Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Stephen Julius Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi pia ya kuchangia bajeti hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Spika, nami nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake ambayo inatoa dira ya mipango ya maendeleo ya Serikali. Nitumie nafasi hii pia kuwapongeza Mawaziri, Mheshimiwa Jenista Mhagama, kwa kazi nzuri na anaonesha kweli akinamama wanaweza. Nimpongeze pia Naibu Waziri kijana, Mheshimiwa Anthony Mavunde kwanza kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya kuwaunganisha vijana wa Tanzania lakini pia kwa programu ile ya mafunzo ya vijana ambayo anaifanya. Nimwombe tu programu hiyo pia ifike Shinyanga kwa sababu kuna vijana wengi wanahitaji programu kama hiyo na kusema kweli kama vijana wenzako hujatuangusha.
Mheshimiwa Spika, kipekee sana kwa niaba ya wananchi wa Shinyanga nataka nimshukuru sana Mheshimiwa Rais. Alipofanya ziara Shinyanga alitoa maelekezo kwa Mamlaka na Wizara ya Maji kushughulikia tatizo la bei ya maji Shinyanga. Kama Mheshimiwa Shabiby
alivyosema, leo nazungumzia kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu kwa sababu bado hatujaona jitihada za Waziri wa Maji kushughulikia tatizo la uendeshaji wa Mamlaka ya Maji Shinyanga.
Mheshimiwa Spika, maji ni huduma ya msingi, maji sio anasa. Shinyanga na mikoa ya Kanda ya Ziwa ni mikoa michache ambayo ina chanzo cha maji cha uhakika cha Ziwa Victoria. Serikali imetumia shilingi bilioni 250 kujenga Mradi wa Maji wa Ihelele, kodi za Watanzania, leo Wizara
haiweki msisitizo wa kutunza mitambo ile. Shilingi bilioni 250 hazijamaliza hata miaka 10, Serikali haipeleki pesa za kutunza mitambo ile. Ni asilimia 25 tu ya mitambo ile ndiyo inafanya kazi, asilimia 75 haifanyi kazi. Ipo mikoa mingine kama Arusha wanahangaika vyanzo vya maji, Gairo huku amezungumza Mheshimiwa Shabiby wanahangaika na vyanzo vya maji, lakini sisi tuna chanzo cha maji cha uhakika lakini hatukitunzi, tumeweka shilingi bilioni 250 hatutunzi.
Mheshimiwa Spika, wiki iliyopita Shinyanga, Kahama, Ngudu, Igunga ambayo yote yapo kwenye Mradi huu wa Ihelele yanatakiwa yapelekewe maji lakini hayajapelekwa. Mradi ule umekatiwa umeme, siku nne wakazi wa Shinyanga hawana maji kwa sababu Serikali haijapeleka mchango wake wa asilimia 60 wa kuendesha mradi ule. Sasa wananchi wanapata adhabu ambapo wamelipia bili zao za maji wanastahili wapate huduma wanaikosa huduma kwa uzembe wa watu wengine, hii inasikitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mradi ule hauwezi kuharibika kwa uzembe wa watu wachache. Nimwombe Waziri, namheshimu, ni rafiki yangu, akae na Wabunge wa Kanda ya Ziwa ambao wanahusika na ule mradi wa maji tushauri namna bora ya uendeshaji wa mradi ule. Mradi ule ukiweza
kuwafikia watumiaji wengi, kwa mfano wa Ngudu, Kwimba, Igunga, Nzega, Tabora, Sikonge na kwa capacity ya mradi ule unaweza kuleta maji mpaka Mkoa wa Dodoma. Pampu zile nane zikifunguliwa zote Dodoma inaweza kupata maji ya Ziwa Victoria. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, andiko la mradi ule linaweza kuhudumia watu milioni 10. Leo ni wakazi wa Manispaa ya Shinyanga ambao hawafiki 200,000 na wakazi wa Mji Mdogo wa Kahama ambao hawafiki 200,000 ndiyo wanahudumia gharama za uendeshaji za mradi wa shilingi bilioni 250. Naomba Serikali iangalie kwa upana mradi huu. Naomba pia Serikali iongeze bidii za kusambaza haya maji kwenye vijiji vile vinavyohusika, zile kilometa tano vijiji vile vipate maji.
Mheshimiwa Spika, lakini yapo mambo ambayo tunaweza kumshauri Waziri, kwa mfano, mamlaka hizo zote mfano SHUWASA na mamlaka nyingine, kwenye vifaa vya mabomba kwa mfano vya kuunganisha maji, vimewekewa kodi, kuna SDL iko pale, kuna VAT iko pale. Vitu kama hivi vikiondolewa kwa sababu maji ni huduma, gharama za uendeshaji wa mamlaka hizi zitakuwa chini na hatimaye wananchi watapata huduma ya maji kwa gharama nafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini pia madeni hayalipwi. Sasa taasisi muhimu kama Mamlaka za Maji zinakatiwa huduma, nilikuwa naangalia television, Kigoma pale wananchi wanagombania maji kwa sababu mamlaka imekatiwa maji. Shinyanga pale tumekatiwa maji siku nne, tuna viwanda pale vya maji, kuna viwanda vya soda, wananchi wanakosa maji eti kwa sababu bili ya KASHUWASA haijalipwa na huyo KASHUWASA hiyo pesa anayotakiwa atoe inatakiwa itolewe upande wa Serikali. Sasa sisi wananchi tumelipa bili tunataka huduma tu. Tunapata adhabu kwa sababu ya watu wengine. Hospitali haina maji, imagine hospitali ya mkoa inayopokea wagonjwa zaidi ya 200 inakatiwa maji. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimezungumza hili kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu kule nyumbani wananchi wamenituma wamesema tunataka nizungumzie suala la maji. Naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu suala hili ulisimamie kwa karibu kwa sababu pale tumeweka pesa nyingi za walipa kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Manispaa ya Shinyanga imejengewa mtandao wa maji safi lakini hakuna mtandao wa majitaka, majitaka yote yanayonyonywa hakuna pa kuyapeleka. Naomba Serikali itenge fedha kwenye bajeti hasa ya Waziri wa Maji, tujenge mtandao wa maji taka kwa sababu ulikuwepo kwenye andiko la mradi huu kwamba lazima na mitandao ya majitaka pia ijengwe. Leo majitaka pale Shinyanga hakuna pa kuyapeleka, mbaya zaidi hata vifaa vinavyokuja vyote ikiwemo na mita zinakuja mita feki, bili za wananchi zinachakachuliwa, wananchi wanapigwa bili kubwa kwa mita feki zinazokuja.
Mheshimiwa Spika, naomba Waziri asimamie hizi mamlaka kwa karibu, aangalie hata hizo mita zinazoagizwa, huyo mtu aliyepewa tenda ya kuagiza mita ziwe zina ubora unaostahili sio kuwaibia wananchi kwa kuleta mita ambazo ni feki, zinaongeza gharama za uendeshaji, zinaongeza bili ya maji kwa wananchi. Wananchi wangu bado hawana uwezo mkubwa wa kubeba mzigo wa gharama za kuhudumia maji ambayo kimsingi Serikali ilitakiwa isaidie ruzuku ili kuweza kuhakikisha mradi huu unawafikia watumiaji wengi.
Mheshimiwa Spika, tukiongeza foot print ya mradi huu gharama zile tutagawana wote, maji yale yafike mpaka Tabora, Sikonge, Ngudu, Sumve, Igunga, Singida na Malya, wote wapate yale maji ili tuweze kugawana gharama za uendeshaji. Tusipofanya hivyo tutaendelea kubeba msalaba huu sisi peke yetu na mradi ule utakufa kwa sababu hatuna uwezo wa kuuhudumia. Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.