Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa niunge mkono taarifa zote mbili zilizowasilishwa na Wenyeviti wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuanza kutoa mchango wangu ningependa kuiambia Serikali, Bunge huwa linakutana hapa kupitisha bajeti ya Wizara na huwa wanatuambia wameweka cealing kwa hiyo, tunafuata cealing waliyotupa, lakini toka taarifa hizi zimeanza kuwasilishwa hapa ndani ya Bunge, hakuna Kamati hata moja ambayo imesema kuna Wizara ambayo imepata fedha zote walizozihitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti,sasa niiombe Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwamba, Bunge likishapitisha bajeti ihakikishe bajeti inafika kwa wakati kwenye zile Wizara, ili ile mipango iliyopangwa kwa ajili ya hizo Wizara iweze kutekelezeka, bila hivyo tutakuwa tunapiga kelele tu na kazi hazifanyiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la migogoro ya wakulima na wafugaji. Tumekuwa tukiona katika vyombo vya habari kwamba wakulima na wafugaji wamekuwa wakigombana kila siku. Ningependa kujua ile Kamati iliyoundwa ya pamoja ya kutatua migogoro imefikia wapi? Amesema msemaji aliyepita, tungetaka kujua wamefikia wapi ili kupunguza mauaji ya wakulima na wafugaji ambayo yanaendelea kutokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ni ya wakulima, wafugaji na wafanyakazi, haipendezi kuona wakulima wetu au wafugaji wakiendelea kuuana kila siku. Ifike wakati sasa Serikali ije na mpango madhubuti wa kutuonesha kwamba wanamalizaje tatizo hili la wafugaji na wakulima. Ili liishe ni lazima tuwe na matumizi bora ya ardhi na ndiyo maana nimeanza kwa kusema kwamba, ni lazima Wizara hii ya ardhi iweze kupatiwa pesa kwa wakati, iweze kupima na kuondoa migogoro hii. Tukiweza kupima na kuwapa wakulima maeneo yao na wafugaji, naamini kabisa tutakwenda kuondoa vifo vya wakulima na wafugaji kila siku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nisemee TANAPA. Niipongeze TANAPA imekuwa ikifanya kazi nzuri sana, lakini yapo matatizo yanayoendelea kujitokeza kwa maaskari wa TANAPA. Ni juzi tu hapa Mbunge alinyanyuka na kusema kwamba kuna mwananchi amepigwa risasi ya jicho na ikatokea kisogoni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuwaomba ndugu zetu wa TANAPA na Wizara kwa ujumla wawe wanafanya utafiti ambao unaweza kujua kwamba askari wanaowaajiri wanao uzalendo wa kweli; kwa sababu kila siku Wizara imekuwa tukikaa nao na wanasema wanatoa mafunzo lakini mafunzo haya naona bado hayasaidii. Ndugu zetu, watoto wetu wameendelea kuuawa na sisi hatupendi kuleta migogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sana TANAPA ichukulie suala hili kwa umakini sana na kufuatilia ili kuondoa tatizo la vifo kwenye mbuga zetu, mapori ya akiba na hifadhi. Naamini tukifanya hivyo tutakwenda kupunguza suala la vifo kwa watu wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la njaa. Juzi tulikuwa tumekwenda Karatu kwenye msiba, kwa bahati nzuri tuliona mizoga ya ng’ombe, mbuzi katika makundi makubwa imetapakaa, imekufa. Sasa ningependa kujua Wizara husika inachukua tahadhari gani kunusuru mifugo hii? Pia si kwa mifugo tu, hata kwa wananchi. Wameanza kufa ng’ombe, lakini itakuwa ni aibu kubwa sana Watanzania wakifa kwa njaa. Ilitolewa taarifa hapa na siamini kama iko sahihi kwa sababu, ma-DC na Wakuu wa Mikoa wamekuwa waoga sana kutoa taarifa sahihi. Ningependa Serikali ihakikishe kwamba, hakuna Mtanzania yeyote atakayekufa kwa njaa katika kipindi hiki cha ukame.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kuzungumzia suala lililosemwa kwenye taarifa yetu; tulikutana na wasafirishaji wa nyama, wafanyabiashara wanaosafirisha wanyama-hai. Walitueleza matatizo yaliyowakumba, walipewa leseni lakini walisitishiwa biashara hiyo; na kibaya zaidi walipositishiwa tayari walikuwa wameshakamata wanyama kwa ajili ya kuwasafirisha. Sasa ningependa kujua ni sababu gani za msingi zilizosababisha watu hawa kusitishiwa biashara yao? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuna taarifa zinazodai kwamba wako watu ambao si Watanzania wamepewa vibali kwa ajili ya kusafirisha wanyama hawa. Ningependa kujua ni sababu gani za msingi zilizosababisha Watanzania hawa ambao rasilimali hizi ziko ndani ya nchi yao, wao wananyimwa, lakini wanapewa wengine. Tungependa waziri anapokuja kujibu atuambie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lile suala nililokuwa nalisemea la kuhusu migogoro ya mipaka; Serikali inachangia sana na hii inaonesha kwamba Wizara zile husika huwa hazitoi ushirikiano, hazishirikishani na hii ndiyo inayoleta shida, kwa sababu unakuta kimeanzishwa Kijiji, Kata, Wilaya au Mkoa lakini hawashirikishi hata haya Mashirika ya TANAPA pale wanapoweka ile mipaka kujua kwamba hili ni eneo la hifadhi. Kwa hiyo, ningeomba sana Wizara zile husika waweze kushirikisha mashirika yetu haya pale wanapokwenda kuanzisha either ni Kijiji au Kata kwenye yale maeneo ambayo yanazunguka hifadhi zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini tukifanya hivi tutaendelea kuondoa malalamiko ya wananchi na nchi yetu itakuwa na amani. Hatuwezi kuona Watanzania wanaendelea kufa kila siku kwa sababu ya sisi tuliopewa nafasi tumeshindwa kuzitumia nafasi zetu kuwaweka waweze kuishi vizuri katika nchi yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, amesema Mwenyekiti katika taarifa yetu, utalii wetu bado hatujaweza kuutangaza vizuri. Tulibahatika sisi Kamati Bunge lililopita kutembelea Afrika Kusini tuliona wenzetu wanavyotumia utalii wa fukwe, lakini nchi yetu tumeshindwa kutumia fukwe tulizonazo na tunazo fukwe nzuri sana; lakini za kwetu ukipita ni harufu tu, utasikia harufu zinazonuka huko tumeshindwa kuzitumia vizuri. Niiombe sasa Wizara itumie utalii wa fukwe lakini pia na yale maeneo ambayo kwenye kamati tumeonesha tuweze kuyatangaza vizuri na kupata watalii wa kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo maeneo mengi sana ya utalii, lakini kama nchi tumeshindwa kutumia na wale wenzetu wa kusini wanayo maeneo na tumeomba kabisa kwamba ile Bodi ya Utalii iweze kupata fedha za kutosha kuweza kutangaza maeneo yale ili tuweze kupata pato kubwa sana la fedha za kigeni kutoka nje kama mataifa mengine ambayo wameweza kupata kupitia maeneo ya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi.