Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika hii hotuba nzuri ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango inayohusu Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano.
Mheshimiwa Spika, mipango ndiyo msingi wa maendeleo. Kusipokuwa na mipango kutakuwa na ubabaishaji. Kwa maana hiyo, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuja na Mpango mzuri wa Maendeleo wa miaka mitano ambao ndiyo utatuongoza katika uhai wa Bunge letu la Kumi na Moja. Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, katika hotuba yake ameonesha vipaumbele mbalimbali ambavyo vinatuongoza katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa nchi ya watu wa kipato cha kati. Mikakati yenyewe utaiona katika ukurasa wa 25, ambapo amesema Serikali imeweka mikakati ya kujenga na kuboresha miundombinu wezeshi na mambo mbalimbali ambayo ameyasema hapo.
Mheshimiwa Spika, napenda zaidi nijikite katika suala la mradi wa makaa ya mawe wa Mchuchuma na mradi wa chuma wa Liganga. Ulimwenguni pote maendeleo tumeyasoma katika historia na katika vitabu mbalimbali yanasema dhahiri kwamba mageuzi yalitokana na ugunduzi wa moto na ugunduzi wa chuma. Sasa makaa ya mawe yanahusika na uzalishaji wa chuma. Uzalishaji wa chuma hapo hapo tunapata chuma na umeme.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sasa Serikali ikiwezekana ilitazame vizuri suala la mradi huu, kwa sababu inaonekana uko katika sehemu mbili; unaweza ukainufaisha Wizara ya Nishati na Madini na vilevile Wizara ya Viwanda. Kwa bahati mbaya sana, inaonekana mkazo hauwekwi katika kuhakikisha kwamba huu mradi wa chuma wa Liganga unafanikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ni kwa vipi Serikali imeweza kufanikiwa kujenga lile bomba la gesi kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam ikaacha kitu muhimu cha kufanikisha uchimbaji wa chuma? Hiki chuma kinaweza kikatusaidia katika mapinduzi ya viwanda. Maana viwanda vinajengwa kwa kutuma chuma, reli tunaweza tukaijenga kwa kutumia chuma hicho hicho, bandari, madaraja na kila kitu, nondo mbalimbali zinaweza zikapatikana kutokana na chuma. Hata sasa hivi nchi hii ina maradhi na cancer mbaya sana ya vyuma chakavu. Watu wanachukua vyuma kutoka kwenye madaraja, kwenye kila sehemu na matokeo yake sasa kunakuwa na uharibifu mbaya sana kwenye miundombinu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ili kuweza kurahisisha na kuweza kuzuia watu kutoka kwenye eneo la kwenda kuchukua vyuma chakavu katika maeneo ya barabara; unakuta alama za barabarani zinaondolewa, madaraja yanabomolewa; ili watu waweze kuchukua vyuma kwenda kuuza kama vyuma chakavu, kwa nini Serikali isije na mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba chuma cha Liganga kinachimbwa na upatikanaji wa vyuma hivi ukawa ni mwepesi ili kuweza kurahisisha viwanda vya aina mbalimbali; vidogo, kwa vya kati na vikubwa viweze kujengwa katika nchi yetu?
Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni suala la reli ya kati. Reli ya kati ni reli ambayo ndiyo msingi wa maendeleo ya nchi yetu na sehemu ya kupumulia kwa Bandari ya Dar es Salaam. Bandari yetu ya Dar es Salaam ina changamoto kubwa, kwa sababu ndiyo lango kuu la uchumi wa nchi hii pamoja na nchi jirani ambazo ni landlocked, kama nchi ya Congo, Zambia, Malawi, Rwanda, Burundi mpaka Uganda; watu hawa wanategemea Bandari ya Dar es Salaam.
Mheshimiwa Spika, badala ya Dar es Salaam kutegemea tu barabara itakuwa kwa kweli inazidiwa kimashindano na bandari nyingine za nchi jirani. Kwa maana hiyo, naunga mkono kwa dhati kabisa ujenzi wa reli ya kati na reli nyingine zote zinazokwenda kaskazini huko, Arusha na Kilimanjaro pamoja na reli mpya ya kutoka Mtwara kwenda Mbambabay. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali ifanye kila linalowezekana hata kama ni kwa kukopa, pamoja na kwamba deni linaonekana linaongezeka kuwa kubwa, naamini kwamba hawa watakaokuja kuwepo, watakuja kulipa wakati utakapotimia, lakini fedha tunazozikopa tuziweke katika vitu ambavyo tuna imani kwamba vitakuja kuwa ni vya kudumu na wao watakaokuja kulipa walipe wakijua kabisa kwamba sisi tuliokuwepo tulisimama vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, najua Serikali inayo mpango mzuri wa kujipanga kukusanya mapato na tunaamini kwamba nia njema hiyo itaungwa mkono pamoja na Bunge letu Tukufu na naamini kabisa kwamba tutaweza kufanikiwa kwa kutekeleza hii mipango ambayo tumejiwekea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nije katika suala la utalii. Habari ya utalii inaeleweka wazi kwamba ndiyo imekuwa ni chanzo cha fedha za kigeni. Kwa ujumla nashukuru kwamba, Serikali imefanikiwa kuwa inaboresha huduma hizi za utalii na matokeo yake watalii wanazidi kuongezeka. Vile vile nina changamoto katika mapori ya akiba ambayo yapo katika nchi hii. Mojawapo ya pori, lipo katika Wilaya yangu ya Mbogwe, pori la Kigosi Myowosi, tumechangia na Mkoa wa Kigoma pamoja na Wilaya nyingine za jirani za Kahama na Bukombe.
Pori hili Serikali ni sawa na kama imelitekeleza na matokeo yake sasa kunakuwa na shida, vurugu za kila aina kwa sababu wananchi wanapeleka huko mifugo kupata malisho, lakini ukiangalia Serikali yenyewe haijaweka miundombinu wezeshi ya kuweza kuwafanya wananchi waweze kuona kwamba kuwepo kwa hili pori kuna faida kwao, kwa maana ya utalii lakini badala yake wanaona ni bora waingize mifugo yao mle na wakati mwingine hata kulima kwa sababu Serikali yenyewe ambayo imelitenga hailiendelezi.
Kwa hiyo, nashauri tu kwamba, Serikali kama kweli ina nia njema, basi ile mamlaka ya mapori ya akiba ambayo tuliambiwa kwamba sheria yake italetwa hapa Bungeni, basi ije haraka ili iweze kutusaidia kujua kwamba kweli haya mapori sasa Serikali ina chombo kinachoyaangalia na kuyaendeleza.
Mheshimiwa Spika, niseme kuhusu suala la maji ya Ziwa Victoria, Wilaya yetu ya Mbogwe na Mkoa wa Geita tuko karibu na ziwa victoria na kwa maana hiyo nashauri kwamba uwepo mpango kabambe wa kuweza kuzipatia Wilaya zilizo jirani na hili ziwa huduma ya maji kutoka katika Ziwa Victoria. La mwisho, nizungumzie habari ya Wilaya na Mikoa mipya ambayo Serikali imeanzisha kama maeneo mapya ya utawala ili kuweza kuhudumia wananchi kwa karibu zaidi.
Mikoa hii na Wilaya hizi zinazo changamoto mbalimbali ambazo zinatakiwa ziingizwe katika mpango wa miaka mitano ili kuhakikisha kwamba wananchi hawa ambao wamesogezewa hizi huduma, wajisikie kwamba kweli Serikali inawatendea haki. Kwa ajili hiyo, basi kuwe na mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba zinatengwa fedha madhubuti kwa ajili ya ujenzi wa huduma mbalimbali zikiwemo majengo ya utawala, hospitali na miundombinu mbalimbali inayohusiana na utoaji huduma kwa wananchi. (Makofi)
Suala la madini pia liko katika Wilaya yangu. Wachimbaji wadogo wadogo katika Wilaya yetu ya Mbogwe tunayo madini ya dhahabu na kuna Resolute wanafanya utafiti lakini wamekuwa wakifanya utafiti muda mrefu sana matokeo yake sasa kunaanza kuwa na ugomvi kati ya wananchi na huyo mwekezaji.
Mheshimiwa Spika, naomba Wizara ya Nishati na Madini ihakikishe kwamba kwa kweli huyu mwekezaji anaanzisha mgodi, la sivyo arudishe leseni yake wananchi wengine wagawiwe ili waweze kuchimba na kuweza kujinufaisha katika maisha yao ya kila siku.
Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, naomba nikupongeze kwa kunipa nafasi hii na naunga mkono hoja. Ahsante kwa kunisikiliza.