Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja hii ya Kamati ya Bajeti. Kwanza niunge mkono hoja ya Kamati ya Bajeti kwa sababu mambo mengi, changamoto ambazo zinaikabili nchi yetu kama Taifa, mengi Kamati imezingatia, kwa hiyo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa makusanyo makubwa ya mapato na kubana matumizi kulingana na mapato hayo halisi bila kutegemea misaada mingine. Baada ya pongezi hizo niwe na ushauri mdogo, kwa sababu tumeona pamoja na makusanyo makubwa ya mapato hayo item mbili ndio zinakula; mishahara pamoja na madeni. Kwa bahati mbaya sana madeni mengi ambayo yanalipwa kwenye kandarasi kubwakubwa na nyingi hizi zinatoka nje, maana yake ni nini? Serikali inatumia hizo bilioni zaidi ya 900 kwa mwezi lakini hela zile baadaye zinahama kutoka nchini zinakwenda nchi za nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningeomba ushauri katika hili, Serikali sasa ni vizuri ili kusisimua uchumi ndani ya nchi nao kuwalipa wawekezaji wa ndani ili kwanza waweze kusisimua uchumi, wakiendelea kufanya biashara wataendelea kutoa ajira kwa wananchi wetu lakini pia mzunguko wa pesa utakuwepo ndani ya nchi lakini kuendelea kuwalipa na yale madeni ya nje tu maana yake zile hela zinakwenda kuimarisha mzunguko kwenye nchi za wenzetu. Tunajua dawa ya deni ni kulipa lakini tuwe na balance ya sehemu zote mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunasema tuna uchumi wa viwanda, ni kweli kabisa tuna uchumi wa viwanda lakini pamoja na uchumi huu wa viwanda Serikali peke yake lazima inaitegemea sana sekta binafsi. Sekta binafsi hizi zingine ziko ndani ya nchi, kwa hiyo tunapowalipa wadeni wa ndani tutakuwa tunawarahisishia kushiriki kwenye uwekezaji wa ndani ya nchi kwenye uchumi wa viwanda. Kwa mfano tu, Serikali leo ikiweza kulipa mifuko ya jamii ambayo wanaidai Serikali mifuko hii itakuwa na uwezo mkubwa wa kuweza kuwekeza kwenye uchumi wa viwanda na sekta nyingine hapa nchini na kutoa ajira na kuimarisha uchumi ndani ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwenye suala la kilimo; kama ukurasa wa 42 unavyosema kilimo ndio uti wa mgongo, kinaajiri zaidi ya asilimia 70, lakini kwa bahati mbaya sana kilimo hicho hicho ukuaji wake kila mwaka unakwenda chini, sasa hivi tunaambiwa ni asilimia tatu ambayo hata yale makubaliano tu ya Maputo kule tunatakiwa angalau tuchangie asilimia 10, lakini kwa mwendo huu inaonekana bado tuna safari ndefu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwenye hili, kwa sababu huwezi kutatua matatizo ya kilimo au kilimo kipande bila kutatua matatizo yanayokabili Sekta yenyewe ya Kilimo, wenzangu wamezungumza mengi lakini lazima Serikali ije na mkakati mzito kwenye kutatua hili tatizo la mipango bora ya matumizi ya ardhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sasa kama zamani wakati wa Mwalimu Julius, ilikuwa inajulikana kabisa mikoa gani ya wafugaji na mikoa gani ya kilimo, kwa sababu hata tunapozungumza matumizi bora ya ardhi maana yake ni kwamba tukatenge ardhi zetu wapi panafaa kwa kilimo, wafugaji wakae wapi, makazi yake wapi. Sasa mpango huohuo uanzie ngazi ya Kitaifa kwanza kwa sababu haiwezekani ukawaweka pamoja wafugaji na wakulima, haiwezekani kukaa pamoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima tujue kabisa mikoa gani itatupa tija kwa ajili ya mifugo na mikoa gani itatupa tija kwa ajili ya kilimo. Nitoe mfano, Mkoa wangu wa Morogoro, tumeambiwa Ghala la Taifa, Ghala la Taifa maana yake ninyi mko zaidi kwenye mambo ya kilimo lakini hali inayoendelea kule kama hii mipango bora hatutaizingatia kuanzia ngazi ya Taifa, Mkoa na Wilaya itakuwa ni hadithi. Kwa hiyo, niombe tu hii mipango bora ya ardhi ianze kuanzia ngazi ya Taifa, itangaze kabisa mikoa gani mahsusi kwa ajili ya kilimo na mikoa gani mahsusi kwa ajili ya mifugo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo katika kilimo, leo kilimo hakivutii wakulima wapya, hakivutii mtu kwenda kuwekeza kwenye kilimo sababu kilimo chetu bado kinategemea mvua, huna uhakika wa kuvuna. Ndiyo maana leo bajeti ya kilimo kwenye mbolea kila mwaka inaongezeka lakini tija inapungua. Kwa nini? Mtu anaweza akapata mbolea, anaweza kupata trekta anaweza kupata mtaji lakini kama hana maji hayo yote ni bure, kama tunavyoona mwaka huu mvua haijanyesha, watu wamewekeza lakini watapata hasara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mfano mzuri ndiyo maana unaona hata Benki ya Kilimo yenyewe ina hela zaidi ya bilioni 59 lakini imekopesha bilioni tatu tu kwa sababu anaona kwamba hata akikopesha uhakika wa kulipa hamna. Ushauri wangu katika hili ni vizuri sasa Serikali tujielekeze zaidi katika mipango yetu kuwekeza kwenye maji, hasa kwenye mabwawa. Kwa hiyo, naungana na maoni ya Kamati kuongeza ile shilingi 50 kila lita ili iwe 100 ili Wizara hii iwe na Mfuko wa kutosha wa maji twende kutatua changamoto za maji na kukabiliana na hali halisi inayolikabili Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sasa hivi tuna ukame, mara nyingi tunakuja na mipango ya kukabiliana na matokeo hatukabiliani na chanzo kilichosababisha ni nini. Sasa hivi tuna tatizo hili la ukame sasa tukawekeze kwenye masuala ya mabwawa ya umwagiliaji ili kilimo chetu kiwe cha uhakika, mtu yeyote akienda kuwekeza kwenye kilimo awe na uhakika wa kuvuna kwa sababu maji ya kumwagilia yapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivi hata hizi benki za biashara tutakuwa tumetatua suala la mitaji kwa wakulima kwa sababu watawakopesha kwa sababu wanawafahamu kwamba wana uhakika wa kulipa kwa sababu wana uhakika wa kuvuna katika uwekezaji huo wa kilimo. Hata tukiongeza mbolea, hata tukiongeza madawa kama uhakika wa maji hamna, kama kilimo cha umwagiliaji hamna, hamna benki yoyote – iwe ya kilimo au iwe ya kibiashara ambayo inaweza kuwekeza kwenye suala la kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuhusu kukopa zaidi ndani, ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge wengi, kuna mmoja alikuwa anazungumza anasema kwa nini sasa hivi hatukopesheki huko nje, kuna sababu gani. Sababu ziko wazi tu, sababu ni kwamba sasa hivi demand imekuwa kubwa kuliko supply, hata hao wakopaji uwezo wao sasa hivi nao ni mdogo. Mfano mdogo tu tunauona sasa hivi hata Marekani wenyewe huyu Rais mpya aliyeingia anasisitiza viwanda vyao wawekezaji warudi kuwekeza ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limeishtua kidogo hata China. China wanasema sasa wanataka kubadilisha badala ya kwenda kuwekeza zaidi nje ya nchi wanaona ni bora kufanya innovation kwenye teknolojia yao ili kupunguza gharama za uzalishaji ili waendelee kuzalisha ndani ya nchi zao, maana yake wa-reduce production cost ili waendelee kulinda ajira yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii ni signal sio nzuri kwetu tunaposema kwamba tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda maana yake support kutoka kwa Mataifa makubwa itakuwa ni ndogo kwa sababu haya sasa na wao sasa hivi wataangalia zaidi Mataifa yao kuliko kuja kuwekeza kwetu kwa sababu wanaona kwamba kuja kuwekeza huku kama wanahamisha ajira za watu wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii kama Serikali tuichukue na twende kwa tahadhari. Ni vizuri katika hili tukajielekeza zaidi katika yale mambo ambayo tuna uwezo nayo na tuko wazuri katika uzalishaji zaidi kuliko haya ya kutegemea wawekezaji kutoka nje. Hawatapenda kwamba tuendelee kama wao halafu tuje tuendelee kugombania soko lilelile, wao wanapenda waendelee kututumia sisi kama soko badala ya kuwa partner wazalishaji wenzao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, katika suala la hizi milioni 50, ni vizuri kwamba Serikali ikaleta haraka sana, ndani ya bajeti hii kabla haijaisha ni vizuri hizi hela zikafika huko vijijini ili ziweze kwenda kusisimua hali ya uchumi na kuongeza mzunguko wa uchumi katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, ni vizuri Serikali tukawa na vipaumbele vichache ambavyo vinalingana na uwezo wetu badala ya kuwa na vipaumbele vingi ambavyo tunaviandika tu, wakati mwingine utekelezaji wake unakuwa hafifu. Ni vizuri tukavichagua vichache tukavitekeleza na kutokana na hali hali sasa hivi – kama alivyosema mwenyewe Waziri wa Fedha – upatikanaji wa mikopo ya masharti nafuu nje imekuwa ni michache sana, mikopo inayopatikana sasa hivi ni ya kibiashara. Kama mikopo inapatikana nje ya kibiashara maana yake itakuwa na masharti magumu na matokeo yake hata tukikopa zaidi itakuwa na riba kubwa na itakuwa ni mzigo mkubwa sana kwa Taifa na vizazi vijavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja ya Kamati, ahsante sana kwa kunipa nafasi.