Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza napongeza Kamati zote kwa taarifa ambazo wamezileta. Kabla sijaanza kuchangia naiomba Serikali, tunakuja hapa tunachangia maeneo mengi, tunashauri lakini unakuta vitu vingi tunavyoshauri mara nyingi havichukuliwi maanani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, tunakuja hapa tunatumia kodi ya wananchi ambao tunawawakilisha, naiomba sana Serikali muwe wasikivu tunapotoa ushauri muuzingatie, haiwezekani tunapiga kelele hapa halafu mwisho wa siku hakuna kinachofanyiwa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na mazao ya biashara. Ukisoma kwenye taarifa ya Kamati katika ukurasa wa 13 inaeleza katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni mazao haya yamekuwa na uzalishaji usioridhisha kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo pamoja na ufanisi mdogo wa vyama vya ushirika na matumizi duni ya teknolojia ya pembejeo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesahau haya mazao yamekuwa yanaendelea kupotea na wakulima wamekata tamaa. Wakulima wanakata tamaa kwa sababu Mheshimiwa Rais mwenyewe wakati wa kampeni na baada ya kupata nafasi ya Urais amekuwa akizungumzia sana hizi tozo na kodi ambazo mmeweka. Wakulima wamefika sehemu wanakata tamaa. Mimi nitoe mfano Mkoa wa Kagera, haya mazao kwa mfano zao kuu la kahawa siyo Mkoa wa Kagera tu, zao kwa kweli watu hawaoni faida yoyote ya kuliendeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali na nimuombe Waziri wa Fedha na Waziri wa Kilimo, kabla hatujaingia kwenye bajeti na sisi Mkoa wa Kagera tumetoa azimio na ninaomba Mikoa mingine mtuunge mkono hatutakuwa tayari kuunga mkono bajeti kama hamtaondoa hizi tozo na kodi ambazo zimewekwa. Tunataka wakulima hawa wafaidi. Hili ninaomba Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono. Haiwezekani mkulima analima hapati faida yoyote, ni lazima tujenge mazingira mazuri hata mkulima anapolima aweze kupata faida. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni maji. Kama wengine walivyochangia kwa kweli suala la maji ni tatizo na janga kubwa la Kitaifa. Tuliishauri hapa Serikali tukasema iongeze tozo lakini Serikali ikakataa ikaja na sababu, leo hakuna Mbunge ambaye anaweza akasimama akasema kwenye Jimbo lake kuna pesa ya maji ambayo imepelekwa angalau hata asilimia 30. Mimi ninaiomba Serikali tunaposhauri muwe mnazingatia. Ninajua mna nia njema lakini kuna mambo mengine lazima muwe mnatusikiliza na sisi tunaposhauri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani tukasimama tukaitetea Serikali wakati Serikali hampeleki pesa, kwenye Majimbo yetu wananchi wanateseka hali ni ngumu. Tunahitaji maji, Mheshimiwa Waziri wa Maji, Kyerwa wananchi wamenituma maji sitakutetea hapa usiponiletea maji, na kuna miradi ambayo tayari tumeshaibuni iko kwenye usanifu, hiyo miradi inahitaji pesa. Kuna miradi mingine ambayo ipo ya miaka ya mingi, hii miradi ipo tu wananchi wanakuuliza tunakosa hata majibu. Kwa hiyo, niombe Serikali izingatie hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee migogoro ya ardhi. Kuna migogoro ya ardhi maeneo mengi. Kwa kweli kwa hapa nimpongeze Waziri kwa kazi wanayoifanya, lakini bado kazi ni kubwa na migogoro hii ni mikubwa, isije ikatokea sasa mauaji yanatokea kila kona. Mimi niwaombe kwa mfano kule Kyerwa kuna eneo ambalo lilishatengwa na Serikali ikatangaza kuwa hili eneo ni la wafugaji. Lakini eneo hili linaloitwa Sina limevamiwa na watu, wengine hawakufuata hata taratibu wameingia wameweka fence ni kama Serikali haioni. Haiwezekani wanaweka hivi vitu Serikali inaona na inajua hili eneo ilishalitenga kwa ajili ya shughuli fulani. Mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri wa Ardhi uje Kyerwa utatue huu mgogoro uishe, tujue nani ana haki ya kuwa kwenye hili eneo kihalali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niiombe sana Serikali, mje hapa mtueleze Waheshimiwa Wabunge kwa nini mpaka sasa hamjapeleka pesa kwenye miradi ya maendeleo. Mlete sababu ambazo tutawaelewa kuliko kukaa kimya pesa haiendi na sisi hatujui kinachoendelea, hata wananchi wanapotuuliza, tunakosa jibu. Ni afadhali mkatueleza kama pesa haipo tujue pesa haipo hilo tukawaambie wananchi, kuliko tunakaa hapa tu kila mtu anazungumzia pesa ya maendeleo na hakuna kitu kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali, ninajua nia ya Rais wetu na dhamira yake, kwa kweli tunamuunga mkono, lakini tunataka pesa. Hatuwezi tukaunga mkono tu kitu kinasemwa, kinasemwa halafu hatuoni kinachoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine niongelee uharibu wa mazingira. Mazingira yetu kwa kweli yameharibiwa sana. Na niombe sana Waheshimiwa Wabunge katika hili, tushirikiane wote kwa pamoja ili tuweze kunusuru mazingira yetu ambayo yameharibiwa. Vyanzo vya maji vimeingiliwa, wakulima wanaingia humo humo, milima na misitu yetu leo haipo tena, leo tunaongelea janga la kitaifa tunasema kuna njaa, kuna ukame. Ukame umesababishwa na sisi viongozi tukiwepo ni hatua zipi ambazo tumechukua ili kunusuru mazingira yetu yawe salama? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tufike wakati sasa siyo kulinda tena kura, wakati mwingine Waheshimiwa wanasiasa mnalinda nafasi zenu hamtaki kuingilia kwenye mambo ambayo ni ya msingi. Watu wanapoharibu mazingira unasema nikisema hapa nitajiharibia kura, unajiharibia wewe. Mwisho wa siku tunakuja kuomba chakula cha njaa, tuhakikishe tunaenda kwa wananchi wetu tuyalinde mazingira yetu ili mazingira yawe salama. Haya mambo ya kusema tunalinda kura wakati nchi inaharibika, tunakoelekea ni kubaya. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge hili tupambane nalo kwa nguvu zetu zote kuhakikisha mazingira yetu tunayarudisha kwenye hali ambayo ni sawa, ili tupate mvua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la mwisho watu wanatangaza janga la njaa, kweli njaa ipo lakini siyo kama…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Bilakwate.