Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kutoa mchango. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Hawa Ghasia pamoja na Kamati yake kwa kazi nzuri waliyoifanya naunga mkono hoja waliyoitoa na mapendekezo waliyoyapendekeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wote tunafahamu kwamba Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliongoza nchi yetu hii kwa miaka 24 na tangu ametutoka ni miaka 17 na siku zote bado amebaki kuwa rejea ya masuala mbalimbali ya uongozi wa Taifa letu na kwa kweli amekuwa kama sehemu ya uongozi wa nchi kwa maana ya reference hata akiwa kaburini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini imekuwa hivyo? Je, ni kwa sababu ameifikisha nchi yetu kule kwenye ndoto kabisa ya maendeleo makubwa ya kiuchumi, hapana. Ni kwa sababu dhamira yake ya kutufikisha huko ilikuwa wazi na ilieleweka pamoja na kwamba hatukufika kule tulikokuwa tunatarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais Dkt. Magufuli sasa hivi ana miezi 15 tu ya uongozi wake. Dhamira ya kutupeleka kwenye nchi ya neema hamna mtu yeyote anayeweza kubisha katika Bunge hili kwamba ipo. Dhamira iko wazi, ni nzuri na inaeleweka.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu sasa hivi na Serikali ya Awamu ya Tano ina miezi 15 tu madarakani kati ya miezi 120 ambayo tunatarajia Rais aiongoze nchi yetu. Leo tunachojadili ni robo tu ya bajeti ya kwanza kamili ya Serikali ya Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo, hamna ubishi kabisa kwamba kuna improvement kwenye kila eneo la utendaji wa Serikali na unapojenga misingi, unapoimarisha misingi ili mbele iwe rahisi kabisa kutengeneza mambo yawe rahisi nafahamu kuna watu watapata shaka watakuwa na uwoga, watapinga. Naamini kwamba nchi hii ni yetu sote na wakati mwingine unasikitika kwamba inapotolewa habari mbaya hapa Bungeni au habari ya kusikitisha, kwa mfano tunaposema Benki fulani imepata hasara nashangaa kuna watu wanapiga makofi kana kwamba hiyo ni habari ya kufurahisha. Nchi hii ni nchi yetu sote, habari ya kusikitisha ni yetu sote. Wawe Wapinzani, wawe watu wa CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tusifike mahali tukaamini kwamba mambo yanapotokea na kunapotokea setbacks basi kuna watu wanapaswa kufurahia. Nchi hii ni yetu sote, watu tunaowaongoza ni wetu sote, hivyo, naamini kabisa kwamba mtu yeyote mwenye akili timamu hawezi akasimama leo akasema nchi yetu imerudi nyuma badala ya kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ndugu amesimama amezungumza kuhusu Zanzibar kwamba kuwe na mazungumzo, tukae, kaka yangu Mheshimiwa Mtulia. Sasa uchaguzi Zanzibar ulikwishafanyika, Serikali ilishapatikana, Serikali halali, imechaguliwa kwa kura halali na ni muhimu kutambua kwamba Serikali ile ni ya Umoja wa Kitaifa kwa sababu kuna vyama vinne ndani ya Serikali ile na Serikali ile iko tayari kuzungumza…
MWENYEKITI: Malizia, malizia.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilinde muda wangu umeliwa.
Wenzetu watusaidie kwamba tuzungumze na nani kwa sababu CUF ziko mbili, tuzungumze na ipi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuzungumze na ile iliyochukua ruzuku au ile nyingine?
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja.