Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia mchana wa leo. Awali ya yote nachukua fursa hii kuwashukuru sana wananchi wapenda amani wa Jimbo la Mbinga Mjini kwa heshima kubwa waliyonipatia, nami
nawahakikishia tu kwamba sitawaangusha, nitawawakilisha kama wanavyotarajia. (Makofi)
Pia nachukua fursa hii kumshukuru na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli kwa kutoa hotuba nzuri, iliyosheheni weledi, iliyoangalia kila sekta na kwa maoni makubwa na mapana kwa maslahi ya Taifa hili la
Tanzania. Nawaomba tu Watanzania wote tuendelee kumwombea ili azma yake ya kuleta maendeleo ndani ya nchi hii ifanikiwe. Kusema ni rahisi, kutenda ni vigumu. Watapita wengi watakejeli, watapita wengi watasema lugha ambazo wanadhani zinastahili ili kuipunguza
thamani hotuba ya Mheshimiwa Rais. Mimi niseme tu kwamba Mheshimiwa Rais ametenda, amesema, ameelekeza na utekelezaji tumeuona.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme neno moja tu kwa kifupi. Tunapozungumzia habari ya amani, umoja, mshikamano na utulivu wakati wa chaguzi, naomba niwakumbushe jambo moja.
Watanzania tunaofanya active-politics tuko milioni tisa tunaotokana na vyama vya siasa. Milioni 50 ya Watanzania wote wanaobaki hawako kwenye active politics. Inapofika wakati wa uchaguzi, sisi milioni kumi tunajiona ndio wababe, tunaoweza kufanya kila kitu, tukawaacha
Watanzania wengine, tunachoma matairi barabarani. Askari wakituzuia sisi wanasiasa, tunasema aaah, mnahatarisha amani.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tofauti kati ya kuhatarisha amani na kusimamia amani. Alichokieleza Mheshimiwa Rais katika hotuba yake, uchaguzi ulikwenda vizuri, zile rabsha rabsha mlizokuwa mnaziona za vyombo vya ulinzi na usalama vilikuwa ni kuhakikisha kwamba nchi hii
inakuwa hamna amani. Nawashukuru sana Jeshi la ulinzi pamoja na Polisi kwa kazi kubwa waliyoifanya. Sisi tutaendelea kuwatia moyo, fanyeni kazi kusimamia amani ili maendeleo yapatikane. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye sekta moja; sekta ya kilimo ukiondoa sekta nyingi ambazo Mheshimiwa Rais alizielezea katika hotuba yake. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais anakiri kwamba asilimia 95 ya chakula tunachokipata hapa nchini kinatokana na Sekta ya Kilimo, lakini anakubali kwamba asilimia 30 ya mapato ya kigeni yanatokana na sekta ya kilimo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee niseme tu mambo machache kuhusu takwimu ya mwaka 2014, sekta gani ziliongoza kwenye kuleta pato la kigeni? Ukiondoa dhahabu ambayo ilileta shilingi bilioni 2,705, sekta zote zilizofuatia kwenye zile sekta tisa, zilikuwa
ni sekta zenye uhusiano na kilimo. Korosho ilileta shilingi bilioni 647, Pamba ilileta shilingi bilioni 558, Tumbaku ilileta shilingi bilioni 319, Kahawa ilileta shilingi bilioni 204, Mkonge ulileta shilingi bilioni 111, Chai ilileta shilingi bilioni 72 na Karafuu ilileta shilingi bilioni 50. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivyo? Ukiangalia zile top ten unakutana na sekta ya kilimo kwenye uchumi wa nchi wetu. Pamoja na mchango wa kilimo kwenye uchumi wa nchi yetu, bado wakulima wadogo wadogo wana changamoto nyingi sana ambazo
tunaiomba Serikali yetu itusaidie kwa haraka sana kuzitatua changamoto hizi. Changamoto ya kwanza ni ya pembejeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru Serikali inatusaidia pembejeo kwenye kilimo cha mazao ya chakula, lakini ukifika kule kwangu Mbinga Mjini. Mbinga Mjini imegawanyika katika maeneo mawili. Kuna milimani ambako tunazalisha Kahawa na mabondeni tunalima mahindi,
lakini wote hawa ni Watanzania, wote hawa wana mchango kwenye uchumi wa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwa watu wa kule Mondeki, Miyangayanga, Luwaita, Utili kwenye milima kule, wale watu wanalima Kahawa, hawawezi kulima mahindi. Kutokuwapatia ruzuku ni kuwafanya wadumae na mwisho wa siku kilimo kitakuwa mzigo baada
ya kilimo kuwa msaada kwa Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni ukosefu wa centers za kufanya utafiti ambazo tunaweza tukajua eneo hili mbegu gani inaweza ikafaa, eneo hili aina gani ya mbolea inaweza ikafaa, mwisho wa siku tuweze kuleta kilimo chenye tija. Tukiulizana hapa sasa hivi ni maeneo
gani, kuna hizi research centers ziko kwa ajili ya kuwasaidia wakulima wa eneo husika, jibu utakalolipata litakuwa bado viko kwenye mchakato au vimekufa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, ukosefu wa wataalamu, hawa tunaowaita Mabwana Shamba na mabwana mifugo. Tuzunguke kule vijijini tuulize lini Bwana Shamba alikwenda kumsaidia mkulima aweze kupanda kwa wakati, aweze kufanya palizi yake kwa
wakati na kumpatia ile elimu ya kilimo bora. Utakuta kwenye sekta hii, sehemu ya wataalamu, Mabwana Shamba na Mabwana Mifugo hatujafanya vizuri sana. (Makofi)
Lingine ni kushuka kwa bei ya mazao. Mkulima analima kwa nguvu zake mwenyewe. Inapofika masuala ya bei, haitabiriki. Pembejeo ziko juu, gharama za uzalishaji ziko juu. Matatizo haya yote yanasababisha kilimo kidumae na malengo tunayotaka ya kuajiri asilimia 75 ya Watanzania wote kutoka vijijini kwenye Sekta ya Kilimo, Mfugo na Uvuvi itapata tatizo kubwa. Changamoto nyingine inayotokana na hili eneo la kilimo ni kodi na tozo mbalimbali zinazowaumiza wakulima. Ukienda kwenye zao la kahawa, kodi na ushuru unaotozwa kwa wakulima unawatesa sana. Unakuta kuna kodi inaitwa Tanzania Coffee Research Institute ambayo ni 0.75, halafu kuna kodi nyingine inaitwa Tanzania Coffee Development Fund ambayo mkulima anatozwa 0.10 kwa kila kilo.
Lingine, kuna leseni ya TCB. Leseni ya TCB kabla ya mwaka juzi ilikuwa ni dola 24, sasa hivi imefika kuwa dola 24,000. Hivi mkulima wa kawaida atawezaje kwenda sambamba na ongezeko hili la dola kwenye TCB? Hali inakuwa ngumu sana. Naiomba Serikali, ili kumwongezea Mheshimiwa Rais nguvu ya kuleta maendeleo…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mapunda, muda umekwisha!
MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Ahsante sana. Naunga mkono hoja.