Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia taarifa hizi za Kamati mbili, Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa na ile ya Katiba na Sheria. Mchango wangu utajikita katika maeneo manne, eneo la kwanza linahusu utekelezaji wa miradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyooneshwa kwenye taarifa zote mbili kwamba, utekelezaji wa miradi bado sio wa kuridhisha kwa sababu fedha kutoka Hazina hazipelekwi kwa wakati. Hii ina madhara sana kwa sababu, mamlaka za Serikali za Mitaa kwenye ngazi ya Wizara inapopanga mpango mpya wa bajeti wakati fedha zile za mwaka uliopita hazijapelekwa kwa wakati huwa wanakuwa katika kigugumizi kwamba, nini kifanyike katika mwaka uliopita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipobadilisha budget circle tulikuwa na matarajio sasa kwamba, kwenye quarter ya kwanza au ya pili, fedha za maendeleo zingetolewa, budget circle imebadilishwa, mambo ni yaleyale, fedha hazitolewi kwa wakati. Sasa hivi Mamlaka za Serikali za Mitaa zinaandaa bajeti, lakini hawajapata fedha nyingi za maendeleo! Kwa hiyo, wanaishia katika kugombana tu kwamba, watekeleze ipi? Ile bajeti ya mwaka jana iwe kama bakaa kwamba ni miradi ambayo haikutekelezwa ili watenge fedha nyingine mwaka huu au wa-assume kwamba fedha zitaletwa ili watekeleze hiyo miradi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zinapochelewa hata hili tatizo ambalo limebainishwa kwenye Kamati ya Sheria kwamba Ofisi ya Makamu wa Rais inatengenezwa chini ya kiwango ni kwa sababu ya fedha kutolewa kidogo kidogo, kwa hiyo, hata Mkandarasi hawezi kutekeleza mradi kama ilivyopangwa kwenye mpango wa awali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili utahusu huu mradi wa TASAF, hakuna anayepinga mradi huu. Mradi huu kwa kweli umenusuru kaya maskini na umeleta mchango mkubwa sana katika kuboresha maisha ya kaya maskini katika nchi yetu, vilevile umewezesha sasa kaya maskini kupata huduma za kiafya, kielimu, ambapo bila mradi huu hawa wananchi wasingepata huduma hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto mbili ambazo nimeziona katika utekelezaji wa mradi huu. Kwanza lile zoezi la kuwatoa wanufaika ambao hawana sifa. Wale wanufaika walichaguliwa kwa kupitia mchakato ambao ulihusisha watu wengi sana na baadaye wakaanza kupata ule msaada, lakini lilipokuja zoezi sasa la kuwatoa hawa watu wameondolewa na wanaambiwa sasa hivi kwamba, warejeshe fedha zote ambazo wamelipwa chini ya mpango huu, wengine hawana uwezo kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi katika Jimbo langu, Kijiji cha Namisangi kuna wananchi ambao wakisikia mlio wa gari tu wanakimbia kwa sababu wamepewa barua na Mkurugenzi warejeshe zaidi ya sh. 400,000 na hawana uwezo wa kurejesha. Kwa hiyo, naomba Wizara husika sasa imchukulie hatua yule Mratibu ambaye kwa uzembe wake alipeleka fedha kwa watu ambao sio wahusika, lakini isiwe hawa wananchi ambao sasa wanapata taabu ya kulala porini wanaogopa kukamatwa kwa sababu ya fedha ambazo walikuwa wananufaika wakati ule mchakato ulipoendeshwa kwa taratibu ambazo zilifuatwa wakati huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuna changamoto katika uratibu wa mradi huu kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa mipya. Kwenye Halmashauri mpya unaambiwa kwamba, wanufaika wataendelea kupata huduma kutoka kwenye Wilaya Mama, kwa hiyo, inakuwa ngumu sana Mkurugenzi wa Wilaya Mpya kufuatilia zoezi hili kwa sababu, bado Mratibu anatumika wa ile Wilaya Mama. Nafikiri wakati umefika sasa kwa Wizara husika ione kwamba, eneo la utawala likianzishwa basi na taratibu za Wilaya ile kunufaika na mradi huu ziendelee kama ilivyo Wizara nyingine, hili suala la kwamba, waendelee kuratibiwa kutoka kwenye Halmashauri Mama inaleta urasimu na inakuwa ni vigumu katika kusimamia mradi huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu yangu ya tatu ni kuhusu Tume ya Utumishi wa Walimu (TSC). Imeoneshwa hapa na Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa kwamba kuna kusuasua kuanzishwa kwa Tume hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana kwa sababu, baada ya kupitisha Sheria hii tuliona kwamba, ni mkombozi kwa Mwalimu, lakini bado kuna kusuasua. Sasa wakati sheria hii ilipoanzishwa watu walitoa maoni yao kwamba, tusibadilishe jina, hii Tume ipewe nyenzo. Tunakokwenda sasa hivi inalekea hii Tume haitapewa nyenzo, kwa hiyo, inakuwa tumebadilisha jina tu, lakini utaratibu ni ule ule. Ni kama tulivyofanya kwenye sekta ya elimu, Ofisi ya Mkaguzi wa Shule tukabadilisha kwamba, Mdhibiti wa Ubora wa Elimu, lakini tumebadilisha jina tu rasilimali bado ni chache na Wakaguzi bado wanapata shida na hawawezi kuzifikia shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusipotenga fedha za kutosha kwa ajili ya kuanzisha Tume ya Utumishi wa Walimu tutakuwa tunawadai Walimu wawajibike wakati haki zao hatujawapa. Tunakimbilia kuwavua vyeo, sijui kuwateremsha madaraja, wakati vitu vyao vya msingi hatuwatekelezei! Hebu niiombe Serikali yangu itenge fedha za kutosha ili tuanzishe hii Tume ya Utumishi wa Walimu, Walimu wapate stahiki zao, Walimu wapate motisha, Walimu wawe na chombo kimoja cha kuwatetea halafu baadaye tuwabane katika uwajibikaji. Haiwezekani tuwabebeshe mzigo mkubwa, lakini inapokuja kuzungumzia maslahi ya Walimu sisi tunarudi nyuma. Kwa hiyo, lazima tuhakikishe kwamba, Walimu hiki chombo kinaanzishwa haraka na kinatengewa fedha za kutosha ili kiweze kutatua kero za Walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie suala la utawala bora. Yamesemwa mengi sana kuhusu madaraka ya Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa. Hili suala ni two way traffic, kuna watendaji ambao ni wabovu, naomba Waheshimiwa Wabunge tunapochangia tusiwalee wale watendaji wabovu. Kuna watendaji ambao wapo kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa ni nusu miungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna DMO mmoja katika Halmashauri fulani akipata fedha za Busket Fund anaangalia zile semina tu za kuhamasisha sijui kutoa mabusha, kufanya nini, lakini dokezo la kununua dawa, amepata fedha migao miwili ya Busket Fund, hajanunua dawa, lakini zile za posho za kwao wameshatumia tayari! Kwa hiyo, wananchi wanapata shida kwa sababu ya uzembe wa mtu mmoja, anapochukuliwa hatua tusione kwamba ni matumizi mabaya ya sheria, hapana ni two way traffic!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mwingine wale Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa wasitumie vibaya ile sheria iliyoanzisha Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Sura Na. 97 ya mwaka 2002 inatoa maelekezo, iko wazi kabisa. Inatoa maelekezo nini kifanyike mtu anapokamatwa kwa masaa 48 lakini Wakuu wengi wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa, hawaitumii. Hata Wakurugenzi kwa sababu kuna ishara sasa hata Wakurugenzi wanataka kuingia huko kwamba kuna maeneo mengine hakuna maelewano kati ya Mameya na Wakurugenzi. Kwa hiyo, tutengeneze mafunzo sasa kwa Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.