Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia hii fursa ya kuwa mchangiaji katika hoja muhimu iliyo mbele yetu. Naomba niseme awali kabisa kwamba naunga mkono hoja. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukiangalia ukurasa wa 26 kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu; huduma za kiuchumi; amebainisha kwamba Serikali iko kwenye mchakato wa kuanzisha mfumo unganishi; mfumo wa kuweka kumbukumbu za ardhi, mfumo funganishi wa kuhifadhi
kumbukumbu za ardhi na tayari wameshaanza kujenga.
Mheshimiwa Spika, jambo hili ni zuri na nitaomba liharakishwe na liweze kukamilika kwa wakati kwa sababu litatusaidia sana katika kuondoa migogoro ya mara kwa mara ya ardhi ambayo kwa kiasi kikubwa ukiangalia inachangiwa na kutokuwa na utaratibu mzuri wa kuweka kumbukumbu za ardhi katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, nyote mnafahamu kuna mgogoro mkubwa kule Misenye uliochukua muda mrefu, lakini ukiuangalia ule mgogoro kwa nini umechukua muda mrefu, sababu kubwa ni kutokuwepo kwa mfumo wa kuweka kumbukumbu za ardhi; na hasa kutokuwa na kumbukumbu
za kielektroniki. Nitaeleza hoja tano kwa nini nasema kutokuwa na mfumo huu kumechangia sana kuleta migogoro ambayo ingeweza kuepukika?
Mheshimiwa Spika, la kwanza, ramani inayotumiwa na NARCO kwa mfano, ramani inayotumiwa na NARCO na iliyotumika katika kugawa blocks kule Misenyi. Ramani hiyo kwanza inatumika kwa siri kubwa, lakini ramani yenyewe ukiwauliza NARCO wenyewe kwamba iko wapi hawawezi kukupa ramani ambayo inatumika; kila mtu anatumia ramani yake kulingana na anavyoona inafaa.
Mheshimiwa Spika, siku moja nilisikitika sana nilipoelezwa na mtaalam mmoja kwamba ramani waliyonayo iliyoanzisha Misenyi Ranch, mpaka ukishavuka Mto Kagera kwenda mpaka Uganda yote ni Misenyi Ranch. Sasa maana yake, mwenye ramani ile na anayetumia ramani
ile anakuwa hatambui na anapuuza ukweli kwamba katika eneo hilo kuna Vijiji, Kata na watu wanaishi. Pia ukiangalia hata blocks zenyewe zilizotengwa katika Misenye Ranch, migogoro iliyopo kati ya blocks na vijiji inasahau ukweli kwamba vijiji vilikuwepo kabla Ranch haijaanzishwa. Kwa hiyo, hii imekuwa ikileta mgogoro.
Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nasema tukiwa na kumbukumbu za vijiji, maana vijiji vinapimwa, vinakuwa na hati, ziwe kwenye mfumo mmoja ili mtu asitoe hati juu ya hati. Maana kwa kufanya hivyo, matokeo yake inakuwa ni kuleta vurugu.
Mheshimiwa Spika, pia ukiangalia ni kwamba mipaka ya blocks zile zilizotengwa inabadilishwa kila kukicha na tuliowapa hizi blocks wana mamlaka siku hizi wanabadilisha blocks kadiri wanavyoona inafaa. Akiamka asubuhi anaanza kutembea anaweka mipaka na leo kwa mfano nimeletewa taarifa zaidi ya kaya 3,000, sasa ni displaced persons ni watu ambao wapo ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
lakini hawana sehemu ya kuishi, wameondolewa katika maeneo yao.
Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ambayo inatokana na kutokuwepo na mfumo wa kuweka kumbukumbu, sote tunafahamu kwamba vijiji katika Misenye Ranch vilikuwepo kabla ya ranch na mipaka inajulikana kwamba ni Mto Kyaka, Kuru na Kigoroga lakini historia hii imepotoshwa, hakuna anayejua historia hii na kumbukumbu hazipo.
Mheshimiwa Spika, tuna tatizo lingine kubwa ambalo sote tunalijua ni kati ya misitu. Kwa mfano kule Minziro ukiangalia migogoro inayojitokeza kule Kata ya Minziro ni mipaka kati ya Minziro kama Kata na Vijiji vilivyo ndani ya Kata ile na Msitu wa Minziro.
Mheshimiwa Spika, sasa nasema ndiyo maana nimefurahia sana huu utaratibu wa kuanzisha mfumo unganishi wa kuweka kumbukumbu za kieletroniki ukianzishwa na taarifa zinaonesha unaanza itatusaidia sana. Hilo ni jambo la kwanza, ndiyo maana nimesema naunga mkono hoja hii kwa sababu inakuja na utaratibu ambao unaweza kutusaidia.
Mheshimiwa Spika, pia migogoro mingi ya ardhi tuliyonayo; iliundwa tume hapa ya kusaidia kutafuta ufumbuzi hadidu za rejea na akasema jambo moja kubwa kwamba tuwe na subira. Akatuomba viongozi tuwe na subira, tusubiri hiyo tume imalize kazi yake.
Mheshimiwa Spika, matarajio yangu tume hiyo ikimaliza kazi yake Wabunge watapewa fursa ya kupokea ripoti hiyo na kushirikishwa kama tulivyoahidiwa; lakini subira hii naona Mheshimiwa Waziri Mkuu iko kwa wanasiasa tu, lakini kwa viongozi wengine kule Kagera, wao hawana
subira yoyote. Hawasubiri cha tume, wala nini, wanaendelea kila mtu anafanya anavyoona anataka.
Mheshimiwa Spika, hivi sasa ninapozungumza imetolewa ultimatum ya miezi minne watu wote kuondoka na kwenda kule watakapoona inafaa; jambo ambalo mimi kama mwakilishi wao silikubali, kwa sababu limetolewa kabla hata Tume yenyewe iliyoundwa kufuatilia suala hili
haijatoa taarifa yake.
Mheshimiwa Spika, ni vizuri wakati wanasiasa tunaombwa kuwa na subira, basi hawa Waheshimiwa wengine nao niombe pia na wao wawe na subira. Subira ikiombwa kwa upande mmoja tu, hiyo siyo subira; sote ni viongozi lengo letu ni moja. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, wananchi waliniomba kule wakasema Mheshimiwa inaonekana sasa ng’ombe wanapendwa kuliko watu, nikawaambia hapana watu kwanza, ng’ombe baadaye. Wakaniomba wakasema Mheshimiwa sasa uturuhusu tushike fimbo tuweze kupambana; nikasema hapana, siwezi kuwaruhusu kwa sasa kwa sababu tuliombwa tuwe na subira. Kama ukifika wakati huo, basi mimi nitakuwa wa kwanza kuongoza mapambano hayo lakini kwa sasa tuwe na subira. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.