Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kidogo kwenye eneo hili la viwanda na uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nichukue nafasi hii niwashukuru sana na kuzipongeza Kamati zote kwa kazi nzuri walizozifanya ambazo zinatupa matumaini. Vilevile nataka niipongeze sana Serikali yangu kwa dhamira nzuri ya kwenda kwenye nchi ya viwanda Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niombe sana, tunapozungumza viwanda nadhani tuna tatizo moja kubwa sana la mikoa ya kusini, hasa hasa Mkoa wa Ruvuma. Hivi sasa tunazungumza habari ya viwanda, lakini Mkoa wa Ruvuma mwaka 2008 ulitenga eneo maalum kwa ajili ya kuweka viwanda. Eneo hili toka mwaka 2008 hadi leo na liko Songea Mjini wale wananchi hawajalipwa fidia, wanaishi maisha ya shida na Serikali haina dalili ya kuonesha lini wataanza kulipa fidia za wananchi wale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wenzangu hapa Waheshimiwa Wabunge wanavyozungumza viwanda katika maeneo yao mie mwenzenu mnaniacha gizani kwa sababu hata hilo eneo la viwanda halipo. Kwa hiyo, nataka niiombe sana Serikali ione umuhimu wa kuhakikisha wale wananchi ambao wanafikia 1,085 wanalipwa fidia zao ili waweze kupisha eneo la kujenga viwanda na ili mipango ya Serikali iweze kufanikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, EPZA imechukua zaidi ya heka 5,000 na Waheshimiwa Wabunge hebu fikirieni mjini kuwa na heka 5,000 kwa ajili ya shughuli za uwekezaji ambazo hazijalipwa mnaona jinsi wananchi wa maeneo yale wanavyoteseka sana na shughuli hiyo. Kwa hiyo, naomba sana, Serikali ione umuhimu wa kuwalipa wananchi hawa. Nitatoa hoja kama haitakuja bajeti ya kulipa watu fidia na basi safari hii nitakwenda sambamba na Mheshimiwa Waziri ili kuhakikisha shilingi ile ya kwake naikamata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nataka niombe sana. Wenzetu wengi katika mapinduzi ya viwanda walijali sana wazawa wao. Sisi tunazungumza sana viwanda lakini tunawahamasisha watu na sidhani kama tumejiandaa vilivyo ili kuhakikisha Watanzania wenyewe ndio wanapata nafasi kubwa zaidi ya kuingia kwenye uwekezaji katika viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maandalizi ya kuwafanya Watanzania waingie katika viwanda yako mambo mengi; lazima tuwe na program maalum ya kuwafanya Watanzania wajiandae kisaikolojia kwamba sasa tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda. Lazima tufike mahali tuwe na mitaala maalum ya kuwafundisha wanasayansi na watafiti ili ifike mahali watakaoendesha viwanda hivyo na watakaoweza kuvihudumia viwanda hivyo iwe ni Watanzania wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wenzetu katika nchi nyingine kama China wanafikia mahali wananchi wao wanapewa mikopo ya kuweza kuanzisha shughuli za viwanda kwa ajili ya kujenga uchumi kwa wananchi wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Tanzania lazima tujiandae, tunajua mabenki yetu yalivyo, ni vizuri tukajiandaa tuweke programu maalum ili Watanzania wapewe kipaumbele katika kuanzisha viwanda na wapate mikopo ya kuweza kuanzishia viwanda hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunavyo viwanda vidogovidogo SIDO na VETA tuna wataalamu wetu, ingawaje hawajapata elimu ya kutosha lakini viwanda vile tuna uwezo kabisa wa kutengeneza program za kuhakikisha tunawapandisha viwango na uwezo wataalam wetu SIDO na VETA ili waje kuwa wawekezaji wazuri katika shughuli za viwanda. Kwa hiyo, nataka niombe sana Serikali iwe na utaratibu mzuri wa kuwafanya Watanzania wenyewe wapate uwezo wa kuwekeza katika viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilitaka niombe sana Serikali iwe na utaratibu mzuri wa kuwafanya Watanzania wenyewe wapate uwezo wa kuwekeza katika viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nilikuwa nataka niangalie upande wa pili vilevile, tumekubaliana kimsingi kwamba hivi viwanda vyetu rasilimali yake kubwa ni kilimo. Lakini tujiulize hivi tumejiandaa vipi kilimo chetu kingia kwenye uzalishaji wa viwanda? Maana hata mtu akianzisha kiwanda cha parachichi leo nina uhakika hatuna uwezo wa kuzalisha maparachichi ya kutosheleza kiwanda cha parachichi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni vizuri kujiandaa kikamilifu kwamba, je, wakulima wetu wanaandaliwa vipi kuweza kuviwezesha viwanda viweze kufanya shughuli zao za uzalishaji? Na kwa maana hiyo, lazima tufike mahali tuangalie mfumo wa benki zetu namna utakavyoweza kuwakopesha wakulima wazalishe mazao ya kutosha mengi, ili mazao hayo yatumike katika kuingiza kwenye shughuli za uchumi wa viwanda; vinginevyo tunaweza tukajikuta tunatengeneza viwanda ambavyo malighafi unaitafuta kutoka nje ya nchi yetu na hii haitakuwa na faida kubwa kwa Watanzania wenyewe. Mwenyekiti, Maana viwanda hivi tunavitazamia vizalishe ndani ya nchi, lakini viwanufaishe wananchi kwa maana ya kutafuta raw materials, lakini vilevile viweze kupata soko la uhakika la matumizi ya viwanda hivyo.
Mheshimiwa Nilikuwa naomba Serikali iweke programu maalum na itengeneze mazingira mazuri ya kuwafanya wakulima waweze kuingia kwenye uzalishaji wa mazao ambayo yatakuwa ndiyo malighafi katika shughuli za viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nishukuru. Nizishukuru Kamati zote na niipongeze sana Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya katika shughuli za kuandaa mazingira ya viwanda; naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana.