Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nina dakika ngapi?
MWENYEKITI: Una dakika saba.
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia fursa ya kuchangia kuhusu hoja iliyoko mbele yetu. Kwanza kabisa napenda nianze kwa kuishukuru Kamati yangu ya Kudumu ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa ushauri na mapendekezo ambayo imeyatoa katika Wizara yangu. Niseme tu kwamba kwa sababu ya muda niliopewa, haitakuwa rahisi kujibu hoja zote zilizojitokeza, kwa hiyo, naomba nijielekeze kwenye masuala machache, kadri ya muda utakavyoruhusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala la mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu, ambalo limezungumzwa na Kamati, lakini pia limezungumzwa na wachangiaji wengi. Kuna vipengele vingi ambavyo vimezungumzwa kuhusiana na mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu. Kwanza ni suala la vigezo vya utoaji mikopo ambavyo kwa sasa tunaangalia uyatima, uhitaji, ulemavu, pamoja na vipaumbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri kwamba hivi vigezo vina matatizo na ninafurahi kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba tayari Wizara yangu imeshaunda Kamati ambayo imepitia hivi vigezo na kuleta mapendekezo ambapo tarehe 28 tulikaa na Kamati yangu ya Kudumu na kuvipitia, nawahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tunapoanza mwaka 2017/2018 katika bajeti hii, tutakuja na vigezo ambavyo vitakuwa vimeboreshwa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la utoaji wa mikopo na kwamba kuna baadhi ya wanafunzi ambao walikuwa wanapata mikopo lakini mikopo yao imefutwa, niseme kwamba Wizara yangu imekuwa ikihakiki wanafunzi wa elimu ya juu ambao wana sifa za kupata mikopo. Wale wote ambao hawana sifa, bila kujali kwamba yuko mwaka wa ngapi, tunawafutia mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nililisema hata katika Bunge la mwezi Novemba. Nasisitiza kwamba huo ndiyo msimamo wa Serikali. Kuna wengine ambao walikuwa wamepata mikopo kwa sababu walidai kwamba wao ni yatima; tumepeleka vile vyeti vya vifo vya wazazi RITA na tukabaini kwamba ni vyeti vya kughushi. Kwa hiyo, tumefuta na tutaendelea kuhakiki na wale wote ambao wamepata mikopo kwa njia ya udanganyifu, hao tutaendelea kuwaondoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la urejeshaji mikopo. Ninakubaliana na Kamati kwamba kwa kweli kasi ya urejeshaji mikopo hairidhishi kabisa. Napokea ushauri wa Kamati kwamba kama Serikali kwa kweli tunapaswa kuimarisha urejeshaji wa mikopo kwa sababu hadi kufikia Juni, 2016 Serikali ilitoa jumla ya shilingi trilioni 2.5 lakini ambazo zimekwisharejeshwa ni shilingi bilioni 147.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utaratibu huu hatuwezi kutegemea kwamba Serikali iendelee kuongeza wigo wa utoaji mikopo wakati urejeshwaji hauko imara. Kwa hiyo, hatua ambazo Serikali tunazichukua, kwanza tumeongeza kato badala ya 8% kuanzia mwezi huu ni 15%. Nitumie fursa hii kuwataka waajiri wahakikishe kwamba wanafanya makato ya mikopo na kuyawasilisha kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nihamie katika eneo lingine ambalo limezungumzwa ambalo ni suala la udahili wa wanafunzi katika elimu ya juu. Hili suala limezungumzwa sana kwamba TCU amegeuka kuwa dalali wa udahili katika vyuo vya binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Serikali inaliangalia suala hilo. Katika udahili wa mwaka 2017/2018 Serikali itafanya mapitio na kuja na mfumo ambao utakuwa na tija zaidi ili vyuo binafsi navyo vijione kwamba vina jukumu la kuboresha elimu yao na kuhakikisha kwamba vinajitangaza kutokana na ubora wa elimu na siyo kutegemea kupata wanafunzi kupitia mgongo wa TCU. Ushauri umepokelewa na utafanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo limezungumzwa ni suala la upatikanaji wa vitabu. Nikiri kwamba kumekuwa na uchelewaji wa usambazaji wa vitabu kutokana na changamoto ambazo zilijitokeza katika suala zima la manunuzi. Nafurahi kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba leo Wizara yangu imeanza kusambaza vitabu 2,426,135 kwa ajili ya kidato cha nne mpaka cha sita. Tunategemea kusambaza vitabu takribani milioni 5.5 kuanzia wiki mbili zijazo. Kwa hiyo, hilo suala la upatikanaji wa vitabu, changamoto ambazo ni za manunuzi zilizochelewesha tutazifanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala moja tu kuhusu elimu ya msingi kwa sababu limezungumzwa sana. Kuna suala ambalo limeulizwa kwamba, je, hii Sera ya Elimu Msingi ya kwamba wanafunzi wanamaliza mpaka kidato cha nne imeanza kutekelezwa au la?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine wamekuwa na maoni tofauti, napenda kutoa ufafanuzi kwamba suala la elimu ya msingi kwamba mwanafunzi atasoma kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne limeainishwa katika Sera ya Elimu ya mwaka 2014. Ili matamko ya sera yaanze kutekelezwa, inahitaji kutungwa sheria, kanuni na taratibu. Kwa sasa sheria inayoongoza jambo hilo bado. Nawahikishia Watanzania kwamba jambo hili litakapoanza kutekelezwa mtajulishwa, lakini kwa sasa hivi bado halijaanza kutekelezwa, elimu yetu bado ni miaka saba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.