Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nami nampongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri iliyosheheni masuala mengi ya maendeleo ya Taifa letu. Pia nampongeza Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri wote walioko chini ya idara
zake zote nikiamini kuwa ushirikiano wao mzuri unaleta maendeleo mengi tunayoyaona sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nataka kuanza kwa kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuendelea kuinua na kukuza uchumi wetu kwa asilimia saba kwa takribani miaka karibu 10 sasa. Nataka kuiomba Serikali yangu sasa iangalie jinsi ya kutafsiri ukuaji huu wa uchumi kwa wananchi wengi walioko chini. Naomba Serikali yetu sasa hivi mikakati yake yote ijielekeze zaidi kwa wananchi katika maeneo haya.
Mheshimiwa Spika, tunazungumzia kilimo lakini bado hatujakipa umuhimu unaotakiwa. Watu wengi wanapata ajira zao, wanapata uchumi wao kifedha kupitia kilimo, ufugaji, uvuvi na shughuli zilizoko vijijini lakini mpaka sasa hivi dhana ya kilimo inaachiwa wananchi wenyewe kuhangaika peke yao. Sikatai Serikali imeingiza nguvu sana kwenye masuala ya pembejeo na vilevile mafunzo kidogo ya ugani lakini haujawa ni mkakati wa kitaifa ambao unaenea kila mahali na kuhakikisha kuwa kila mtu anayelima, anayefuga au anayevua anafikiwa. Tuna mifano ya mikakati ya kitaifa ambayo imefanywa na ikafanikiwa kama REA. Kwa nini tusifanye mambo hayohayo katika masuala ya uzalishaji ili sasa ule ukuaji wa uchumi ukaonekane katika ukuaji wa uchumi wa wananchi mmoja mmoja vijijni.
Mheshimiwa Spika, napenda sana kuhamasisha hili suala kwa sababu najua ukombozi wetu utatokana na wananchi wetu kuweza kuzalisha kwa tija, kuuza kwa tija na kuweza kumudu maisha yao. Nataka kuhamasisha uwezekano wa kuwa na mikakati ya kutoa mafunzo mahsusi
kwa vikundi vya wanawake, wanaume na vijana wanaofanya kazi za kilimo. Isiwe ni programu au mradi mmoja mmoja unaokwenda kule kwa ufadhili mmoja au mwingine lakini uwe ni mkakati wa Kitaifa. Mataifa yote yaliyofaidika na green revolution ulikuwa ni mkakati wa kitaifa. Naomba sana iangaliwe jinsi ambavyo kutakuwa na mkakati wa kuhakikisha kuwa uzalishaji unakuwa wa tija. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sisi wengine tunakotoka kilimo ndiyo kazi kubwa ya wananchi wengi na wengine tunatoka maeneo mazuri sana kwa kilimo lakini tumekwama miundombinu inayounganisha wakulima na masoko. Sasa hatuwezi kuzungumzia kilimo cha tija bila kuwa na miundombinu bora ya usafirishaji, maghala, maji na masuala kama hayo. Tunazungumzia vitu kimoja kimoja bila kuviunganisha, lile suala la mnyororo mzima wa uzalishaji naomba sana lizingatiwe. Mwaka juzi tulizungumzia sana masuala ya maghala pamoja na stakabadhi ya mazao ghalani. Sijausikia sana lakini napenda uendelee kwa sababu hata kule ambako umefanyika umekuwa wa tija sana na wakulima wengi wananufaika na inawasaidia kuondokana na yale masuala ya kulanguliwa.
Mheshimiwa Spika, nataka kuzungumzia suala zima la Maafisa Ugani. Hata kama hatuwezi kuwapata wale wataalam waliosomea degree lakini tufundishe watu vijijini, vijana wasomi ambao wamekaa bure wawe wanafanya hizi kazi za kuraghibisha masuala haya vijijini kwetu ili tuweze kuwa na watu ambao wanatoa taaluma japo kwa kiasi fulani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile nazungumzia masuala ya maendeleo. Kwa kweli nchi yetu ni kubwa sana na kweli sio rahisi kila mahali kukua kwa wakati mmoja. Hata hivyo, kwa miaka hamsini hii kuna maeneo ambayo yamekua sana na kuna maeneo ambayo bado yako nyuma sana. Naomba sana Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla, hebu waangalie na yale maeneo ya pembezoni ambayo yana tija na yana wananchi ambao ni wachapakazi lakini wanakosa zile huduma muhimu kama miundombinu na taaluma mbalimbali za kuwawezesha kukuza uchumi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mimi natokea Jimbo la Ileje, lina mvua nyingi sana, lina udongo mzuri sana, lina misitu lakini tuko nyuma kiuchumi kwa sababu ni Jimbo ambalo halina miundombinu hata kidogo yaani Ileje ni kama kijiji kikubwa. Umeme tunamshukuru Mungu sasa REA inakwenda lakini hakuna barabara ya lami hata moja, maji ni mengi sana lakini haina miundombinu ya kuyapeleka kwa wananchi. Tuna
maeneo mazuri ya kulima lakini wananchi watalima wayapeleke wapi mazao yao wakati hakuna barabara wala masoko? Kwa hiyo, haya ni mambo ambayo tunataka kuomba sasa Serikali hebu katika kuangalia maendeleo tujikite na kule pembezoni nako ili wananchi wa Tanzania
wa kule waone kuwa na wao tunapowapa hizi data za kukua kwa uchumi nao waone kweli wanakua.
Mheshimiwa Spika, nataka kuja kwenye suala lingine la maji. Kama hatuwezi kuzungumzia maji na kuhakikisha kuwa maji yanapatikana kwa kweli tunapoteza muda wetu. Tunazungumzia uchumi wa viwanda, tunazungumzia masuala ya usindikaji, tunazungumzia masuala ya kufuga kwa tija, tunazungumzia umwagiliaji, tutafanyaje bila kuwa na uhakika na maji?
Mheshimiwa Spika, kuna maeneo ambayo yana maji mengi, kuna maeneo ambayo hayana maji kabisa lakini utakuta treatment ni ile ile moja, haiwezekani! Sehemu ambayo ina maji mengi treatment yake au utaratibu wa kuhakikisha hayo maji yanapatikana unakuwa tofauti na kule
ambako hakuna maji kabisa. Kwa hiyo, ionekane kabisa hiyo tofauti lakini kama kila mahali watu wanazungumzia visima hata mahali ambapo kuna maji mengi, haiwezekani! Mimi kwangu sihitaji visima, nahitaji miundombinu ya kunipelekea maji kwa wananchi. Kwa hiyo, hayo nayo yatofautishwe wakati wa kuweka mikakati. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nataka niende kwenye suala la VICOBA, SACCOS na Vyama vya Ushirika. Kwa kweli hili ndilo kimbilio la wananchi wengi kwa sababu mabenki hatuwezi kuyategemea, tumeshaona. Hata hivyo, SACCOS, VICOBA vinajiendesha vyenyewe havina mkakati wa Serikali wa kusema sasa tunatoa mafunzo ya aina hii. Wanaachiwa NGO’s, wanaachiwa taasisi zenyewe kujianzishia vitu vyao, kunakuwa hakuna mfumo ambao unalingana nchi nzima wa VICOBA, SACCOS ambavyo vinaweza vikategemewa hata kuwa ndio njia bora ya kupata mikopo.
Mheshimiwa Spika, najua Mheshimiwa Jenista ananisikia na amekuwa akilifanyia kazi sana ili tusaidie kuwe na mfumo mzuri wa VICOBA na SACCOS nchi nzima, hata kama ni kuwekea utaratibu wa sheria au kanuni ambazo zitatumika kila mahali ili mwisho wa yote hizi SACCOS na
VICOBA ndio zije zitengeneze benki za vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ajira kwa vijana. Ajira kwa vijana ingekuwa ni jambo rahisi sana kulifanya kama tungekuwa tuna njia ya kuhakikisha kuwa tunawaweka hawa vijana pamoja na kuwawezesha. Kwenda kuwaambia tu vijana, ‘mkalime, mkajiajiri’ bila kuwaonesha wakajiajiri vipi au waende wapi ndiyo watapata nini au kuwawekea mitaji au mafunzo, wataendelea kucheza pool, kunywa viroba, kuvuta bangi na kufanya uhalifu wa kila aina. Tuwe na system ya kuwawekea vikosi vya kazi. Mwaka wa kwanza, wa pili na wa tatu tuwawezeshe, mwisho wa yote hawa watakuja kuwa responsible. Kule ambako tunawawezesha mbona wanafanya kazi nzuri sana, sidhani kama vijana ni wakorofi kiasi hicho lakini hawana njia.
Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja.