Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. DAIMU I. MPAKATE Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi siku ya leo kuchangia hoja ya hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza naunga mkono kwa asilimia 100.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuunga mkono nataka nianzie kwenye jambo la vijana, Serikali imeagiza Halmashauri zetu kutoa asilimia tano kwa vijana na asilimia tano kwa akinamama, jambo hili kiutekelezaji bado linaendelea kuwa gumu, maeneo mengi Halmashauri zetu hawatekelezi ipasavyo kwa hiyo, inasababisha kudumaa kwa maendeleo katika maeneo yetu ambayo tunatoka.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la wazee kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi tulihubiri sana. Suala la posho ya wazee zaidi ya miaka 65, lakini mpaka leo utekelezaji wake bado haujaonesha dalili kwamba jambo hili litafuatiliwa na wazee wetu kuanza kupewa posho kama tulivyoahidi kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la elimu katika maeneo mengi tunashukuru kiasi ambacho kinatolewa na Serikali kwa ajili ya kuwapinguzia mzigo wazazi, lakini changamoto kubwa tunayopambana nayo katika maeneo yaliyokuwa mengi, hasa Jimboni kwangu, ni juu ya uchakavu wa majengo ya madarasa ya shule za msingi na sekondari katika maeneo karibu yote yaliyopo katika maeneo ya Jimbo langu. Shule hizi zilijengwa miaka ya 1975, 1970, 1980, zilizo nyingi zina umri mkubwa, pengine Wabunge wengine humu ndani walikuwa bado hawajazaliwa, kama ilivyo mdogo wangu Mheshimiwa Goodluck.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa majengo yale yamechakaa, yanapaswa tena kutokana na ongezeko la wanafunzi lilivyo, tuongeze mapya na haya ya zamani yaweze kukarabatiwa ili yawe na hadhi ya kuweza kusomesha watoto wetu katika madarasa yale.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna upungufu mkubwa sana wa walimu, hasa katika Halmashauri yetu ya Wilaya ya Tunduru tuna upungufu mkubwa wa zaidi ya walimu 650 ambao wanapaswa kuwepo katika madarasa kwa sababu maeneo mengi katika shule zangu za msingi walimu hawazidi wanne, watatu, shule chache zina walimu watano mpaka sita. Jambo hili linairudisha sana Halmashauri yetu ya Tunduru kielimu kwa kuwa watoto wamekuwa wengi
lakini kuna upungufu wa walimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, walimu wa awali kwa ajili ya madarasa ya awali hakuna kabisa, anachukuliwa mtu ambaye ana idea kidogo anaenda kufundisha, naomba Serikali ione umuhimu wa kuwafanya walimu wa awali waweze kupata mafunzo, waweze
kuwafundisha watoto wetu ili waweze kuwahudumia ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuliongelea zaidi ni suala la afya katika maeneo yetu. Kwa kweli kuna upungufu mkubwa wa zahanati katika Jimbo la Tunduru Kusini na Jimbo la Tunduru kwa ujumla. Jimboni kwangu kuna vijiji 67, lakini ni vijiji 24 tu ambavyo vina zahanati. Pamoja na kuwepo zahanati hizo 24 bado watumishi katika zahanati hizo ni wachache sana. Kuna watumishi wasiozidi wawili kila zahanati jambo hili linatia doa sana kwa wananchi wetu kwa sababu wanashindwa kupata huduma ile kwa uhahika zaidi kwa sababu idadi ya watumishi katika zahanati hizo imekuwa ni ndogo kwa hiyo, hawapati ile huduma inayotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru tuna Hospitali moja ya Mbesa ambayo miaka ya nyuma, wakati wa Serikali ya Awamu ya Nne, Rais aliahidi hospitali hiyo kuwa hospitali teule kwa niaba ya watu wa Tunduru Kusini. Hospitali ile
inahudumia asilimia 80 ya wakazi wa Wilaya ya Tunduru na Halmshauri yake, lakini idadi ya waganga wako watatu tu.
Naomba Serikali kulingana na mikataba iliyokuwepo na Hospitali ile ya mission basi itekelezwe kuongeza ikama ya idadi ya wafanyakazi wanaotakiwa katika hospitali ile ili waweze kuhudumia watu wetu wa Tunduru kwa ujumla na Wilaya ya jirani ambayo inategemea hospitali ile.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuliongelea, ni suala la kilimo. Tumepiga kelele sana ndani humu, jambo la pembejeo, katika hotuba ya Waziri wa kilimo mwaka jana, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba alizungumzia suala la pembejeo kuuzwa madukani kama soda, ninaomba Serikali ituambie imekwama wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa ruzuku unatugombanisha wakulima na Serikali yao, inagombanisha wakulima na Wabunge, Unagombanisha wakulima na Madiwani, kwa sababu wale wanaochaguliwa kupewa zile ruzuku wanakuwa ni wachache kulingana na idadi ya kaya
zilizopo katika kila kijiji. Naomba sana, mpango ule ulikuwa ni mzuri, kila mtu atakayekuwa na uwezo ataenda kununua pembejeo ile dukani kulingana na hali ilivyo. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali ikafikiria namna ya kutoa ruzuku katika viwanda vyetu vinavyozalisha pembejeo ili viweze kutoa asilimia 100 kwa pembejeo zote zinazozalishwa katika viwanda vile na kusambazwa kwa wakulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi ukazungumzia wakulima ukaacha kuzungumza suala la ushirika. Ushirika huko vijijini ndiyo unaosaidia sana wakulima wetu katika maeneo yaliyokuwa mengi. Hata walio wengi, Wabunge na Madiwani, wametokea katika sekta hii ya ushirika, lakini bado kuna jambo ambalo linafanywa, Serikali bado haijaweza kuiimarisha Tume ya Ushirika ili iweze kufanya kazi yake vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba Serikali ihakikishe Tume hii inapewa meno kwa kuipa viongozi wanaotakiwa kwa maana ya Mwenyekiti wa Tume na Wajumbe wake ili waweze kusimamia ushirika huu uweze kufanya kazi vizuri. Mbili, naomba Serikali ihakikishe kwamba,
watumishi wa Tume wanaenea kutoka Mikoani mpaka Wilayani ili kuhakikisha kwamba wanasimamia ushirika ipasavyo, wakulima waweze kupata tija katika mazao yao wanayozalisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, utakuta kwamba kwa mfano sekta ya korosho wanaushirika wengi wanajiendesha bila usimamizi wowote, hata kama ni mtoto wako umempa ndizi kila siku anaanza kuuza sokoni, anakaa mwezi mzima hujamtembelea ukajua amepata shilingi ngapi, siku ukimuuliza atakupa majibu ambayo hayataendana na wazo lako amepata kiasi gani kwa muda huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili linaendana pamoja na ushirika, tunawatumia hawa kwa muda wote, lakini kwa sababu wamekosa usimamizi wa biashara yao kwa muda wa miezi mitatu, minne tunaporudi kuwahakiki tunakuta kuna matatizo mengi, wakulima wanakosa malipo yao bila maelezo ya kutosha kwa sababu Maafisa Ushirika wa kusimamia zao hili la korosho wanakuwa ni wachache kwa kipindi kile cha msimu wa korosho wanashindwa
kuwasimamia kuhakikisha kwamba pesa wanayopelekewa inanunua korosho kama ambavyo imekusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa sana niliongelee ni mgawo wa maeneo ya utawala. Tunduru ni kubwa sana, inalingana katika eneo la ukubwa na Mkoa wa Mtwara na Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru imeanza tangu 1905. Mkoa wa Ruvuma naamini
ndiyo Halmashauri ya kwanza, lakini kuna Halmashauri tano, saba zimezaliwa Tunduru iko palepale. Kutoka eneo moja mpaka lingine naamini Naibu Waziri wa TAMISEMI amefika pale ameona. Kutoka mwanzo mpaka mwisho kilometa 200 unatembea mtu anatafuta huduma kwa ajili ya Halmashauri yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba maombi yetu yafikiriwe tuhakikishe kwamba, Majimbo yote mawili yanakuwa na Halmashauri zinazojitegemea ili tuweze kuwahudumia watu wetu kwa haraka. Kwa sababu tunavyozungumza zahanati kama nilivyozungumza mwanzo ziko 24, mtu anatembea zaidi ya kilometa 30 hadi 40 kufuata huduma za afya. Utapozungumza hospitali ya Wilaya iko zaidi ya kilometa 80 hadi 100 ili kuipata hospitali hii. Mkitugawia maeneo haya mambo mengine haya zahanati, hospitali ya Wilaya itakuwa rahisi zaidi kuwahudumia wananchi wetu. Naomba sana Serikali iweze kufikiria mgawo huu wa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ili tuweze kuwahudumia wananchi wetu kwa uzuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho kabisa suala la barabara. (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naunga mkono hoja.