Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Ignas Aloyce Malocha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakuru sana kwa kunipa nafasi
niungane na wenzangu katika kuchangia taarifa hizi zote mbili, Kamati ya Miundombinu na
Kamati ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanza naomba nianze na Kamati ya Miundombinu,
kwanza naipongeza Kamati kwa taarifa nzuri, nampongeza Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na
watendaji wote katika Wizara hii kwa utendaji mzuri. Kwa kweli kiuwajibikaji wanawajibika vizuri
na nadhani tatizo kubwa litakuwa ni pesa. Sasa labda nizungumzie suala moja ambalo naona
kwangu kama linanitesa, ni vipaumbele vya Serikali katika suala la barabara za lami,
tunafahamu kwamba sisi wote kwamba kuunganisha Mikoa na baadae itakuja Wilaya.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nazungumzia Mkoa wa Rukwa unasemekana
tumeunganisha barabara ya lami ni sawa, ni katika ukanda wa upande wa juu. Mkoa wa
Rukwa umegawanyika katika pande mbili; ukija ukanda wa Bonde la Ziwa Rukwa barabara
kuanzia kibaoni unakuja, Kiliamatundu, unakuja Kamsamba, unakuja Mlowo; ni ukanda
mwingine tofauti kabisa ambao hauwezi kufaidika kabisa na barabara ya lami ya kutoka
Tunduma mpaka Sumbawanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu imekingwa na mlima ambao gari haiwezi kubeba
mzigo wa zaidi ya tani tatu, lazima iwe inabeba nusunusu na barabara hii bahati nzuri
inaunganisha Mikoa mitatu; Katavi, Rukwa na Songwe. Barabara hii ina kilometa karibu 200 na
ni barabara ya siku nyingi hata wakati wa ukoloni ilikuwepo ndio maana sababu ya kuwepo
wakati wa ukoloni ni umuhimu wake; potential zilizopo katika maeneo yale, kilimo ni bonde la
ufa linakubali mazao karibu mengi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sijaua ni kwanini Serikali haijatilia umuhimu wa kuweka
lami katika barabara hii, na juzi wakati wamekuja watu wa MCC II waliuona umuhimu wa
kuweka lami barabara hiyo kulingana na vigezo vilivyokuwa vimewekwa, ni bahati mbaya tu
waliweza kujiondoa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka kuiambia Serikali kwa nini haitaki kuona umuhimu
huo ambao hata watu wa MCC wamekuja kuiona na wakoloni waliona; kwa nini haitaki kuona
umuhimu wa kutenegeza barabara hii katika kiwango cha lami? Ni barabara ambayo ina eneo
la bonde la ufa na ina rutuba, inakubali mazao yote, inalima mpunga, matunda; ina mito
isiyokakuka karibu kipindi chote cha mwaka na mvua za kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba Waziri atakapokuwa anakuja
kutoa maelezo atueleze ni kwa nini Serikali haitaki kuangalia barabara hii na ninajua sababu
yake ni viongozi kutokupita katika maeneo yale na bahati mbaya sana Mawaziri karibu walio wote ni wageni. Nawaomba safari hii mjaribu kutembelea ile barabara mtaona umuhimu,
itawagusa mpaka kwenye mioyo yenu, naombeni sana mtusaidie katika eneo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nishukuru kwa ujenzi ambao mnatarajia kuanza wa
daraja la Mto Momba, niwashukuru sana. Lakini faida ya ujenzi wa daraja lile ni kuunganisha
sasa ile barabara kwa lami; lakini kama mtalijenga mkaacha barabara ya vumbi itakuwa haina
maana yoyote. Kwa hiyo, na mimi nashauri kabisa jitihada za kujenga hilo daraja tunapongeza
lakini ziende sambamba na kufanya barabara ile iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakuja kwa upande wa Kamati ya Nishati na Madini; kwanza
nampongeza Waziri, Naibu Waziri na watendaji wake wote na Kamati kwa taarifa yao nzuri.
Lakini nataka kusema ni muhanga wa REA katika Jimbo langu. Jimbo langu nimeeleza mara
kadhaa kwamba ni jimbo ambalo limeachwa kabisa halina miundombinu ya umeme; na kwa
jinsi lilivyokaa kijiografia sijajua ni kwa sababu gani linaendelea kuchelewa. Ninafahamu wazi
kwamba tumepangiwa kuletewa umeme katika REA III.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini sisi tunakuwa nyuma kiasi hicho, kila jambo
tunakuwa nyuma na tunakaa gizani? Na bahati nzuri yapo maeneo mnapeleka umeme
mnapeleke watu hawataki kuutumia, umeme umeenda watu hawataki kuutumia, lakini lie eneo
ni eneo ambalo ukipeleka umeme watu watautumia kwa sababu vipo viashiria vya uchumi
vingi sana na ndio maana utakuta karibu eneo lote watu wamefunga solar; sasa watu
wanaojimudu kununua solar ukiwapelekea umeme utakuwa umewasaidia sana.
Ninamuomba Mheshimiwa Waziri ulione hili, nataka kipaumbele katika suala la umeme
katika maeneo yale yote; nikiungana na Mheshimiwa Kikwembe kule hatuna umeme kabisa.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, halafu cha ajabu mmekuja kupitisha nguzo mkapitisha Muze,
mkapitisha kwenye Kata zangu mkapeleka Mpanda sijui mlipeleka wapi huko; kwa hiyo
wananchi wangu wanaziona nguzo tu. Juzi niliongea na Meneja wa TANESCO kwamba
naomba basi ulete hata umeme wa TANESCO potelea mbali wananchi watalipa; wamewasha
kijiji kimoja cha Muze wananchi wamelipa karibu shilingi laki moja na kitu; wanajitoa wamalipa.
Sasa wanalipa kwa gharama hiyo je, ukipeleka umeme wa REA si wananchi wengi watafaidika
na umeme huu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo jambo lingine ambalo nilikuwa naomba Mheshimiwa
Waziri unisaidie umeme ambao mnapeleka REA III kwangu upande wa Kusini Mashariki,
mmefikisha nguzo katika Wilaya ya Mbozi kwa kijiji cha Kamsamba; kijiji cha Kamsamba kinacho
tutenganisha ni mto. Mmeshapeleka nguzo mmefunga na transfoma kwa maana REA II
watapata umeme wale watu, nina vijiji zaidi ya nane ambavyo vimepangana vinauangalia
umeme utawashwa Kamsamba halafu huku hakuna umeme, zaidi ya vijiji nane na vyenye
uchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri uliangalie hilo, kuwasha
umeme Kamsamba halafu kinachotutenganisha ni mto haizidi hata mita 500; kwa nini umeme
usivuke ukaja kuvisaidia vijiji vyangu zaidi ya nane ambavyo vina uhitaji huo umeme na
kupunguza gharama?
Mheshimiwa Naibu Spika, halafu tukubaliane vile vile hata kisiasa mnakuwa mmeniweka
mahali pabaya; wananchi wanashangaa kijiji kimoja kimepata umeme ng‟ambo ile, vijiji zaidi
ya nane viko huku vinachelewa kwa Mheshimiwa Silinde ni mambo ya ajabu sana. Kwa hiyo, Mheshimiwa utakapokuwa unakuja ueleze ni kwa nini usitumie ule ule umeme kuvusha huku.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ukanda ule una mito mingi sana isiyokauka na
nilishaeleza hapa kuna mto mmoja unaitwa Mto Nzovwe ulishafanyiwa utafiti kwamba unaweza
kutoa megawati kumi; nashangaa kwanini Serikali haitaki kutumia chanzo hiki kuongeza umeme
katika Mkoa wa Rukwa na umeme ambao una unafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nataka Waziri utakapokuja kama ukipata nafasi
unipe maelezo juu ya jambo hili. Nilikuwa na jirani yangu Mheshimiwa Mipata anasema kwake
umeme unakatika katika kwa hiyo, mliangalie na suala la kukatika katika umeme kwenye
baaadhi ya maeneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja lakini naomba
maelezo kutoka kwa Mheshimiwa Waziri.