananchi wetu ambao hawana uwezo wasije wakachukua maamuzi ambayo hawajayapanga na kama kuna uwezekano ifutwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nimtakie Waziri afya njema pamoja na timu yake kwa ujumla.