Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa, japokuwa nilidhani kwamba ningeweza kuchangia mchana lakini nakushukuru sana inawezekana mchana kutakuwa na wachangiaji walio wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia katika Taarifa zote za Kamati kama ambavyo zimewasilishwa na Wenyeviti. Kwa masikitiko makubwa sana, taarifa hii ya Kamati ya Mifugo na Maji iliyowasilishwa mbele ya Bunge lako Tukufu, ukurasa wa 12 unazungumzia migogoro kati ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikitishwa sana na taarifa hii ya Kamati ambayo kwa namna moja au nyingine wameshindwa kabisa kuona kwamba mgogoro kati ya wakulima na wafugaji ni mgogoro mkubwa ambao unahitaji Serikali kuingilia kati kwa haraka. Nimesikitishwa sana kwa sababu ukisoma taarifa hii, mgogoro kati ya wakulima na wafugaji umeandikwa nusu page, kwa kweli ni masikitiko yangu makubwa na hiki ni kilio cha wakulima wote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sina maana kwamba hatuwapendi wafugaji, tunawapenda sana wafugaji, lakini kwa namna ambavyo Serikali imeshindwa kutatua migogoro kati ya wakulima na wafugaji na ndiyo maana nasimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu na mara zote ambapo nasimama tunaona kabisa hatari kubwa; ile amani tuliyoachiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere inakwenda kupotea kwa sababu tu ya mgogoro huu kati ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimelisema hili kwa muda mrefu sana na hata Waheshimiwa Mawaziri wanafahamu hilo. Mgogoro huu kati yetu, sisi Rufiji kule, hatuna mgogoro wa ardhi naomba Bunge lako Tukufu litambue, Rufiji hatuna mgogoro wa ardhi; tulichonacho ni criminal trespass, mwingiliano wa jinai ambao unafanywa na wafugaji katika maeneo ya wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili ni kubwa na mwezi wa 11 watu wawili wameuawa, mkulima alichinjwa na mfugaji alichomwa moto akiwa hai katika maeneo ya Kilimani. Cha kushangaza sana hakuna kiongozi yeyote wa Serikali au Wizara aliyefika katika maeneo husika ili kuweza kutoa pole na kuweza kuongea ili kuondoa mgogoro huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni masikitiko yangu makubwa sana na Wanarufiji wote leo hii wananiangalia kwenye TV, nimesimama mbele hapa; si Tanzania tu, dunia nzima Wandengereko wote dunia nzima na Warufiji wote wanajua; mgogoro kati ya wakulima na wafugaji unapaswa utatuliwe haraka sana vinginevyo unakwenda kuligawa Taifa hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yale mambo mazuri ambayo alituachia Rais wetu wa Awamu ya Kwanza, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kupendana Watanzania tunaona kabisa kwamba tunaanza kubaguana. Mimi nasema wazi mbele ya Bunge lako Tukufu, mgogoro huu unakuwa mgumu kwa sababu viongozi wa Wizara hii wengi ni wafugaji na wanashindwa kutatua matatizo ya wakulima. Naomba niishie hapo, message sent and delivered kama ambavyo Mheshimiwa Rais amekuwa akisisitiza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni tatizo kubwa la RUBADA. Tunayo hii Mamlaka ya RUBADA, Mamlaka ya kuendeleza Bonde la Mto Rufiji. RUBADA ilianzishwa mwaka 1978. Dhamira ya uanzishwaji wa RUBADA ilikuwa ni kuendeleza bonde pamoja na Mto Rufiji, lakini tunasikitika sana Warufiji baada ya Mamlaka hii kukabidhiwa Bonde la Mto Rufiji basi wananchi wa Rufiji wamekuwa maskini wa hali ya juu. RUBADA imeshindwa kuwasaidia Warufiji lakini pia RUBADA imeshindwa kuwasaidia wananchi wote wanaoishi na wanaopitiwa katika Bonde la Mto Rufiji kuanzia Morogoro na maeneo mengine yote ya Tanzania yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Bunge liazimie sasa kuivunja RUBADA mara moja na Mamlaka yote ambayo inamilikiwa na RUBADA ibaki chini ya Halmashauri husika ikiwa ni pamoja na vijiji. Tunaamini kabisa Warufiji tukikabidhiwa bonde letu la Mto Rufiji tutaweza kuwatafuta wawekezaji watakaosaidia kilimo cha umwagiliaji. Naomba katika maazimio liingie azimio la kuifuta RUBADA, haina maslahi yoyote na hawana uwezo wa kuwasaidia Watanzania wanaoishi maeneo ya Rufiji zaidi ya kufanya udalali ambao hata sisi wenyewe tunaweza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikumbushie jambo lingine la mwisho, ni kuhusu ujenzi wa nyumba zinazojengwa na National housing.Tukiangalia dhamira ya Mwalimu Nyerere, mimi ni mjamaa kweli kweli! Tukiangalia azimio la Mheshimiwa Rais wetu wa kwanza, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, uanzishwaji wa National Housing ulilenga kuwasaidia Watanzania wanyonge, Watanzania wadogo wasio na uwezo, wafanyakazi wa Serikali, lakini leo hii National Housing ipo kwa ajili ya matajiri tu. Hakuna Mtumishi wa Serikali wala Mtanzania mnyonge mwenye uwezo wa kwenda kupanga kwenye nyumba za National Housing.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliombe Bunge lako Tukufu, ile dhamira ya uanzishwaji wa National Housing kama ambavyo Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Kwanza alivyoanzisha, kuchukua nyumba za Mabepari na kumilikiwa na Serikali. Dhamira ile ilikuwa ni kwenda kuwasaidia Watanzania wanyonge pamoja na Watumishi wa Serikali, naomba Bunge lako pia liazimie, National Housing iweze kuchunguzwa na kuangaliwa sasa ni namna gani itaweza kuwasaidia Watanzania walio wanyonge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe maazimio haya yaingie na niombe Mwenyekiti wa Kamati atakaposimama hapa aweze kujibu hoja hizi kama ambavyo nimeweza kuzieleza. Mgogoro wa wakulima na wafugaji unahitaji kuingiliwa kwa haraka sana na Serikali ili uweze kutatuliwa. Ni jambo la aibu sana kwa Kamati kuandika nusu page mogogoro wa wakulima na wafugaji. Watanzania wanauawa, Watanzania wanauana, wamepoteza dhamira ya kupendana wenyewe kwa wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba ile miiko ya Mwalimu Nyerere aliyoianzisha wakati ule wa kupigania uhuru na hata baada ya uhuru. Tunaomba Kamati iweze kujiuliza ni kwa nini wamefikia hatua hii?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma vizuri ukurasa wa 13 unasema kwamba viongozi wa Serikali ambao wanashiriki katika kutatua migogoro hii hawakuwashirikisha wafugaji. Hili ni jambo la aibu kabisa. Ni wakulima wangapi wameshirikishwa katika mgogoro huu? Hili ni jambo la aibu, lakini tunafahamu kwamba kwa sababu wakulima hawana pa kusemea, lakini sisi kama viongozi wao tunasimama hapa kwa ajili ya kuwatetea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao wapiga kura walio wengi; lakini tunatambua kwamba katika pato la Taifa, kilimo kinachangia asilimia zaidi ya 70. Tuiombe Serikali itambue hilo. Pia hata Wizara ukiiangalia namna ambavyo inatupuuza wakulima. Ukiangalia katika bajeti iliyopita, Wilaya yetu ya Rufiji ambayo tuna ekari zaidi ya 13,000 ambapo kuna bonde zuri kwa ajili ya kilimo tungeweza kuuza Tanzania, Afrika Mashariki na Afrika ya Kati, lakini Wizara ya Kilimo imetenga sifuri kwenye bajeti yake ya kilimo kusaidia wananchi wa Rufiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kusaidia kilimo tunaamini kwamba hata hiyo Tanzania ya viwanda hatutafikia huko. Naomba kuwasilisha lakini naomba; katika maazimio niliyoyaomba ni pamoja na kuifuta RUBADA kwa sababu haina faida yoyote kwa Watanzania. RUBADA wamekuwa madalali na sisi hawatusaidii lolote. Tunaomba bonde libaki chini ya wananchi wanaomiliki bonde hilo na maeneo ya mto ili tuweze kuwatafuta watu watakaoweza kutusaidia katika kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuwasilisha.