Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. ABDALLAH N. MAFTAHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia mpango huu kwa niaba ya wananchi wa Mtwara Mjini. Nianze tu moja kwa moja kuangazia huu Mpango kwa sababu Mpango kwa kiasi kikubwa unaonesha namna gani nchi yetu sasa hivi inaingia katika uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la msingi sana ambalo sijaliona katika Mpango huu, ni usimamizi wa hivyo viwanda. Kwa masikitiko makubwa kabisa, hivi sasa tuna baadhi ya viwanda ambavyo vimejengwa katika nchi yetu na wawekezaji mbalimbali kutoka nje ya nchi. Kwa mfano, ukija pale Mtwara Vijijini kuna Kiwanda kinaitwa Kiwanda cha Dangote, lakini ukiangalia katika kiwanda hiki unaweza kuona kuna changamoto nyingi sana ambazo Serikali imeshindwa kuzisimamia na kuzitatua, lakini tunaleta Mpango ambao unasema kwamba Tanzania itaondoa umaskini kupitia Sekta hii ya Viwanda wakati hivyo viwanda vichache tunashindwa kuvisimamia na kuleta tija kwa wananchi wetu ili kuondoa umaskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa sana, niliweza kuzungumza suala hili katika mwelekeo wa Mpango kwamba Kiwanda cha Dangote kilichopo Mtwara kimeajiri Watanzania ambao wanatoka sehemu mbalimbali ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini kuna Makampuni mle matatu ambayo ni ya kigeni yanayosimamia uendeshaji. Ipo Kampuni ya Kichina, kuna Kampuni kutoka India na Kampuni nyingine kutoka kule Nigeria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi kampuni zilizopo katika Kiwanda hiki cha Dangote zinanyanyasa kwa kiasi kikubwa sana wananchi wa Tanzania. Sasa swali langu katika Mpango huu ni kwamba, kama tumetengeneza utaratibu wa kuhakikisha kwamba viwanda vinatatua changamoto za umaskini wakati tunashindwa kusimamia viwanda hivi; na pale nilizungumza katika mwelekeo wa Mpango huu kwamba malipo ya mishahara ya wafanyakazi wa Tanzania ambao ni wazalendo ni midogo na hata hiyo midogo yenyewe wanapunjwa. Badala ya kulipwa Sh. 12,000/= kwa siku ambazo zinaandikwa kwenye makaratasi, wanapewa Sh. 7,000/=.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilizungumza katika mwelekeo wa Mpango hapa Bungeni lakini mpaka leo hii tunapotaka kupitisha huu Mpango, bado marekebisho hayajafanyika katika Kiwanda cha Dangote. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara aunde Tume Maalum iweze kutembelea Kiwanda hiki cha Dangote kwa sababu kinanyanyasa Watanzania walioajiriwa pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze suala zima la bandari. Kwa mujibu wa mwelekeo wa Mpango huu, umesema tutaboresha uchumi wa nchi kwa kujenga bandari mbalimbali na Mheshimiwa Profesa Maji Marefu kazungumza hapa kwamba, bandari siku zote tunaangalia Bandari ya Dar es Salaam na sasa hivi tunaenda kujenga Bandari mpya ya Bagamoyo wakati Mwenyezi Mungu ametubariki, Mtwara tuna bandari ambayo ina kina kirefu Afrika Mashariki na Kati, Bandari ambayo Mwenyezi Mungu ametujaalia wala haihitaji kuchimba, lakini tunaenda kujenga bandari mpya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashangaa, wakati Serikali hii ina mpango wa kuhakikisha kwamba inabana matumizi, lakini tunaenda kujenga bandari mpya ambayo itatumia Dola za Marekani bilioni karibu 22.5, wakati Bandari ya Mtwara ambayo Mwenyezi Mungu ametubariki ilikuwa ni kuboresha tu kidogo na iweze kutumika kuinua uchumi wa nchi hii. Sasa mipango hii, ni kweli lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunaondoka hapa tulipo ili kuwa na maendeleo ya nchi hii wakati tunatumia pesa bila mpango ambao kimsingi unastahiki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu, kama kweli tunahitaji kuboresha uchumi wa nchi hii, tuboreshe Bandari za Mtwara, tuboreshe Mtwara Corridor, tuboreshe Tanga na maeneo mengine. Tusifikirie tu Dar es Salaam, Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala zima la elimu. Sasa hivi tunasema kwamba Serikali imeweka sera ya kutoa elimu bure, lakini kwa masikitiko makubwa kabisa, ukitembelea mashuleni huko, hii sera ya elimu bure imekuja kudumaza usimamizi wa elimu. Tunaangalia fedha za uendeshaji wa hizi shule, kwa mfano, Shule za Msingi; nilitembelea baadhi ya shule kama tano, sita pale Mtwara Mjini katika Jimbo langu, ukipitia fedha zilizoingia shuleni kwa miezi hii mitatu, ni jambo la kusikitisha sana. Kwa mwezi Sh. 27,000/= pesa za maendeleo halafu tunasema kwamba tunahitaji kuinua elimu kwa Sera ya Elimu Bure. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwa namna ya kipekee kabisa, Serikali iweke utaratibu wa kupeleka fedha mashuleni kama kweli tunahitaji kusimamia elimu na elimu ndiyo chachu ya maendeleo katika dira ya nchi yoyote duniani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kwa kifupi kilimo na uvuvi. Mpango huu umeelekeza kwamba tutainua kilimo kwa kuboresha mazao ya biashara na mazao ya chakula kwa wakulima, lakini nikizungumzia kwa mfano suala zima la zao la korosho Tanzania, tuna Bodi ya Korosho Tanzania, Bodi ambayo inasimamia Sekta hii ya Korosho Tanzania, lakini kwa masikitiko makubwa kabisa, hawana mkakati hata mmoja kuhakikisha kwamba huyu mkulima anayelima zao la korosho anapewa pesa ambazo zinastahiki pale anapouza mazao yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha ajabu kabisa, ukiangalia katika uuzaji wa mazao haya, zao la korosho kwa mfano, mkulima amewekewa tozo nyingi sana, mpaka tozo ya gunia ambalo Mhindi anakuja kusafirishia korosho kutoka Tanzania kwenda India anabebeshwa mkulima, halafu tunasema tunahitaji kuinua kilimo wakati mpaka leo tunavyozungumza bado bei ya korosho iko chini sana. Korosho inauzwa Sh. 1,800/= hadi Sh. 2,000/=. Ni jambo la kusikitisha kwamba Serikali inashindwa kumtafutia mkulima masoko ya zao la korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, korosho ni zao ambalo mwaka 2015 na mwaka 2014 limeingiza pesa nyingi Serikalini. Ukiondoa tumbaku, zao linalofuata ni korosho, lakini tunashindwa kuweka mikakati ya uhakikisha kwamba tunainua zao hili na mkulima anaweza kunufaika na kilimo hiki cha korosho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Mungu ametubariki Tanzania tuna Bahari ya Hindi kuanzia kule Mtwara mpaka Tanga, lakini cha ajabu ni kwamba Serikali katika Mpango huu sijaona kwamba imeweka utaratibu kuona inaboresha namna gani Wavuvi wetu wa Tanzania ili waweze kununuliwa vifaa, kupewa vifaa vya kisasa vya uvuvi ili waweze kuwa na uvuvi wenye tija na mwisho wa siku waweze kuondokana na umaskini. Leo tunakuja tunasema tunataka kuboresha kilimo na uvuvi wakati mipango yetu haioneshi namna gani tunaweza kuondoa umaskini kupitia Sekta hii ya Uvuvi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wazungu wanasema kwamba Tanzania Mungu ametubariki na hasa upande huu wa Kusini, tunasema ni vision sea, ni bahari ambayo ina samaki kedekede huko chini lakini Serikali haina mpango wowote wa kuinua Sekta hii ya Uvuvi ili Watanzania tuweze kuondokana na umaskini. Tunapiga danadana tu! Ooh, tutajenga Chuo cha Mikindani, wakati hatuna utaratibu, hatujaweka mkakati wowote wa kuhakikisha kwamba tunanunua maboti na vifaa vya uvuvi ili tuweze kuwasaidia wavuvi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kidogo suala zima la maendeleo. Maendeleo yoyote yanategemea amani na utulivu wa nchi, lakini kwa masikitiko makubwa kabisa, kwa mfano ukija Mtwara Mjini tangu mwaka 2013, 2014 mpaka leo hii 2015, Serikali iliweza kuchukua ardhi ya wananchi, maeneo ya Tanga na maeneo ya Mji mwema. Nimezungumza hili jana hapa kwenye briefing na hii ni mara yangu ya tatu nazungumza; Mtwara kuna mgogoro mkubwa sana wa ardhi. Wananchi wamenyang‟anywa ardhi zao na Serikali wakasema kwamba wataenda kulipa fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka 2013 mpaka leo hii, hakuna senti yoyote iliyotolewa na Serikali. Cha ajabu Serikali ukiiuliza, inasema tutafanya, tutafanya. Wananchi hawana sehemu za kulima, halafu tunakuja na Mpango wa kusema kwamba eti tunataka kuondoa umaskini Tanzania, wakati wananchi wananyang‟anywa ardhi na hawapewi fidia zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu, kwa sababu Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Lukuvi yupo hapa, atembelee Mtwara, akaangalie changamoto za ardhi ambazo zinaelekea sasa kuleta mpasuko wa Kitaifa na mtengamano wa Kitaifa kwa sababu wananchi wanasema tutafika wakati tumechoka na mwelekeo huu utakuwa hauna maana, Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la amani na utulivu ni jambo la msingi sana. Kama tunahitaji kweli kuhakikisha tunaleta tija katika Taifa hili, umaskini unaondoka, ni lazima tuvutie uwekezaji. Huwezi kuvutia uwekezaji kama hakuna amani na utulivu. Issue ya Zanzibar nayo ni ya msingi sana, siyo issue ya kubeza. Tunahitaji kukaa pamoja ili kujadiliana namna gani tunaweza kuleta amani na utulivu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Mikataba ya Tanzania, kwa mfano Mikataba ya Uwekezaji, mingi haina tija katika Taifa hili. Kwa mfano, kuna Mkataba wa Mlimani City, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kiliingia mkataba na Mwekezaji kutoka Botswana, Mkataba ambao kimsingi Serikali ya Tanzania inakusanya kwa mwaka asilimia 10% tu ya mapato yanayopatikana pale, wakati kuna mamilioni mengi ya pesa yanakwenda kwa Mwekezaji. Kwa hiyo, tunahitaji sasa kama Taifa tuingie kwenye Mikataba na huu Mpango uoneshe ni namna gani Bunge linaweza kupitisha Mikataba yote ya Tanzania ili tuweze kuwa na uwekezaji wenye tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze angalau kwa kifupi suala zima la afya. Afya ni jambo la msingi sana. Hatuwezi kusema kwamba tunahitaji maendeleo kama Watanzania wengi wanakufa kwa sababu ya afya. Ukija Mikoa ya Kusini, nilizungumza hili wakati wa kikao cha pili kwamba Kanda zote Tanzania tayari zimekamilika kuwa na Hospitali za Rufaa. Kanda ya Kusini mpaka hivi sasa, ujenzi wa Hospitali hii, jengo moja tu, unasuasua ambalo Mheshimiwa Waziri hapa alizungumza kwenye Bunge lako Tukufu kwamba iko katika hatua za umaliziaji ujenzi wa OPD, lakini mpaka hivi sasa ujenzi huo unasuasua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Hospitali ya Mkoa ya Mtwara hakuna X-Ray, Hospitali ya Wilaya hakuna X-Ray, halafu leo tunasema tunataka kuondoa umaskini, tunapitisha Mpango huu. Naomba kwa namna ya kipekee kabisa, kama kweli tunahitaji kuondoa umaskini Tanzania, ni lazima tujali afya za Watanzania, ni lazima tuboreshe afya za Watanzania, tuhakikishe kwamba vifaa tiba vinapatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi.