Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa
kunipa nafasi hii niweze kuchangia taarifa hizi mbili za Kamati ya Nishati na Kamati ya
Miundombinu. Lakini kabla ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye
ameendelea kunipa afya njema na leo hii nimesimama hapa katika upande huu nikiwa peke
yangu kabisa na afya njema kuwawakilisha wananchi wa Jimbo la Mtwara Mjini ambao
wamenituma nije nieleze haya ambayo nakusudia kuyaeleza hivi sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Wenyeviti wote wa Kamati zote mbili kwa
mawasilisho yao mazuri kabisa. Niungane na wenzangu kutoa vipengele kadhaa ambavyo
wameweza kuvionesha katika taarifa zao zote mbili.
Nianze na Wizara hii ama taarifa hii ya Miundombinu, moja kwa moja sehemu moja
wamezungumza kwamba, Serikali imeweka ama imeanza mkakati wa kupanua viwanja vya
ndege na mimi ni-declare interest ni Mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma,
tuliweza kutembelea pale Dar es Salaam, Terminal III kuangalia upanuzi wa ule uwanja.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo ambalo naweza kulizungumza kwamba, tulipata
maelezo pale kwa yule mkandarasi kuna suala hili ambalo Mwenyekiti wa Kamati kaeleza
kwamba ucheleweshwaji wa kupewa pesa ili waweze kuendelea na ule ujenzi na ule ujenzi
uweze kukamilika kwa wakati. Hili suala kwa kweli, Serikali inatakiwa iliangalie kwa jicho la
kipekee kabisa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka hivi sasa tunavyozungumza ni kwamba ujenzi wa
utanuzi ule unasuasua kwa sababu yule mkandarasi hajamaliziwa pesa zake. Kwa hiyo, tulikuwa
tunaomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hoja atueleze kwa nini anachelewesha
kumpa mkandarasi pesa ili utanuzi wa ile Terminal III uweze kwisha kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nizungumzie utanuzi huu uendane sambamba na
utanuzi wa viwanja vile tunaita viwanja vya kanda, kwa mfano Kanda ya Kusini kiwanja kikuu
kiko Mtwara Mjini na pale Mtwara Mjini tulizungumza wakati wa bajeti mwaka uliopita kwamba
ule uwanja hauna taa, ule uwanja unatakiwa utanuliwe! Ule uwanja safari moja tulishindwa
kutua pale tukalazimika kurudi Dar es Salaam kwa sababu ya ukosefu wa taa na taa zilikuwepo
huko miaka ya nyuma, lakini ziliweza kuondolewa hatujui zilipelekwa wapi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri
atakapohitimisha hoja hii atueleze ya kwamba mkakati upoje wa kutanua ule uwanja wa
Mtwara ikiwemo sambamba na kuweka taa za ule uwanja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine nizungumzie suala hili la utanuzi wa bandari,
wenzangu wamezungumza sana hapa kwamba kuna mkakati huu kwa mujibu wa Kamati wa
kutanua Bandari za Mtwara na Tanga. Lakini katika utanuzi wa bandari hizi, Mtwara haikutajwa
kinaga ubaga kama ilivyotajwa bandari zingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri atakavyokuja
kuhitimisha hoja atueleze kwa sababu mwaka jana tulipitisha bajeti hapa kwamba kuna utanuzi
wa gati moja Mtwara Mjini ambapo Bandari ya Mtwara tunasema ni bandari yenye kina kirefu
kuliko bandari zote Afrika Mashariki na kati lakini bado nimezungumza na Meneja wa ile bandari
pale Mtwara anasema bado mkataba ule haujasainiwa; pesa zilitengwa sasa tunataka kujua
kwamba tatizo ni nini mpaka leo hawajasaini ule mkataba wa kutanua gati la Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nizungumze suala hili la meli ambalo limetajwa katika
Kamati kwamba inaipongeza Serikali kununua meli na wanataka kukarabati meli za Ziwa
Victoria lakini niombe kwamba isiwe tu katika Ziwa Victoria; tuna Bahari ya Hindi kwa mfano
Mtwara miaka ya nyuma tulikuwa tunasafiri kwa usafiri wa meli kwa kiasi kikubwa na niseme tu
kwamba sasa hivi pale kuna kiwanda ambacho kinazalisha cement kwa kiasi kikubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Dangote anasafirisha anasafirisha cement yake kwa
barabara na barabara inaharibika sana wakati Mtwara tuna bandari yenye kina kirefu
angeweza kununua meli mzigo wake ukawa unapitia katika Bandari ya Mtwara kuelekea Dar es Salaam na kwingineko duniani. Lakini tunaacha hatuboreshi, hatununui meli kwa ajili ya
usafirishaji wa mizigo kwa kupitia Bandari ya Mtwara - Dar es Salaam na kipindi kile tulikuwa
tunaafiri kutoka Mtwara mpaka Zanzibar kwa kupitia Bahari ya Hindi; sasa hivi haya mambo
hayapo kabisa na wala hayatajwi kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana kwamba Serikali ihakikishe ya kwamba
inavyoboresha ununuzi wa meli katika Ziwa Victoria wahakikishe na Bahari ya Hindi pia kuwe na
ununuzi wa hizi meli, lakini hata kule Ziwa Victoria, ukienda kule Ziwa Tanganyika pia kule
Kigoma wana shida sana ya usafiri wa meli kuelekea nchi zile za jirani. Nilikuwa naomba kuwe
na uunganishaji wa aina hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala hili la barabara ambalo Kamati imezungumza kwa
kiasi kikubwa kwamba kuna ucheleweshwaji wa pesa za ujenzi wa barabara na niseme tu hata
barabara ile ya kutoka Mtwara Mjini kwenda Mivata ambayo inaunganisha Wilaya zote za
Mtwara Mjini na Mheshimiwa Ghasia juzi aliuliza swali hapa ndani kwamba mkataba ule
unasubiri nini kusainiwa? Na ukimuuliza Meneja wa TANROADS anasema tayari umesainiwa lakini
Waziri anasema bado haujasainiwa kuna mambo wanayashughulikia; sasa sijui imekwama wapi
kusaini ujenzi ule wa kilometa 50 kutoka Mtwara Mjini mpaka Mivata; tunaomba tupate taarifa
kutoka kwa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika nishati na madini; hivi sasa ninavyozungumza
Mtwara na Lindi takribani miezi zaidi ya mitatu hivi sasa umeme unakatika sana; kila sekunde
umeme unakata. Tunashukuru sana Serikali kwamba imeweza kutanua wigo wa umeme kutoka
Mtwara Mjini kuelekea Lindi na Wilaya zake zote. Sasa tunashangaa kwamba utanuzi huu
hauendani sambamba na kuhakikisha kwamba nishati ile inapatikana na ufanisi. Mtwara Mjini,
Lindi na Wilaya zake zote umeme unakatika sana, tunaomba maelezo ya kina kutoka kwa
Mheshimiwa Waziri hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nizungumze kidogo ambalo Kamati pia imegusia suala la
madini Tanzanite One. Hili suala mimi nikiwa chuoni mwaka 2008 alitembelea Rais wa Afrika
Kusini wakati ule Mheshimiwa Thabo Mbeki alikuwa na article yake aliandika inaitwa “African
Renaissance” yaani kwamba Waafrika tunatakiwa tufufuke tena upya na alikuwa ametueleza
sana kwamba watanzania nyie sisi tuna madini haya ya Tanzanite ambayo yanapatikana
Tanzania tu; dunia nzima wanategemea Tanzania lakini wanufaikaji wa kwanza ni Wamarekani,
wanufaika namba mbili ni Wahindi, watatu ni Waafrika Kusini, wanne ni Wakenya na watano ni
sisi wenyewe Watanzania; yaani sisi wenyewe ni wa mwisho. Alitueleza haya Mheshimiwa Rais
Thabo Mbeki pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Nkurumah Hall. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tangu mwaka 2008 yule ametufungua masikio lakini
mpaka leo bado tuaambiwa kwamba kampuni ama taasisi hii ya madini ya Serikali (STAMICO)
inajiendesha kihasara; tunashangaa hasara hizi zinatoka wapi? Wakati madini tunayo yamejaa
kweli kweli na haya yapo Tanzania tu hata tungeamua wenyewe kuuza bei yoyote tunayohitaji.
Kwa nini tusiende kujifunza kwa wenzetu ambao wameendelea kupitia sekta hii ya madini kwa
mfano Botswana kanchi kidogo tu, tunashindwa nini na Wizara ipo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nieleze kwamba hii STAMICO kampuni ama taasisi hii ya
madini imeshindwa kufanya kazi zake, wakati tunahoji kwenye Kamati ya PIC juzi tu hapa
hawana hata mtaji, wanadaiwa kwelikweli wakati tuna madini yamejaa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana kama Serikali imeshindwa kuziwezesha hizi
taasisi zake ikiwemo STAMICO basi ni vyema ingeifuta kwamba kusiwe na hii taasisi kwasababu
tunaendelea kutumia resources nyingi za Kiserikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimalizie suala hili la kusambaza gesi ambalo Kamati
imezungumza pia kwamba kuna ucheleweshwaji wa kusambaza gesi ambayo tulipitisha
kwenye bajeti hapa katika Bunge lako hili Tukufu lakini nieleze na niombe sana kwamba
usambazaji huu uanzie kule inakotoka gesi Mtwara na Lindi ili iweze kutunufaisha sisi na
baadaye kunufaisha Watanzania wote kama ilivyokuwa kwenye korosho. Ahsante sana kwa
kunipa nafasi hii.