Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia hoja hii iliyopo Mezani. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniongezea timu katika Wizara yangu. Katika wiki hizi mbili ameteua Kamishna Mkuu mpya wa Magereza, Kamishna Mkuu wa Uhamiaji aliyeteuliwa leo, Kamishna Mkuu wa Kupambana na Madawa ya Kulevya na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai. Hawa ni watu wa muhimu sana katika kazi hii. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niwaambie, ndiyo kwanza kazi inaanza. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, niwashukuru sana Kamati kwa ushauri ambao wamekuwa wakitupatia Wizara. Niwaambie tu kwa ujumla wao mapendekezo na ushauri wote ambao wametupatia tutaufanyia kazi na hasa tunapoelekea katika maandalizi ya bajeti ya mwaka unaofuata. Nakushukuru sana Mwenyekiti wa Kamati, wewe umekuwa dictionary yetu nzuri katika Wizara hii ukizingatia institutional memory uliyonayo ya kufanya kazi katika Wizara hii pamoja na timu yako. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo tumelipokea, mmeongelea sana suala la vitendeakazi pamoja na maslahi ya askari wetu wa vyombo vyote ambavyo viko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani. Wenzetu wa Wizara ya Fedha tayari wameshatusaidia baadhi ya vitu ambavyo vilikuwa vinadaiwa na askari wetu. Kuna baadhi ambavyo tayari wameshaanza kutoa na tunaamini kwa kadri ambavyo wamekuwa wakijitahidi wataendelea kutoa na vingine. Kwa hiyo, jambo hilo linafanyiwa kazi na stahili hizo zimekuwa zikitolewa na hivyo kupandisha morali ya kazi ya vijana wetu. Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunasubiria magari, Waheshimiwa Wabunge wengi katika maeneo yenu mmeongelea suala la magari. Ni kweli nimepita katika maeneo mengi ambako nimeona umbali na uhitaji wa magari kwa ajili ya operesheni pamoja na mambo mengine ni mkubwa. Niwaahidi, tutatoa vipaumbele kwa kadri ya maeneo yalivyo kadri tutakavyokuwa tumepata magari hayo ili kuweza kuongeza tija ya usalama wa raia pamoja na mali zao katika maeneo yenu, tutalifanyia kazi hilo. Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea pia maombi ya vituo, tutaendelea kushirikiana nanyi na hamasa mnazozifanya katika maeneo yenu ili hili nalo liweze kupewa uzito unaostahili. Sisi tutajitahidi kwa kadri ya uwezo wetu kuweza kuhakikisha tunatengeneza mazingira hayo. Nia yetu ni moja ya kuweza kuhakikisha mazingira ya askari yanaendana na kazi wanayofanya ili raia waweze kujizalishia mali katika mazingira ambayo ni salama na wao waweze kufanya kazi wakiwa salama. Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo limeongelewa na Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge ni lile linalohusu wakimbizi pamoja na makazi ya wale raia ambao walipewa uraia baada ya kukaa kwa muda mrefu. Jambo hili tunaendelea kulijadili na wiki ijayo tutakaa kikao cha pamoja kuweza kujadiliana. Mambo ambayo tunategemea kuyajadili ni pamoja na njia nzuri. Wazo hili lilipoahirishwa mwanzoni ilikuwa hawa watu wapewe fedha za kwenda kuanzia maisha sehemu nyingine. Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Wizara mtazamo wetu uko sawasawa na mtazamo wa Kamati kwamba hatuwezi tukawapa watu uraia halafu wakatengeneza kanchi kao ndani ya nchi yetu kwa kukaa eneo lao, kwa kuwa na uongozi wao, wana lugha yao moja na tabia zao moja. Watu wakishapewa uraia wa Tanzania wanakuwa Watanzania na wanatakiwa waishi kwa desturi na Katiba ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo ambalo tutajadiliana na development partners pamoja na sisi wenyewe kuweka huo msimamo na tutalitolea uamuzi katika Serikali. Tutawajulisha Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge kwa kadri tutakavyopata muda na forum zetu hizi ambazo ni za Kibunge za kupeana taarifa. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa upande wa wakimbizi tulifuta utaratibu wa wakimbizi kuingia kwa ujumla kwa sababu hali ya mara baada ya tension za kisiasa na kabla na sasa ilivyo ni tofauti. Kwa hiyo, tunatengeneza utaratibu ule ikiwa ni pamoja na udhibiti ili kuweza kudhibiti uhalifu kwani kuna wengine wanaweza wakaingia kwa gia ya ukimbizi na wakafanya vitu ambavyo ni vya kihalifu. Hii inadhihirika katika ukanda ambako wakimbizi wapo jinsi ambavyo matukio ya uhalifu yamekuwa yakizidi maeneo mengine na upatikanaji wa silaha ambazo si za Tanzania ukizidi katika maeneo hayo. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine na Mheshimiwa Naibu Waziri alilisemea kwa kiwango kikubwa nampongeza kwa hilo linahusu namna ya kuifanya Magereza ijitegemee. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu tayari ameshaitisha kikao ambacho kitafanyika Jumatatu lakini lengo lake ni namna ya kutumia fursa tulizonazo katika Magereza kwenda kwenye uzalishaji. Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nilipokuwa najibu swali nililisemea kwamba tunataka Magereza ambayo yana maeneo ya uzalishaji tuyatumie kwenye uzalishaji. Tutatoka kwenye uzalishaji wa kizamani kwenda kwenye uzalishaji wa kisasa ili maeneo yote yale yazalishwe kwa zaidi ya asilimia 85. Tukifanya hivyo tuna uhakika Magereza yatajitegemea kwa chakula lakini hata kwa fedha kwa sababu tunaamini uzalishaji huo ukishazidi kuna baadhi ya mazao ambayo tutauza NFRA pamoja na maeneo mengine na vilevile tunaweza hata tukapeleka kwenye shule za bweni ili watu wetu waweze kupata chakula hicho. Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho lililoongelewa sana ni hili la madawa ya kulevya. Vita hii ya madawa ya kulevya ni vita ya kila Mtanzania na vita hii haijaanza sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi tangu nilipofika nilikuta tayari Mheshimiwa Kitwanga ameshakamata mapapa wakubwa tu na tulivyotoka pale tumeendeleza. Ninachowaambia Waheshimiwa Wabunge tunaweza tukatofautiana mtazamo kwenye approach na ninyi kama Wabunge na kama washauri wetu mkitushauri njia nzuri ya kufanikisha jambo hili sisi mara zote tutakuwa tunapokea ushauri huo. Kwa sababu vita hii si ya mtu mmoja, mkituambia tukifanya hivi tutafanikiwa zaidi maana yake vita ni yetu sote, sisi tutaendelea kupokea ushauri. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja tu ambalo nawahakikishia na ambalo nawaomba wote tuwe nalo, tusibadili lengo la kuhakikisha tunapambana na vita ya madawa ya kulevya, tuendelee nalo. Mheshimiwa Rais alishatoa dira hiyo na sisi wasaidizi wake tunatembea katika nyayo zile kuweza kuhakikisha tunafanikiwa hilo. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wengine walikuwa wanasema mbona Waziri hujasema, nimeshazunguka mikoa yote kasoro Njombe, Ruvuma, Singida na Songwe. Kwenye mikoa yote huko nilikopita nimetoa maelekezo ya makosa ambayo ni ya kipaumbele ya kufanyiwa kazi:- Moja, ni madawa ya kulevya, kila mkoa nimeelekeza, si jambo la mjadala. Mbili, ni uhalifu wa kutumia silaha, nimesema si jambo la mjadala. Tatu, nimesema ni ubakaji, si jambo la mjadala. Nne, nimesema ni ujangili, si jambo la mjadala. Tano, nimesema yale masuala yanayohusisha ugaidi, si mambo ya mjadala. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikishatoa maelekezo kama hayo sibinafsishi tena hiyo shughuli…
Mtanzania ambaye linamhusu jambo hili popote pale alipo na mkiwepo Waheshimiwa Wabunge lazima tusimamie mambo haya kwa upana wake kwa maslahi ya Taifa letu. Jambo likishakuwa la aina hii kila mmoja anatakiwa atimize wajibu wake. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge katika masuala haya ambayo ni ya Kitaifa tushirikiane wote, tusaidiane wote. Watu huwa hawagombani kwa ajili ya kazi, watu wanasaidiana kazi, tusaidiane kazi kuweza kuhakikisha kwamba inapofanikiwa inakuwa yetu sote na inaposhindikana tunakuwa tumeshindwa wote kama Taifa. Taifa letu likipata hasara, Taifa letu likipata aibu tunakuwa tumepata aibu wote. United we stand divided we fall, twende pamoja tuweze kuhakikisha kwamba tunafanikiwa katika mambo haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.