Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia jambo ambalo liko mbele ya Bunge letu Tukufu. Nitaanza na suala zima la kuchangia katika Kamati ya Katiba na Sheria ambayo na mimi ni Mjumbe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu haikufanya kazi vizuri kwa sababu bajeti ilikuwa ni finyu. Kuna maeneo ambayo tulipaswa kwenda kufanya ili tuweze kuona uzoefu na pesa ambazo zimekwenda kwenye miradi lakini tumeshindwa kufanya hivyo. Jambo la kusikitisha zaidi ni kwamba, kama utakumbuka Bunge letu Tukufu liliridhia kwamba na sisi tutoe mchango kwa wenzetu wale waliopatwa na tetemeko kule Kagera lakini pia Kamati yetu ambayo inaitazama Ofisi ya Waziri Mkuu tulishindwa kwenda hata kuwaona wenzetu wale waliokumbwa na ile kadhia. Kwa hiyo, nitarajie kwamba jambo hili tuliangalie kwa kina katika bajeti zijazo, Kamati hizi ziweze kupewa uwezeshaji wa kutosha ili zifanye kazi yake kamili ya kuisimamia Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika katika Wizara ya Sheria na Katiba, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora; Tume hii haikutengewa fedha kabisa ya kufanya kazi, zaidi ya mishahara na OC hakuna kingine ambacho kimewekwa katika Tume hii. Sasa tutakubaliana kwamba sasa hivi kwa kadri utandawazi unavyoongezeka na kadri ambavyo hata shughuli za kiuchumi zinazidi kupanuka, uwekezaji unaongezeka katika nchi yetu, basi pia matukio ya uvunjaji wa haki za binadamu nao unaongezeka. Kwa hiyo, tulitarajia kwamba, Tume hii iongezewe nguvu ya kifedha ili iweze kufanya kazi. Matukio yale yalilyokuwa yanatokea mwanzo siyo yanayotokea sasa. Sasa hivi teknolojia jinsi inavyokua na matukio nayo ya unyanyasaji na uvunjifu wa haki za binadamu nayo ndivyo yanavyozidi kuongezeka. Kwa hiyo, natarajia kwamba ofisi hii itaongezewe uwezo ili iweze ikafanya kazi yake vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulipotembelea Ofisi ya Waziri wa Sheria, tulikutana na changamoto kwamba hata jengo la ofisi liko katika mazingira ambayo siyo mazuri sana. Mheshimiwa Mshua ambaye niko naye hapa karibu aliweza hata kupoteza fahamu tukiwa ndani ya ofisi ya Waziri wa Sheria na Katiba, kwa maana kwamba ofisi haikuwa hata na mazingira mazuri kiasi kwamba hata watumishi pale sijui hata afya zao zitakuwa katika hali gani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo niendelee katika Ofisi ya Rais, Utumishi pamoja na Serikali za Mitaa, kwamba tuna tatizo katika Halmashauri ya Lushoto. Pesa ambazo tunazipata kutokana na own source tunazipeleka kulipa Watumishi wa Serikali ambao bado hawajapata vibali vya ajira kutoka Serikali Kuu. Takribani shilingi milioni 28 zinatumika kulipa Watumishi wa Halmashauri. Kwa hiyo hii inachangia kwamba pesa hizi ambazo zilipaswa kwenda kwenye asilimia tano ya akinamama na asilimia tano ya vijana na pia asilimia 20 kwa ajili ya kuwawezesha Wenyeviti wa Serikali za Vijiji kupata posho zao zinashindwa kwenda katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo limekuwa ni tatizo, Wenyeviti wa Vijiji katika Halmashauri yangu wana miaka zaidi ya 10 hawajawahi kupata fedha, hili ni tatizo kubwa linawafanya sasa wanashindwa hata kutekeleza wajibu wao. Kwa hiyo, niiombe Wizara hii ya Utumishi ihakikishe kwamba inatupokea mzigo wa watumishi hawa ili angalau pesa hii iende kwenye maeneo ambayo yanahusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la watumishi pia linaenda katika Idara ya Afya. Tumejenga zahanati 10 ambazo ziko tayari lakini hazina watumishi. Tumeiunga kauli mbiu ya Serikali ya Awamu hii ya Tano ya kujenga zahanati kwa kila kijiji, lakini sasa zahanati zile zinaanza kuchakaa bila kutumika. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali ihakikishe kwamba hawa watumishi wa afya wanaajiriwa kwa haraka ili waende kuwatumikia wananchi hawa wa Halmashauri ya Lushoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la ufungaji wa mazao kwa mtindo wa Lumbesa. Namwomba ndugu yangu Mheshimiwa Simbachawene kwamba hili tangazo bado halijaenea vizuri huku katika Halmashauri. Huku kwenye Halmashauri bado wanasubiri hawa wanaofunga Lumbesa kwenye yale mageti ya kukusanya ushuru, nadhani kwamba ingependeza zaidi kwa sababu hawa wanaofunga haya mazao wanafunga kutoka kwenye magulio na kwenye vijiji basi hii kazi wapewe Watendaji wa Vijiji wakishirikiana na Wenyeviti, kule kule wanakofungasha haya mazao ndiko ambako waanze kuwabana ili angalau hili tatizo liweze kuondoka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumza tatizo hili tunamaanisha kwamba akinamama ndiyo wanaoathirika sana kwa sababu ndiyo wazalishaji wakubwa katika halmashauri zetu. Utakuta wameshavuna viazi, wameshavuna nyanya na karoti halafu anakuja mwanaume anafunga kwa kadri anavyoweza, gunia moja linafungwa mpaka debe 10. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri kwamba, ule waraka ambao ameutoa basi aendelee kuukazia ashuke mpaka katika ngazi za vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la TASAF; TASAF nayo ina changamoto kwa sababu vile vigezo ambavyo vimeainishwa vya kaya maskini inawezekana katika zile hatua za awali, wananchi hawakujitokeza vizuri kwenye mikutano, kwa hiyo wakajiangalia walioko kwenye mikutano maskini ni nani wakaandika wale walioko kwenye mikutano, lakini baada ya uhakiki, inaonekana kabisa kwamba maskini halisi waliachwa majumbani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba Serikali pamoja na nia njema hii ya kuhakiki, naomba niendelee kwa sababu hata mimi katika pitapita zangu kuna mmoja ambaye alikuwa ni mnufaika wa TASAF yeye alikuwa siku za TASAF ndiyo ambazo ananunua bia na tulivyombaini tukatoa taarifa na akaondolewa kwenye ule mpango. Kwa hiyo, tuendelee kufanya utafiti ili watu hawa ambao hawastahiki wasiwepo katika hilo eneo la kupata hizi fedha za uwezeshaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo niongelee kuhusu asilimia tano kwa vijana na akinamama kwamba Halmashauri nyingi zinashindwa kutenga hii pesa katika Halmashauri zao na sababu ziko wazi. Huko nyuma, Serikali ya Awamu ya Nne ilikuwa imetoa matamko mengi ya kujenga haya majengo ya sekondari ambayo hakukuwa na mafungu, kwa hiyo Wakurugenzi nao kwa kuwa wanabanwa wakawa wanatafuta mahali gani wataweza kupata hizi pesa. Kwa hiyo, niombe kwamba sasa hivi hizi pesa hebu tuzitengenezee utaratibu mzuri Halmashauri wakati zinakaguliwa hasa na Kamati ile ya Serikali za Mitaa, tuangalie ni asilimia ngapi wametoa kwa ajili ya hawa vijana, ni asilimia ngapi zimetoka kwa ajili ya akinamama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama itapendeza kutokana na hili lindi la watu wenye ulemavu kuongezeka kwenda mijini, nashauri Bunge hili kwamba tufike mahali kwa nini tusipunguze japo asilimia moja katika hizi, tukatoa asilimia moja kwa vijana na asilimia moja kwa akinamama ili tukatengeneze asilimia mbili zikaenda kwa wenzetu walemavu kwa sababu huko kwenye Halmashauri ikiwa tunaweza kuwatambua itakuwa ni eneo zuri pia la kupunguza wao wasiende mijini. Kwa hiyo, kama tutaona linafaa tunaweza tukaliingiza, hizo asilimia angalau na wenzetu hawa wenye ulemavu waweze kupata asilimia hii kutoka katika mapato ya halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho nikazie kwenye asilimia 20 ambayo inapaswa kwenda kwa Wenyeviti wa Vijiji na Serikali za Mitaa. Hizi pesa Mheshimiwa Waziri Simbachawene haziendi. Halmashauri hazitengi hizi pesa, Wenyeviti hawapati posho na wakati mwingine inakwamisha hata tunapohamasisha shughuli za maendeleo, wanakosa nguvu ya ushawishi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri akazie hili kwamba Halmashauri ziwatengee pesa hizi za posho Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na Wenyeviti wa Vijiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana.