Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Edwin Mgante Sannda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii. Kwanza kabisa nipende kuchukua fursa hii kuzipongeza Kamati zote mbili kwa taarifa na mapendekezo yao na pia nianze kwa kusema naunga maoni na mapendekezo yote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, basi nichukue fursa kuzungumzia machache. Kwa upande wa Kamati ya Maliasili napenda kwanza kushauri kutolewe na zitengwe fedha kwa ajili ya kutoa elimu ili watu wafahamu umuhimu na faida za uhifadhi kati ya mipaka ya mapori ya akiba, mapori tengefu na maeneo ya makazi. Watu wamekuwa hawaelewi umuhimu wa hili jambo; ndiyo maana unakuta watu wanavamia, mifugo mara nyingine inakwenda inaingia ndani ya hifadhi, kunakuwa na vurumai sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufuatilia hakuna fedha hata kidogo zinazotengwa za kutoa elimu kupitia Wizara na hizi Mamlaka za Uhifadhi; sasa wanawezaje kuendesha hiyo kampeni ya kuelimisha wananchi? Matokeo yake wanakwenda na nguvu tu, wakati mwingi wanatumia nguvu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejaribu kwenye Jimbo langu Kondoa kufanya zoezi hili na likafanikiwa kwa kiwango kikubwa, watu wameanza kuelewa kutii sheria bila shuruti, kwa maana ya kutokuingia kule ndani, lakini pia taasisi hizi zinazohusika na uhifadhi ni lazima ziwe na fungu la kufanya zoezi hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwetu kuna pori la akiba la Swagaswaga na lipo Mkungunero na watu lazima waelewe namna ya ku-co-exist, tusipo co-exist na wananchi wakajua kuna faida gani ya haya mapori, wakaziona na wakanufaika nayo ina maana itakuwa vurumai inaendelea tu. Kwa hiyo, nataka kusisitiza Wizara lazima kutengwe fungu hawa watu waweze kuelimishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika hiyo hiyo namba mbili, askari wa wanyamapori; kweli wana jukumu la uhifadhi, lakini ndugu zetu hawa kwa kuwa wamekuwa wanahifadhi wanyamapori wamekuwa na wenyewe kama wanyama, wanaua hovyo. Wakati mwingine hata hakuna sababu ya kutumia nguvu kubwa hiyo, lakini wanakutana na mtu labda tena wakati mwingine; mimi nina kesi mwezi wa 12 hapa, alikuwa ameonekana kijana ana pikipiki amebeba kifurushi cha sukari guru, kinavuja vuja hivi wao wakadhani ni nyama ya pori labda ni swala. Walimfuatilia wao wana gari lao land cruiser yule kijana ana pikipiki wamekwenda kumuua kwenye kijiji wala si kwenye hifadhi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kijana mmoja, hana silaha hana lolote, anaendesha pikipiki yake of course na yeye alikimbia maana wale askari wa hifadhi wakionekana watu wanapata hofu; akawa anakimbia na pikipiki yake wale jamaa wamemkimbiza wamefika hatua kijana asiye na silaha anapigwa risasi sita. Sasa hata kama angekuwa ni Thomson Gazelle ameuwawa pale si furushi la sukari guru kweli hukumu yake ilistahili kupigwa risasi zote zile? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara na mamlaka, hizi taasisi hebu tuwafundishe hawa askari wetu wawe na ubinadamu kidogo. Halafu baada ya kumuua wamemchukua wakamkimbizia porini ili waje kudai kwamba mtu huyu ameuwawa ndani ya hifadhi; mtu kauwawa kijijini. Wakachukua na furushi lake la sukari guru na pikipiki wakaingia nayo ndani kwenda kupotosha ushahidi. Kumekuwa na taratibu hiyo mara nyingi sana kwa sababu askari kwa askari taarifa ikiripotiwa wanalindana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuona dalili zile, bahati nzuri nilifika kwenye tukio mapema sana, nimshukuru sana Mheshimiwa Mwigulu nilizungumza naye nikamwambia nina wasiwasi hapa kuna dalili za kupotosha ushahidi, watu wameingiza maiti ndani. Wewe umeua mtu si unamuacha kwenye crime scene? Tena ni askari una ujuzi, unaondoa kwenye crime scene unapeleka porini ili ukamsingizie. Basi akaweka jitihada ule utaratibu ukafuatwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, walikuwa ni askari saba mpaka sasa hivi wamekamatwa askari watatu tu wako ndani including wawili waliopiga risasi; mmoja ali-shoot risasi mbili na mwingine risasi nne. Imeenda kupasua mapafu na moyo mpaka kijana wa watu akapoteza maisha namna hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuwafundishe askari wetu; Mheshimiwa Waziri na viongozi wote huko; hawa jamaa wawe na ubinadamu. Kuwa wahifadhi wa wanyampori haina maana nao ni wanyama. Nataka kupendekeza, tukio lile lilitangazwa na likawa kubwa sana kwenye vyombo vya habari, basi hata hawa maaskari watakapohukumiwa nalo lijulikane ili wananchi wapate imani na Serikali yao kwa sababu wanaona watu wanawekwa ndani kwa muda tu halafu wanapotea. Mtu aliyeua namna hii stahili yake ni hukumu ya kunyongwa mpaka kufa, umeua makusudi, si bahati mbaya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nisisitize sana Wizara iliangalie hili kwa kina sana na limetokea, Mkungunero; miaka ya nyuma wakati wa tokomeza tuliona haya yamekuwa kwa wingi sana. Kwa hiyo, nisisitize Wizara ilitilie mkazo na kuwafunda wale askari, si wanyama wale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka kuzungumzia uimarishwaji wa ile mipaka kati ya mapori tengefu, mapori ya akiba, hifadhi na maeneo ya wananchi. Ndugu zangu siku vile vikosi kazi vinapokwenda kuweka ile mipaka ishirikishe wananchi. Kwa sababu unaweza ukasema usishirikishe wananchi baadaye migogoro inaendelea miaka nenda rudi. Wawe sehemu ya uwekaji wa mipaka ile. Idara za ardhi katika Halmashauri zetu zishiriki, wanakwenda na GPS wanaona mipaka na wanajiridhisha hii ndio iliyoandikwa na ndio tunayoijua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu vinginevyo malalamiko yanaendelea, aaa, mpaka ulikuwa hapa, sasa wameusogeza mbele. Sasa tutaendekeza malalamiko ya namna hii kwa muda gani? Kuna ugumu gani Wizara na hizi mamlaka za hifadhi kuwashirikisha wananchi na idara za Halmashauri zikaenda na vifaa; na document zao wanazo basi utaratibu unakuwa clear. Hilo nalisisitiza sana ili tuweze kupunguza hii migogoro isyokwisha kati ya hifadhi na maeneo ya makazi na kilimo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo kwa ufupi sana kuhusu kilimo; jamani tutazungumza sana kilimo na uchumi wa viwanda. Hiki kilimo kama hatutakiwekea bajeti kubwa kabisa ya kutosha kwenye upande wa umwagiliaji tutakuwa tunapiga story tu.