Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi hii na mimi kuweza kuchangia hoja iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Spika, nami nianze na suala zima la maji. Suala hili limekuwa ni changamoto kubwa sana kwa Watanzania wa nchi hii. Nitazungumzia suala la maji kwa Manispaa ya Dodoma, lakini pia nitazungumzia suala la maji kwa Wilaya ya Chemba.
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Chemba tuna Mradi wa Maji Ntomoko. Mradi huu umeanza mwaka 2014 na ulikuwa una gharama ya shilingi bilioni 2.8. Mradi huu ulitakiwa kuhudumia vijiji 18 lakini ni kwa bahati mbaya sana katika vijiji 18 vijiji nane vikaondolewa vikabaki vijiji 10. Kati
ya hivyo vijiji 10 hivi ninavyoongea hakuna kijiji hata kimoja ambacho kimepata maji kutokana na mradi huo na mpaka sasa mkandarasi ameshalipwa shilingi bilioni 2.4, maji hakuna.
Mheshimiwa Spika, Mradi wa Maji Ntomoko ulidhamiria kupeleka maji kwenye kituo cha afya ambacho kinatumika kama Hospitali ya Wilaya ya Chemba. Hospitali ile haina maji, miundombinu ya maji imeshaharibika. Mwanamke mjamzito anapokwenda hospitalini kupata huduma ya kujifungua sharti ndugu zake waende na ndoo ya maji kichwani ili mwanamke yule aweze kupata huduma ya maji. Kama ndugu zake wakishindwa kwenda na maji mwanamke yule atapata huduma ya kujifungua, atafungashiwa uchafu wake atakwenda nao nyumbani kwake kwenda kupata huduma ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, suala la maji ni kero katika Taifa letu, ni shida katika nchi hii. Tatizo la maji katika Taifa hili siyo suala la upatikanaji wa vyanzo vya maji kwani tunavyo vya kutosha sana. Shida ya Taifa hili ni mfumo wa namna ya kuyasambaza maji hayo kuwafikishia Watanzania kwenye maeneo yao, vyanzo vya maji vipo vya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, maji ya Ntomoko ninayokwambia siyo maji unayokwenda kuyachimba bali ni maporomoko ya maji unakwenda kuyatega wananchi wanapata maji, imekuwa ni shida kweli kweli. Shilingi bilioni mbili watu wamelamba, wamekaa kimya, Watanzania wanapata shida na suala la maji. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mimi niseme ule mradi kwa kuwa ulikuwa ukamilike mwezi wa Pili mwaka huu umeshindikana na hakuna sababu zozote za msingi ambazo Watanzania wa Wilaya ya Chemba wanapewa, tunaomba huo mradi uondolewe kwetu ili tutafutiwe mradi mwingine mbadala utakaoweza kuleta tija na utakaofanya wananchi wetu waweze kupata maji. Nimeamua kulisemea hili kwa Waziri Mkuu ili na yeye aweze kuona kwa jicho la pekee sana hususani kwenye ile hospitali ambayo watu wanakwenda kupata huduma pale. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye suala zima la maafa. Mfuko wa maafa uko kwenye ofisi ya Waziri Mkuu. Kama unavyojua nchi yetu imekumbwa na ukame na hali ya chakula katika Taifa letu siyo nzuri kwenye maeneo kadhaa na hususan katika Mkoa wangu wa Dodoma hali ya chakula ni mbaya sana. Nilisema hapa siku ya Jumatatu kwenye briefing kwamba Watanzania wa Mkoa wa Dodoma
kuna njaa ya kutosha na imekithiri.
Mheshimiwa Spika, hapa ninapoongea, debe la mahindi Dodoma Mjini hapa sokoni pale Mwembeni na Majengo ni Sh.23,000, kilo ya mahindi wanapima Sh.1,250. Kondoa debe ni Sh.25,000, Chemba ni Sh.27,000, Kongwa kwako pale Kibaigwa ni Sh.22,500. Sijaona kwenye kitabu cha Waziri Mkuu akituambia suala la ukame katika Taifa hili katika yale maeneo ambayo yana changamoto ya bei kubwa za mazao ni nini amekifanya au anatarajia kufanya kitu gani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hii si sawa, hatuwatendei haki hawa Watanzania wetu. Watu wanakufa, watu wanajiua, wanaume Wilaya ya Kondoa wawili wameamua kujiua kwa sababu familia zao zimekosa chakula kwa muda wa siku tatu. Wanaume wanakimbia familia zao, wanawake ndiyo
wanaobaki kwenye majumba na watoto wao lakini mwanamke huyo naye mvua Dodoma safari hii haijanyesha ya kutosha. Hata vibarua mwanamke aende akalime apate fedha ya kununua kilo ya mahindi hakuna. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ningetaka kujua ni lini Serikali itatuletea chakula watu wa Dodoma. Tunahitaji chakula watu wa Dododma na naamini hata wewe unahitaji chakula kwa ajili ya watu wa Kongwa. Mheshimiwa Waziri Mkuu watu wa Dodoma tunaomba yale mahindi yanayooza Shinyanga tani 8,000 tunazihitaji watu wa Dodoma tuna shida na chakula, acheni kuozesha chakula wakati watu wanakufa kwa njaa. Kama ninyi upande wa pili hamuwezi kusema sisi tuacheni tuseme, tuko hapa kwa ajili ya kuwasemea Watanzania. Hatuko hapa kwa ajili ya kuona nafsi zetu ziko salama lakini kesho tutakuwa huko na sisi mitaani maana yake kazi hii siyo ya kudumu. Niombe nipate ufafanuzi kwenye suala hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye suala la Mahakama. Mahakama zetu zimekuwa ni changamoto kubwa sana hususani kwenye upande wa watumishi, lakini pia kwenye suala zima la miundombinu kwa maana ya majengo yako. Wilaya yangu ya Chemba haina hata hiyo
Mahakama ya Wilaya tu.
Mheshimiwa Spika, pili, Mahakama hizi za Mwanzo ambazo ziko kwenye Kata zetu kule chini ziko kwenye nyumba za watu ambao wamejitolea, lakini hata hao wahudumu unakuta kuna Karani mmoja na Hakimu mmoja anayeweza kuzunguka kwenye Kata zaidi ya nane, ameenda Kata chache sana ni Kata tano. Tuone ni namna gani tunaongeza Watumishi kwenye sekta hii ama kwenye Wizara hii ya Mahakama ili wananchi wetu waweze kupata huduma hii kwa urahisi lakini pili kwa uharaka ili waweze kuendelea na shughuli zingine. (Makofi).
Mheshimiwa Spika, lingine ni migogoro ya ardhi. Kaka yangu Mheshimiwa Shabiby amezungumzia tu mgogoro wa kwako kule pamoja na kwake. Kuna mgogoro kama huo wa Kiteto, mgogoro uliko baina ya Wilaya ya Chemba pamoja na Wilaya ya Kiteto ukiwa unahusisha hifadhi ya WMA-Makame. Wananchi wanakufa kule, hakuna vyombo vya habari vinavyoweza kuwamulika watu kwa namna gani wanavyokufa.
Mheshimiwa Spika, hayo matrekta yamechomwa moto hivi ninavyoongea, watu wameshapigwa, kuna watu 18 wameshafungwa jela, Mahakama ya Kiteto lakini kuna watu 27 wapo lock up Kiteto mpaka leo. Kwa hiyo, suala hili la migogoro tungeomba sana lishughulikiwe. Wabunge tuliambiwa tuorodheshe migogoro iliyoko katika maeneo yetu, tumeorodhesha migogoro hii kwa nchi nzima lakini hatupewi ripoti migogoro hiyo imesuluhishwa kwa namna gani na imeishia wapi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu aweze kuona suala la migogoro ya ardhi ndiyo itakayokwenda kutuletea vita ya wenyewe kwa wenyewe. Bila kumaliza migogoro ya ardhi ndoto za kufikia Tanzania ya Viwanda ni hadithi za Abunuwasi. Haitakuwepo kwa sababu ardhi hiyo ndiyo tunayoitarajia Watanzania wetu waweze kutafuta malighafi mbalimbali ili tuweze kuendesha hivyo viwanda ambavyo tunavisema leo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe sana mgogoro wa Kiteto pamoja na Chemba ambao unahusisha pia Makame-WMA ambayo iko Kiteto ambayo hifadhi ile inawanufaisha watu wa Kiteto basi ufanyiwe kazi kwa haraka ili wananchi wale waweze kupata maeneo yao ya kuweza
kulima na waweze kujijengea uchumi wa familia zao lakini na Taifa kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa muda ulioweza kunipatia.