Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mawaziri wake, dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama na ndugu yangu Mheshimiwa
Mavunde kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini kwa kuwasilisha hotuba yao nzuri yenye mwelekeo wa kazi kwa kipindi hiki cha mwaka 2017/2018. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza sana ndugu yangu Mheshimiwa Kassim Majaliwa, Waziri wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kweli amefanya kazi nzuri kwa kipindi hiki cha mwaka mmoja, nasi wananchi wa Lindi tuna matumaini makubwa na yeye na tuko nyuma yake katika kuunga mkono jitihada kubwa anazozifanya katika kuwatumikia Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuchangia katika hotuba yake ambayo ameiwasilisha Mheshimiwa Waziri wetu. Naipongeza sana Serikali kwa jitihada kubwa inayoifanya ya kuongeza kukuza uchumi, lakini kupunguza umaskini wa wananchi wetu katika kuboresha sekta mbalimbali ikiwemo Sekta ya Mawasiliano, Ujenzi wa barabara, Bandari, reli, viwanja vya ndege na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia namna ambavyo Serikali inaendelea kuboresha miundombinu yetu hasa ya barabara na hasa tukiangalia Jiji la Dar es Salaam tumeshuhudia msongamano wa magari unavyoendelea kupungua. Hizi ni jitihada kubwa sana ambazo zinafanywa na Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika jitihada hizi za kuunganisha barabara za mikoa na mikoa na kuendelea kukarabati barabara hizi, ni vizuri sana tukaangalia katika Mkoa wetu wa Lindi kutoka Dar es Salaam, barabara inayokwenda Lindi kuna maeneo ambayo sasa hivi yanasumbua sana. Ukitokea hoteli tatu kwenda Mbwemkuru kuna maeneo yana mashimo mengi sana kiasi kwamba magari hayawezi kupita vizuri. Hata Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania alipokuja katika ziara yake Mkoa wa Lindi aliona namna ambavyo barabara
ile imeharibika hata kama mashimo yale yalitiwa kifusi kidogo, lakini hali ilikuwa siyo shwari.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba barabara hii waitazame kwa sababu kwa kweli tumehangaika katika kipindi kirefu sana tangu uhuru upatikane, lakini tunaishukuru Serikali yetu imejitahidi kuiwezesha barabara hii kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali iendelee kuiangalia vizuri ili iendelee kutuhudumia wananchi wa Mikoa hii ya Kusini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 30 ameongelea vivuko na usafiri majini. Napenda kuishukuru sana Serikali kwamba katika kipindi cha Bajeti hii ambayo tunaimalizia katika eneo la Lindi Manispaa, tulipata pesa shilingi bilioni 1.2 kwa ajili ya kujenga kivuko cha Lindi – Kitunda, lakini hatuoni chochote kinachoendelea.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Kitunda wanahangaika sana hasa wanawake, pindi anaposhindwa kujifungua na analazimika kuja katika hospitali kubwa ya Mkoa kufanyiwa operation namna ya kumsafirisha mtu huyu ni tatizo kubwa sana. Kwa hiyo, naiomba Serikali ituangalie, itusaidie kwa nguvu zote ili tuweze kupata kivuko kiweze kutusaidia wananchi wa Lindi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mradi huu wa LNG, uchakataji wa gesi katika eneo hili la Lindi Manispaa, Kata ya Mbanja, Kijiji cha Likong’o. Eneo hili lilishapimwa na lilishatolewa hatimiliki ya eneo lile na wananchi sasa hawana uhakika tena wa wao kuendelea kuishi pale, lakini wananchi wale hawajapewa fidia zao mpaka leo. Kwa hiyo, naiomba Serikali kuharakisha kwa sababu eneo lile limekuwa siyo lao tena na limeshakuwa sasa ni miliki ya Serikali kupitia Shirika hili la Mafuta. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu sikivu kuwasaidia wananchi hawa ili waweze kupata fidia na wao waweze kujiendeleza katika maeneo mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kwamba Serikali inafanya jitihada kubwa sana katika kuwawezesha vijana wetu kupata mafunzo ya stadi za kazi na ujuzi ili na wao waweze kushiriki katika uendelezaji au uanzishaji wa viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana katika Mkoa wetu wa Lindi tumebahatika kupata Chuo cha VETA na kipo katika eneo la Lindi Manispaa. Tunajua Sera ya Elimu ni kujenga vyuo kila Wilaya, lakini kutokana na uchumi tuliokuwa nao, itachukua muda mrefu sana kuweza kuwa na Chuo cha VETA kila Wilaya. Ombi langu kwa Serikali ni kwamba, chuo hiki kimekuwa kinatoa mafunzo mengi sana pale Lindi, lakini vijana wanaoshiriki ni wachache sana kwa sababu ya ukata wa maisha. Chuo kina changamoto zifuatazo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza hakina mabweni ya kulala wanafunzi, lakini nyumba za Walimu na miundombinu pia ya maji machafu imekuwa ni changamoto kubwa. Kwa hiyo, tuna imani kubwa na Serikali hii. Tunaomba itusaidie sana katika kuhakikisha Chuo kile kinakuwa na mabweni ya kulala wanafunzi ili ndugu zetu wanaoishi katika Wilaya nyingine ikiwemo Liwale, Nachingwea, Ruangwa, Kilwa, Lindi Vijijini nao waweze kushiriki katika kupata mafunzo katika chuo kile cha VETA. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine kubwa sana; wanafunzi wanaosoma pale wanaishi katika nyumba za watu binafsi wakilipa pango, kwa hiyo, imekuwa ni changamoto kubwa sana. Wanajilipia pango wenyewe, lakini hata gharama za maisha za kuishi ni za kwao
wenyewe. Kwa hiyo, imekuwa ni changamoto kubwa sana na wazazi wengi wanashindwa kuleta wanafunzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali itusaidie wakati mipango mingine; mipango ya muda mrefu inaendelea ya kutujengea mabweni, basi ihakikishe inatoa gharama ya chakula kuwapunguzia ukali wa maisha wanafunzi ambao wanasoma pale na nina imani mkitusaidia kutuchangia gharama za chakula, basi wanafunzi wa maeneo mengine ya Wilaya nyingine wataweza kushiriki katika kuja kusoma mafunzo ya ufundi stadi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru sana Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kushirikiana na Jumuiya ya Ulaya na Plan International, tunao mradi wa YEE. Mradi huu unafanya vizuri sana katika eneo letu la Lindi Manispaa na Lindi Vijijini. Kwa hiyo, tunawashukuru sana. Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.