Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wengine wamechangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri ambayo imejaa uzalendo na ukweli ndani yake, kwa sababu nilipokuwa nikisoma hakuna chembechembe za ushilawadu ndani yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwa ukurasa namba 16 unaosema asilimia 56 ya nguvu kazi ya Taifa ni vijana, wengi wa vijana hawa wameajiriwa kwenye sekta isiyo rasmi na ni wengi kweli zaidi ya asilimia 70 katika nchi yetu na kwa wakati huu kundi hili linazidi kuongezeka maana mwanzoni lilikuwa na vijana wachache, lakini hasa ambao wana elimu ya darasa la saba, kidato cha nne na wengine kidato cha sita, lakini sasa hivi linaingiza kundi la vijana wasomi ambao pia wamemaliza hata chuo kikuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kundi hili linaanza kuwa muhimu sana wakati huu na tusipoangalia kama Serikali basi tutakuwa tunapoteza nguvu kazi nyingi kwa sababu wanajiunga kwenye kundi la sekta isiyo rasmi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta hii isiyo rasmi ina changamoto nyingi. Moja ni udogo wa mtaji, mitaji yao ni kidogo sana. Pili, ni tija ndogo kwenye uzalishaji wanaohusikanao, pia wana matumizi duni sana ya teknolojia pia utaratibu wa wao kujisajili na kuwa kwenye sekta rasmi ni mrefu sana Kiserikali unawakwaza. Kodi ambazo zinatozwa kwenye kundi hili si rafiki sana kuwafanya waondoke kwenye sekta isiyo rasmi kuingia kwenye sekta iliyo rasmi, kubwa kabisa ni kwamba kundi hili lina ukosefu wa mahali pa kufanyia shughuli zake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia mara nyingi watu hawa wamekuwa wakiondolewa, wakikaa mahali fulani kidogo wanaondolewa, aidha inatolewa amri na Mkuu wa Wilaya au Mkuu wa Mkoa. Wote tumeshuhudia kipindi kilichopita namna ambavyo kundi hili la wafanyabiashara, wale wasio rasmi, walivyofurushwa kule Mwanza na Dar es Salaam mpaka Mheshimiwa Rais mwenyewe akaingilia kati. Kwa kuangalia matatizo haya waliyonayo hatujaonesha kama Taifa kwamba tunataka kulipunguza kundi hili la sekta isiyo rasmi ili liingie kwenye sekta iliyo rasmi, hivyo mchango wake katika Taifa hili kiuchumi na kimapato umekuwa
mdogo sana kwa sababu siyo rahisi sana kulifuatilia kundi hili kwa mifumo rasmi iliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iangalie upya mfumo wake ili kulifanya kundi hili litoke katika sekta isiyo rasmi liingie kwenye sekta rasmi ambayo itatoa mchango mkubwa kwenye uchumi wa nchi yetu, vinginevyo tukiliacha namna hii na kundi hili linaendelea kukua basi tutakuwa na kundi kubwa. Tunapokuwa na kundi kubwa limekaa kwenye sekta isiyo rasmi, wataalam wa uchumi wanasema bado kundi hilo litabaki kwenye hali ya umaskini.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naisihi Serikali ije na mkakati au sera mpya kwa sababu sera iliyopo inayolihusu kundi hili, ile ambayo nimeiona ni ile ya mwaka 1994. Sasa kama ipo nyingine labda sijaiona, lakini kama ni ya zamani kiasi hicho basi Serikali ni vizuri ije na sera mpya, sera hiyo iainishe ni kwa namna gani inalitoa kundi hili kutoka kwenye sekta isiyo rasmi kuliingiza kwenye sekta iliyo rasmi ili kundi hili pia liweze kulipa kodi kwa Serikali na liweze kutoa ajira kwa wananchi walio wengi kwa sababu likibaki kwenye kundi hili la sekta isiyo rasmi haliwezi kutoa ajira tunazozitegemea na hatuwezi kupata mapato ya kutosha kwenye kundi hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka niliongelee ni suala la taarifa zinazotoka kwenye Taasisi za Serikali. Mwaka jana mwezi wa Oktoba mwanzoni au mwezi wa Septemba mwishoni, Tanzania Meteorological Agency (TMA) walitoa taarifa yao kuhusiana na hali ya mvua
ya vuli na mwelekeo wa mvua za masika zitakavyokuwa. Taarifa hii ilitolewa kipindi kile cha Oktoba na Disemba na wakatahadharisha pia kwamba kipindi cha masika Novemba mpaka Aprili pia ni wakati wa mvua za masika lakini mvua zitakuwa ni kidogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hizi sikuona kama zinaratibiwa vizuri na kutumiwa vizuri na watu walioko Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kiasi kwamba sasa tulipofika kwenye mvua za vuli, mvua za vuli kweli zilikuwa ni chache, maeneo mengi yalikuwa ni makavu na maeneo mengi yanayotumia mvua za vuli kulima walipolima hawakuotesha na wengine waliootesha mazao yalikauka kwa sababu kipindi cha mvua kilikuwa kifupi sana. Hata hivyo, kipindi cha mvua za masika pia kilichelewa sana mvua maeneo mengine zimenyesha Februari na Januari mwishoni, matokeo yake wakulima walipopanda mvua tena zimekuja kukatika hapa katikati. Sasa matokeo yake tumekuwa na mavuno kidogo katika maeneo mengi ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua na tunakumbuka kweye Bunge hili kwamba Bunge lililopita, Waziri wa Kilimo alikuja na takwimu akasema Wilaya kama 55 hivi zina upungufu mkubwa wa chakula, lakini hatukuona hatua zinazochukuliwa na Serikali kuanzia pale TMA walipotangaza
hali za mvua kutopatikana zile za vuli na hata hizi za masika. Hatukuona hatua zinazochukuliwa na Wizara ya Kilimo ili kuwatahadharisha wakulima na kuwatayarisha waweze kujitayarisha na jambo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naona shida hapa kwamba, taarifa zinatoka hukohuko Serikalini, Taasisi ni ya Serikali, zinakuja huku upande mwingine hazitumiki vizuri. Sasa ninaiomba Serikali wawe na uratibu mzuri wa taarifa zinazotoka hasa zinazotusaidia wanyonge kama wakulima
huko kijijini. Vinginevyo tusipopata tahadhari ya namna hii tunaendelea na mambo tukijua mambo yatakuwa kawaida na kumbe kule mbele tunakutana na hatari. Kwa hiyo, niiombe Serikali wawe wanaratibu vizuri taarifa zinazotoka kwenye taasisi zake ziweze kuwa za manufaa kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu ya mwaka jana inasema fedha zilizoombwa ni shilingi bilioni 236 na kuendelea, lakini mwaka 2017/2018 fedha zilizoombwa ni shilingi bilioni 171. Fedha ya Matumizi ya Maendeleo 2016/2017 ni shilingi bilioni 165 lakini mwaka 2017/2018 ni bilioniā€¦
Ooh! Ahsante, naomba kuunga mkono hoja.