Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami niweze kuchangia kidogo katika hoja hii muhimu iliyokuwa mbele yetu. Kwanza na-declare, ni Mjumbe wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma na nimeshiriki kikamilifu na nipongeze sana hotuba hii ya Kamati kwa asilimia zote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tulifanya ziara kadhaa katika mashirika kadhaa ya umma lakini pia tuliweza kufanya ziara kadhaa katika makampuni hapa na pale ili kuangalia uwekezaji ambao taifa letu imefanya. Nishukuru sana Mashirika hayo aliyoonesha ushirikiano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza nijikite moja kwa moja katika hoja iliyopo ambapo bado inaonekana kuna tatizo kubwa sana la kusaini mikataba ambayo taasisi zetu za umma zimekuwa zikifanya na wawekezaji mbalimbali. Mfano; Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kilisaini mkataba na kampuni kutoka Botswana inaitwa Mlimani GH na mkataba huo ni wa miaka 50 ambapo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Serikali itakuwa inapata asilimia 10 tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonesha jinsi gani ambavyo tumekuwa tukisaini mikataba hiyo, lakini pia inaonesha kwamba baada ya matumizi hayo na uwekezaji huo na Serikali kupata hiyo asilimia 10 baada ya miaka 50 ndiyo Serikali itakuja kunufaika na kupewa hayo majengo. Kwa mtaji huo tunarudi kule kule kwenye business as usual kwa sababu hakuna mtu ana guarantee kwamba Mlimani City kwenye miaka 50 ijayo itakuwa kwenye hali gani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii inapelekea Taifa letu kukosa magawio, lakini pia imekuwa ikipata hasara kubwa na kushindwa kuchangia katika Mfuko Mkuu wa Serikali na mwisho wa siku kuleta mzigo mzito sana kwa Watanzania. Kwa hiyo, moja kati ya Kamati ilipopitia na kuona, imeona kwamba mkataba kama huu uliofanywa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam umekuwa ni mkataba ambao ni mzigo mzito sana kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tangu sijawa Mbunge wa Mikumi, nilikuwa nikisikia mkataba uliokuwa ukiendelea kati ya TANESCO na IPTL, tunaweza kuona kwamba mkataba huu pia umeonekana kuwa mzigo mzito na sisi tulikuwa tukisikia katika Bunge la 2014, Novemba. Bunge hili liliamua kwamba ule mkataba usitishwe na zile mali ziweze kutaifishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Waziri atakapokuja hapa tuweze kujua mkataba huo umeishia wapi kwa sababu umeonekana kuwa mzigo mzito sana kwa Watanzania, kwa sababu Tanzania inaonekana kulipa shilingi milioni 300 kwa IPTL. Kwa hiyo, inaonekanaka milioni 300 kwa siku, ni mzigo mkubwa sana kwa Taifa letu ambalo kila siku tunasema bado liko kwenye hali ya checheme checheme. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hiyo, mashirika mengi ya umma yamekuwa yakiilalamikia Serikali, imekuwa ikiyapa madeni mazito, inakopa katika masuala haya ya msingi. Mfano, katika taasisi za umma kama TANESCO, inaidai Serikali pesa nyingi, lakini pia suala la maji safi na taka inadai pesa nyingi. Vile vile mifuko ya kijamii imekuwa ikidai pia pesa nyingi sana kwa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi Juni 2016 imeonekana kwamba Serikali inadaiwa trilioni mbili nukta sita na PSPF. Kwa hiyo, unaweza ukaona jinsi gani Serikali imekuwa ikipeleka mizigo mizito sana kwa hii mifuko ya kijamii ambayo sasa ili kuweza kututumka imeanza kupeleka hili gao la mafao sasa hivi watu wanaambiwa mpaka wafikishe miaka 55. Mpaka hapa ninavyoongea nimepigiwa simu na watu wangu wa Kilombero Sugar Company wananiambia walikuwa wakitaka kusaini na PPF kwenye fomu zao lakini wameambiwa wasubiri mpaka miaka 55. Huo ni mzigo mzito sana kwa Watanzania ndugu zangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba sana Serikali iweze kulipa madeni yake ambayo inadaiwa na taasisi zake. Hiyo nimetaja mfano tu wa PSPF lakini mifuko mingi ya kijamii inaonekana kukopwa na Serikali bila kulipwa kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine, tunajaribu kuangalia migongano ya Sera na Sheria. TR ndiyo msimamizi wa mashirika yote ya umma lakini inaonekana mifuko hii ya kijamii inapotaka kwenda kufanya manunuzi au inapotaka kufanya michanganuo ya kujiendesha na kuweka uwekezaji imekuwa ikipata miongozo kutoka sehemu tofauti. Mara huku wanaambiwa na BOT, mara huku wanaitwa na SSRA miluzi mingi inampoteza mbwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mifuko hii ya jamiii inaonekana kwamba inashindwa jinsi ya kwenda kwa sababu TR anakuwa hana taarifa rasmi za kuhusu uwekezaji unaotaka kufanyika kwa sababu viongozi wa sehemu mbalimbali wakiwemo BOT pamoja na SSRA wameonekana kuwa wakitoa miongozo tofauti kitu ambacho kinapelekea mashirika haya kwenda kununua bidhaa au kununua viwanja na ardhi kwa bei kubwa ambayo inapelekea mashirika haya yajenge nyumba kwa pesa nyingi ambazo mwisho wa siku Mtanzania maskini ndiyo anataabika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua Shirika la Nyumba kama NHC linataka kujenga nyumba ambazo zitakuwa na uwezo na kumfanya mwananchi wa kawaida aweze kumudu lakini kwa gharama ambazo zipo hadi sisi Wabunge tunaanza ku-beep kwamba jinsi gani tunaweza tukanunua hizo nyumba hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo nyumba zinazosemwa za bei nafuu tumeenda kukagua juzi mradi wa NHC kule Chamazi ni hela nyingi sana ambayo kiukweli kwa maskini wa Kitanzania itakuwa ngumu sana kuweza kuchukua nyumba kama hizo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana pamoja na yote, lakini pia kwenye Bodi za Wakurugenzi wameonekana wakichaguliwa watu ambao hawana uwezo kiasi kwamba wanapeleka mashirika mengi kufa na mashirika mengine pia kuweza kuwa na watendaji ambao ni wabovu. Wakurugenzi wengi wanaoteuliwa wanateuliwa kirafikirafiki na wengine wanapewa ahsante ahsante, kitu ambacho kinapelekea mashirika yetu ya muhimu kwa Taifa letu kuweza kufa.
Mheshimiwa Mwenyekiti,Kwa hiyo tunashauri upatikanaji wa Watendaji hao uweze kufanyika kwa recruitment ili waweze kushindanishwa na wafanyiwe interview ili majina matatu yaweze kupelekwa kwenye mamlaka ambazo zinaweza kuteua mmoja atakayekuwa na tija na kusaidia mashirika yetu ya umma kwa ajili ya kwenda kufanya hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mambo mengine yanayosumbua ni pamoja na wanasiasa kuingilia mashirika haya ya umma ambayo mengine yanafanya biashara. Utasikia kuna miongozo kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara fulani mara Naibu Waziri anasema hiki na hiki, fungu liende huku, kitu ambacho kinapelekea matatizo makubwa sana kwenye haya mashirika yetu ya umma na kufanya mengi yaweze ku-stuck na kushindwa kuendelea na kazi ambayo wamekuwa wakiifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nisisitize tunahitaji kuwaachia watendaji wetu wakuu ambao tumewapa madaraka na mamlaka ya kuweza kuongoza ili waweze kutupeleka kwenye sehemu nzuri itakayopeleka uwekezaji wenye tija kwa sababu tumeshuhudia sehemu mbalimbali watendaji hao walikuwa wanafanya kazi chini ya kiwango lakini tumeendelea kucheka na nyani na mwisho wake Tanzania inaendelea kuvuna mabua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe sana ndugu zangu nitakapokuja hapa mtupe majibu jinsi gani ambavyo mtaweza kuwezesha Ofisi ya TR ili aweze kuwa na meno na nguvu ya kuweza kuyasimamia mashirika haya ambayo sasa hivi madaraka yake TR anaonekana kuwa ameporwa na sasa hivi anafanya kazi nusu nusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja.