Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie muda huu ambao umenipa kupata nafasi ya kuchangia hoja ambazo zimeletwa mbele yetu na Kamati mbili za Kudumu za Bunge. Nami nianze kwa kumpongeza sana Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala. Yeye pamoja na Makamu Mwenyekiti lakini na Wajumbe wa Kamati hiyo ya Katiba, Sheria na Utawala kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kipindi cha mwaka mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwe mkweli, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kamati hii imefanya kazi kubwa sana ya kutushauri Serikalini katika mambo ambayo yanahusu utendaji kazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu. Naomba niseme kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu naishukuru sana Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala kwa kazi nzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitumie pia nafasi hii nimpongeze sana Rais wetu, Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli; Makamu wa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan; Waziri Mkuu, ndugu yetu Mheshimiwa Kassim Majaliwa na Serikali nzima kwa maana ya watendaji wote ndani ya Serikali ya Awamu ya Tano. Nasema hivi kwa sababu, kwa kweli mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Mheshimiwa Rais wetu na Serikali nzima wamejipambanua kwa nia njema ya kuleta maendeleo katika nchi yetu ya Tanzania. Watanzania wanalifahamu hili na sifanyi vibaya kusema kwamba ndiyo maana hata uchaguzi huu mdogo uliopita Watanzania wameonesha imani kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa mchango mzuri walioutoa katika taarifa hizi mbili za Kamati. Nasi kama Serikali, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwa yale ambayo ni mambo yanayohusu Wizara moja na nyingine, Ofisi ya Waziri Mkuu itachukua nafasi ya kuyaratibu ili kuona mawazo mazuri haya yaliyosemwa na Wabunge na Kamati hizi mbili yanafanyiwa kazi kwa maendeleo ya nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hoja zilizotolewa, jambo ambalo lilichukua nafasi kubwa hapa ilikuwa ni suala zima la ajira kwa vijana. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, kazi hii ya kutambua ni namna gani Serikali ya Awamu ya Tano itajikita katika kupunguza tatizo la ajira nchini imeshaanza kwa kiasi cha kutosha. Naomba niwahikikishie Waheshimiwa Wabunge tunaposhughulikia tatizo hili la ajira tutaangalia Watanzania wote bila kujali itikadi zao za vyama, bila kujali dini, bila kujali kitu chochote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliamua kwa kuanza kufanya utafiti wa kutambua nguvu kazi iliyoko katika nchi yetu ya Tanzania. Hilo ndilo lilikuwa jambo la msingi ili tuweze kushughulikia ajira. Baada ya utafiti wa mwaka 2014 tulitambua viwango mbalimbali vya nguvu kazi iliyopo katika nchi yetu ambavyo vinaweza kusaidia na kutupeleka kwenye maendeleo tunayoyataka. Tuliona ni muhimu pia tuzitambue sekta kiongozi ambazo zina uwezo wa kutoa ajira za kutosha kwa vijana wa Tanzania. Tulibainisha sekta tano ambazo zinaweza kuwa ndizo sekta hasa za kutoa ajira nchini kilimo ikiwa ni sekta mojawapo, mawasiliano na teknolojia, utalii, ujenzi na sekta nyingine ambazo ndizo tuliona tuanze kuzifanyia kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kufanya utafiti wa mwaka 2014 tulichokigundua ni kwamba tunayo kazi kubwa ya kufanya kama Serikali. Tuligundua kwamba kiwango cha nguvu kazi ya juu kilichopo katika nchi yetu ya Tanzania ni asilimia 3.6 na tunatakiwa kukipandisha kiwango hicho cha nguvu kazi mpaka asilimia 12 ndipo tuweze kutengeneza ajira. Pia tuligundua kiwango cha nguvu kazi tulichonacho katika nchi yetu ya Tanzania ili kuweza kutatua tatizo la ajira ni asilimia 16.6 na tunatakiwa kukipandisha mpaka asilimia 14. Tuligundua kiwango cha nguvu kazi tuliyo nayo nchini ya ujuzi wa hali ya chini ni asilimia 79 hadi 80. Ukiwa na ujuzi mkubwa wa kiasi kidogo, ukiwa na ujuzi wa hali ya juu wa kiasi cha kawaida huwezi kutoa ajira wala kuleta maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilishukuru sana Bunge lako Tukufu katika bajeti ya mwaka 2016/2017 ili kuinua viwango vya ujuzi na nguvu kazi katika nchi yetu, mlitutengea fedha na sisi sasa tumeweza kutengeneza progamu nne muhimu sana za kuweza kutengeneza ajira kwa wananchi wa Tanzania. Ili kuinua ujuzi na kuwafanya vijana wa Tanzania waajirike tumeamua kufanya mambo yafuatayo:-
(i) Tumetengeneza ajira ya kukuza ujuzi kupitia mfumo wa uanangezi; (ii) Tumetengeneza programu ya kukuza ujuzi kwa kurasimisha ujuzi katika mfumo usio rasmi wa mafunzo;
(iii) Tumetengeneza programu ya mafunzo kwa vitendo (internship) kwa wanafunzi wetu ili waweze kuajirika na kujiajiri; na
(iv) Tumetengeneza programu ya kukuza ujuzi kwa Watanzania waliopo makazini waweze kuendana na soko la ajira na teknolojia tuliyonayo sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini hayo yakifanyika kwa mwaka mmoja tumejiwekea lengo la kukuza ujuzi na kuwafanya vijana wa Kitanzania wajiajiri ama waajirike wasiopungua 27,000. Kwa hiyo, kazi hiyo inaendelea vizuri. Nataka kusema hapa kazi hiyo imekuwa nzuri kwa sababu Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala imetushauri vizuri sana na tumefanya nao kazi vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepokea yote yaliyozungumzwa kuhusu NSSF na ni kweli tunaendelea kufanya kazi nzuri. Nichukue nafasi hii kuipongeza sekta ya hifadhi ya jamii katika nchi yetu ya Tanzania kwa kazi nzuri wanazozifanya. Sekta ya hifadhi ya jamii imeendelea kukua na mpaka sasa rasilimali zilizopo kwenye sekta hii ya hifadhi ya jamii zimefikia thamani ya shilingi trilioni 10.2 katika nchi yetu ya Tanzania, ni mtaji mkubwa sana. Uwekezaji katika sekta hii tu ya hifadhi ya jamii umefikia thamani ya shilingi trilioni 9.2 katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, unaona kwamba sekta hii ina mchango pia mkubwa sana wa uchumi wa nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kama Serikali tutaendelea kusimamia sekta ya hifadhi ya jamii vizuri kwa kuzingatia miongozo na sheria tulizonazo pamoja na kuboresha mafao ya wastaafu katika sekta ya hifadhi ya jamii lakini tutaitumia pia sekta hii kukuza uchumi wa Tanzania na kutengeneza ajira kwa Watanzania wote katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi ya pekee sana kuwashukuru sana Wabunge lakini kulishukuru sana Bunge lako Tukufu kwa jinsi ambavyo mmekuwa mstari wa mbele kuishauri Serikali katika mambo yale ambayo mnaona kwamba yanaweza kuendeleza maendeleo ya nchi yetu ya Tanzania. Naomba niwahakikishie Serikali ya Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli ni Serikali sikivu, ina nia njema ya kuleta maendeleo ya nchi yetu na tutaendelea kufanya hivyo bila kusita. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge wote kwa pamoja tufanye kazi na wote lengo letu liwe ni kuleta maendeleo katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.