Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano.
Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo wametuletea Mpango huu wa Miaka Mitano ambao umezungumzia mambo ya msingi na muhimu kabisa kwa ajili ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo la muhimu kabisa ambalo napenda kuisisitiza Serikali ni kwamba iwekeze zaidi katika suala la nishati. Tumeona jinsi ambavyo Serikali katika miaka mitano iliyopita imeweza kuwekeza kwenye nishati na tumeona jinsi ambavyo kuwepo kwa nishati hii kwa asilimia 30, wananchi wengi wameweza kunufaika kwa kutumia umeme ambao upo mpaka vijijini. Kwa hiyo, napenda kusisitiza sasa kwamba Serikali iongeze uwekezaji katika suala zima la umeme hasa vijijini ili tutakapokuwa na umeme wa uhakika vijijini, itawezesha wananchi wetu kuweza kujiajiri katika shughuli mbalimbali za kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile tunaona jinsi ambavyo Awamu ya Tano tumekusudia kujenga viwanda, kwa hiyo kwa kuwa na umeme maeneo yote ya vijijini na mijini tutaweza kuongeza uwekezaji kwa suala zima la viwanda na vijijini wawekezaji wataweza kuwekeza katika viwanda. Kwa hiyo, niombe tu Serikali katika suala zima la umeme iongeze fedha nyingi katika Mpango huu wa miaka mitano ili tuweze kuona wananchi wengi hasa wa vijijini ambao kwa kipindi kirefu walikuwa hawana umeme waweze kunufaika zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika suala la madini, Serikali imesema kwamba itawezesha sekta muhimu za kiuchumi ikiwepo sekta ya kilimo na madini. Napenda kuomba Serikali iwekeze katika suala zima la madini hasa kwa wachimbaji wadogo kwa kuongeza mitaji ili kuwawezesha vijana wengi waweze kujiajiri. Wapo vijana wengi sana ambao wanatumia nguvu zao katika shughuli mbalimbali za kiuchumi hasa katika uchimbaji wa madini, lakini wanakosa vifaa muhimu kwa ajili ya uchimbaji wa madini.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imeona iangalie sekta hizi za kiuchumi kuweza kuziboresha zaidi, napenda kutoa msisitizo kwamba Serikali iongeze fedha hasa kuwawezesha wachimbaji wadogo kuwapa zana bora za kuweza kufanyia shughuli za kiuchumi ili vijana wengi waweze kujiajiri katika sekta hiyo ya kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nina mapendekezo pia katika suala zima la maji. Ni muhimu sana Serikali iangalie uwezekano wa suala la maji hasa vijijini. Kwa miaka iliyopita tumeona jinsi ambavyo wananchi wengi hasa vijijini hawana maji safi na salama. Kwa hiyo, ili wananchi tuweze kufanya shughuli zetu vizuri na yaweze kupatikana maendeleo endelevu, tunapenda pia katika Mpango huu tuongeze fedha nyingi sana katika suala zima la upatikanaji wa maji safi na salama hasa vijijini ili akinamama ambao wamekuwa wakitumia muda mrefu kwenda kutafuta maji umbali mrefu zaidi ya kilomita tano wapate nafuu. Wakiweza kupatiwa maji safi na salama na kuwa karibu zaidi nina uhakika nguvu zao nyingi wataweza kuwekeza katika shughuli za kiuchumi zaidi na wengi wataweza kuongeza pato la Taifa hili la Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vile vile katika maeneo ambapo tumezungukwa na maziwa kwa mfano katika Kanda ya Ziwa tumezungukwa na Ziwa Viktoria. Napenda kutoa msisitizo kwamba Serikali iweke mpango mkakati wa kutosha ili tuweze kuvuta maji kutoka Ziwa Viktoria na maziwa mengine kwa maeneo ambayo yamezungukwa na maziwa. Hii itawezesha wananchi walio wengi kuweza kupata maji safi na salama.
Mheshimiwa Spika, inasikitisha sana kuona kwamba nchi hii ya Tanzania tumezungukwa na mito, maziwa kama nilivyosema Ziwa Viktoria limetuzunguka lakini wananchi hawana maji safi na salama. Kwa hiyo, niombe sasa katika Mpango huu wa Miaka Mitano, Serikali hebu iwekeze vizuri, iweke mkakati mkubwa wa uhakika wa kuhakikisha kwamba inavuta maji kutoka Ziwa Viktoria na maziwa mengine ili wananchi waweze kufikiwa na maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika miaka iliyopita tumeona jinsi ambavyo Serikali wameweza kuvuta maji kutoka Ziwa Viktoria mpaka Kahama sasa yanaelekea Shinyanga yanaenda mpaka Tabora lakini Mikoa ambayo tumezungukwa na ziwa kama Geita wananchi hawana maji safi na salama. Kwa hiyo, nichukue tu fursa hii kusisitiza kwamba kwa kuwa imeweka kwenye Mpango wake hebu sasa iangalie uwezekano wa kupata fedha za kutosha iwekeze katika suala zima la upatikanaji wa maji ili maji haya yawezeshe shughuli mbalimbali kwa sababu huwezi ukawa na viwanda bila ya kuwa na maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba Serikali iangalie suala la maji kwa uhakika kwa sababu maji ni changamoto kubwa. Tumeona jinsi ambavyo kila mmoja hapa anasimama anasema naye ana changamoto hiyo ya maji. Kwa hiyo, suala la maji liwe kipaumbele katika mpango mkakati wa miaka mitano hii ili wananchi wetu waweze kunufaika na kuweza kufanya shughuli zao vizuri kwa sababu wana maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tunajua pia suala la maji ni uhai, tukiwa na maji safi na salama hata afya za wananchi zitakwenda vizuri. Ndiyo maana napenda kusisitiza sana Serikali ijikite katika kuhakikisha kwamba maji safi na salama yanapatikana kwa wananchi wa Tanzania wakiwemo wa Mkoa wa Geita ambapo tuna changamoto sana ya maji. Tumezungukwa na ziwa lakini hatuna maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo lingine la msingi kabisa katika Mpango huu ambalo limenigusa, nimeona jinsi ambavyo Serikali imejipanga kuwekeza katika suala zima la reli ya kati. Ili tuweze kuwa na uchumi imara, ni vyema Serikali ikawekeza zaidi katika reli. Nami naunga mkono kabisa iweke mpango mzuri kuwekeza katika reli ya kati kwa standard gauge ili kuwezesha usafirishaji wa bidhaa muhimu kutoka bandari ya Dar es Salaam kwenda katika mikoa ya pembezoni ambayo iko mbali na bahari ya Dar es Salaam ambako ndiko kwenye bandari kuu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile tunajua nchi yetu ya Tanzania imezungukwa na nchi mbalimbali ambazo hazina bahari. Nina uhakika kwamba tukijenga hii reli kwa sababu kupitia hii reli ya kati ambayo inakwenda Mikoa ya Kigoma na mikoa mingine mpaka nchi za jirani Burundi, Rwanda na sehemu mbalimbali uchumi utaimarika. Kwa hiyo, katika miaka mitano hii Serikali ikiwekeza katika mpango mzima wa reli ya kati na kuiwezesha vizuri kabisa nina hakika uchumi wetu wa Tanzania utaweza kuimarika vizuri zaidi na tutaongeza mapato ya Taifa kwa sababu wenzetu wa nchi za jirani wataweza kutumia bandari yetu ya Dar es Salaam na kuweza kuongeza pato letu la Taifa katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo vilevile na sisi ambao tunatokea mikoa ya pembezoni tutaweza kupata bidhaa katika bei nafuu zaidi. Kwa sasa hivi unakuta bei ya simenti Dar es Salaam inauzwa kwa bei ndogo mfuko Sh.15,000/= lakini ukifika Geita mfuko huo huo unauzwa Sh.22,000/= mpaka 25,000/=. Kwa hiyo, tunaona jinsi ambavyo maisha ya wananchi yanakuwa ni ya gharama kubwa sana, lakini Serikali ikiwekeza katika reli nina uhakika hata usafirishaji wa bidhaa muhimu kama simenti na vitu vingine itawezesha bei ya bidhaa kuwa bei ambayo inamwezesha Mtanzania hata wa hali ya kawaida kuweza kufanya shughuli zake za kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vile vile katika suala la reli, napendekeza kama kuna uwezekano tuweze kujenga hata bomba la mafuta kwenye njia hiyo hiyo ya reli kutoka Dar es Salaam kwenda mpaka Mikoa ya Kanda ya Ziwa hiyo ya Tabora kuelekea Kigoma hata katika nchi za jirani. Hii itasaidia kupunguza bei ya mafuta kwani kwa sasa hivi Dar es Salaam lita moja inauzwa Sh.1,400/= lakini ukifika Mikoa ya Geita, Mwanza bei inakuwa imepanda zaidi inakuwa zaidi ya Sh.2,000/=.
Mheshimiwa Spika, haya yote yatawezekana ili kuboresha uchumi wetu pale ambapo tutafikiria kuwa na bomba la mafuta kutokea Dar es Salaam kwenda katika mikoa ya pembezoni, Mikoa ya Kanda ya Ziwa na mikoa mingine ambapo itatuwezesha kuinua uchumi halisi wa wananchi katika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vile vile katika suala zima la miundombinu, ni vizuri sasa Serikali iangalie katika mkakati wake ambao umekuwa nao na Sera ya Taifa ya kuunganisha kati ya mkoa kwa mkoa, wilaya na wilaya kwa barabara za lami. Napenda kuunga mkono kwamba Serikali iendelee kuwekeza fedha ili tuweze kuunganisha kwa barabara za lami mikoa kwa mikoa, wilaya kwa mikoa na wilaya kwa wilaya. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile tuangalie hata ile mipango mikakati iliyopita pamoja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliyopita. Kwa mfano, katika Mkoa wangu wa Geita katika Ilani tulikuwa tumekusudia kujenga barabara ya lami kutoka Geita kuelekea Kahama kupitia Bukoli lakini vile vile kujenga barabara ya lami kutoka Geita kwenda Bukombe ambayo ni wilaya mpya katika Mkoa wa Geita. Kwa hiyo, niombe Serikali pia iangalie yale mambo yaliyokuwepo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliyopita ihakikishe inayafanyiwa kazi ili wananchi tuweze kunufaika zaidi. Kwa sababu tukiwa na barabara za lami Mkoa kwa mkoa, wilaya kwa wilaya, wilaya kwa mkoa, nina uhakika wananchi wengi wataweza kunufaika kwa sababu wataweza kusafirisha mazao yao vizuri na watafanya biashara zao vizuri na kwa uhakika na mwisho wa siku pato la Taifa litaweza kuwa la uhakika na litainuka na tutakuwa na uchumi ulio bora katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, kwa kuwa Serikali hii imekusudia kuwekeza katika suala zima la viwanda na mimi kila nikisimama nimekuwa nikizungumzia suala la viwanda na mikoa mingine kama ya Geita ambayo ni mipya haina viwanda. Niiombe Serikali kwa kuwa imeamua kuwekeza katika masuala ya viwanda, tuiangalie mikoa hii kwa kuanzisha viwanda kutokana na rasilimali zinazopatikana kwenye maeneo yale.
Mheshimiwa Spika, naomba ikiwezekana tujengewe hata kiwanda cha simenti. Katika Kanda ya Ziwa hatuna kiwanda cha simenti hata kimoja. Wananchi wanahangaika sana kupata simenti, bei ni ghali sana ndiyo maana watu wanashindwa kujenga nyumba bora kwa sababu bei ya simenti ipo juu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ni ya viwanda, niombe awamu hii tuhakikishe Kanda ya Ziwa tunakuwa na kiwanda cha simenti ili wananchi waweze kunufaika kutokana na rasilimali ambazo tuko nazo katika maeneo yetu. Sambamba na hilo, tuangalie pia kwa kikanda kwamba kanda hii inazalisha mazao fulani tuwekeze viwanda vya aina hiyo kulingana na mazao yanayopatikana katika maeneo yale.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, napenda kutoa msisitizo kwamba Serikali iangalie uwezekano wa kuwekeza zaidi katika masuala ambayo nimeyazungumzia, suala la umeme na viwanda katika maeneo yote ili wananchi wetu waweze kushiriki katika kuhakikisha kwamba uchumi wao unaweza kuinuka kwa sababu bila ya ushiriki wa wananchi wa kawaida haiwezekani uchumi kuinuka zaidi. Niombe tu Serikali itilie mkazo katika kuona kwamba yale ambayo imezungumzia katika Mpango ya Miaka Mitano yafanyiwe utekelezaji maana wakati mwingine tunapanga mipango lakini utekelezaji wake unakuwa ni asilimia ndogo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe yale ambayo tumeyapanga kwa miaka mitano hii tuhakikishe basi tunayafanyia kazi kama ni fedha tutafute fedha ili tuweze kuyatekeleza na kuhakikisha kwamba uchumi wetu unainuka kwa sababu ya uwepo wa mambo ambayo tumeyapanga katika miaka hii mitano na kwamba yametekelezwa hatua kwa hatua.
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja nikiomba Serikali ihakikishe inayafanyia kazi mambo yote niliyoyazungumza. Ahsante sana.