Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua katika mwelekeo wa Mpango huu, juu ya hoja ambayo tulijadili sana mwaka jana wakati wa Mpango wa Serikali 2016/2017, nayo ni kuhusu Mahakama ya Mafisadi. Suala hili limekuwa kimya nashangaa kwa nini wakati mafisadi wapo, wengine wamestaafu, ni kwa nini kwenye mwelekeo wa Mpango huu wa 2017 suala hili la Mahakama ya Mafisadi halipo?
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka kujua juu ya mwelekeo wa Mpango huu kuhusu ujenzi na ukarabati wa Mahakama Tanzania na hasa katika Jimbo langu la Mtwara Mjini Mahakama ni chakavu sana na hazikidhi haja. Je, ni lini suala hili litatatuliwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vya korosho ni muhimu sana katika kuinua uchumi wa nchi hii hasa Mikoa ya Kusini. Naomba kujua ni lini Serikali itafufua Viwanda vya Korosho, Mikoa ya Kusini ili kuinua uchumi kwa kuongeza thamani ya korosho na bei?
Mheshimiwa Naibu Spika, mikataba ya gesi na mafuta ni muhimu sana kuletwa Bungeni ili ijadiliwe kabla ya kuingia kwenye mikataba hii. Kwa muda mrefu mikataba imekuwa haina tija kwa Taifa hili na mapendekezo ya Mpango huu suala hili halipo, naomba majibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ardhi ni muhimu sana maana kumekuwa na migogoro mingi ya ardhi hapa nchini. Kwa mfano, kumekuwa na utaratibu wa Serikali kuchukua ardhi kwa wananchi na kukaa muda mrefu bila kulipa fidia kwa mfano Mtwara Mjini tangu mwaka 2012 mpaka leo UTT ilipima viwanja Mji Mwema ambako ni mashamba ya wananchi hawajalipwa. Hili ni jambo la hatari sana, naomba majibu tafadhali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia elimu ndiyo msingi wa maendeleo wa nchi yoyote ile duniani. Sera ya Elimu bure iangaliwe upya ili shule ziweze kujiendesha. Shule zinapata OC ya Sh. 27,000/= tu kwa mwezi itaweza kuendesha ofisi na shule kweli? Ni jambo la ajabu sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo ya elimu ya juu iangaliwe upya ili kila Mtanzania mwenye sifa ya kusoma elimu ya juu apate mkopo kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi. Kunyima mikopo watoto maskini kama ilivyo kwa mwaka huu ni jambo hatari sana kwa mustakabali wa Taifa letu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana miundombinu ya barabara kama vile reli kutoka Mtwara Mjini hadi Mchuchuma na Liganga kwenye chuma na makaa ya mawe iwekwe kwenye Mpango wa mwaka 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, utanuzi wa Bandari ya Mtwara ufanyike kwa haraka ili kuinua uchumi wa nchi yetu. Bandari hii haihitaji gharama sana kwa kuwa ni natural harbour, Serikali itenge fedha haraka kwa ajili ya utanuzi wa bandari hii. Sijaona suala hili kwenye mapendekezo ya Mpango huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo barabara ya Mtwara - Newala imetengewa fedha lakini mpaka sasa hata robo kilomita haijatengenezwa, ni jambo la ajabu sana. Naomba barabara hii ianze kujengwa tafadhali.