Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naungana na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni Mheshimiwa Rais alifanya ziara Mkoani Mtwara na ametufanyia kazi kubwa sana, mojawapo ikiwa ni kutatua changamoto ambayo ilikuwa inakabili Kiwanda cha Dangote. Hapa jana kuna mchangiaji mmoja alitoa maelezo ambayo pengine
alichokifanya Rais kule Mtwara hakukielewa, anasema Dangote amepewa eneo la mgodi kwa ajili ya kuchimba makaa na maamuzi yale yatakuwa na athari kama tutakavyofanya mchanga kutoka kwenye migodi ya almasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilichofanyika Mtwara ni tofauti na hicho alichokisema mchangiaji kwa sababu Mheshimiwa Rais ametatua changamoto mbili kuu ambazo Kiwanda cha Dangote kilikuwa kinakabiliwa nayo. Changamoto ya kwanza ilikuwa ni upatikanaji wa Makaa na alisema tunaamua hapa hapa. Mheshimiwa Muhongo na Mawaziri wengine walikuwepo na walipewa siku saba kwamba taratibu zote zifuatwe ili achimbe mkaa mwenyewe na kodi zote stahili alipe ili apeleke kwenye kiwanda chake cha Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha pili, Mheshimiwa Rais alitatua tatizo la muda mrefu ambalo ni upatikanaji wa gesi asilia kutoka Madimba. Tulikuwa tunalalamika hapa kwamba wawekezaji wakubwa hawasikilizwi, kwa hiyo, Mheshimiwa Rais akatoa maamuzi pale kwamba TPDC impe
umeme Dangote bila kupitia kwa mtu mwingine wa pili. Kwa hiyo, maamuzi yale ni ya kumpongeza sana Mheshimiwa Rais na siyo ya kumkatisha tamaa kwamba alichofanya siyo sahihi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwa niaba ya Wabunge wa Mtwara na kwa niaba ya wananchi wa Mtwara tunamshukuru sana Rais wetu kwa maamuzi mazito aliyoyafanya katika ziara yake Mkoani Mtwara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nichangie hoja nyingine ukurasa wa 23 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hatua alizochukua katika kusimamia zao la korosho. Wananchi wa Mtwara na wananchi wa Kusini wanakupongeza kwa kile ulichokifanya mwaka huu. Kwanza hukusita kuvunja bodi pale uzembe ulipotokea, lakini pili, ulichukua hatua ya kusimamisha uendeshaji wa Mfuko wa
Pembejeo na kazi hiyo sasa ikapelekwa kwenye Bodi ya Korosho na kusimamia kwa karibu kwa yale yanayoendelea katika tasnia ya korosho katika msimu wote. Hata pale zilipopotea tani 2,000 kwenye lile ghala la Masasi, ulichukua hatua za haraka na wale watuhumiwa sasa hivi
wamefikishwa kwenye vyombo vya sheria. Tunakupongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizo, bado kwenye mfumo wetu wa Stakabadhi Ghalani kuna changamoto ambazo kwa usimamizi wako Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wa Kilimo nafikiri msimu huu mtazirekebisha ili bei ya korosho izidi kupaa, na sisi Wana-
Mtwara tunategemea bei ya korosho mwaka huu itafika kilo shilingi 5,000. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilizopo ni pamoja na wakulima kucheleweshewa malipo na hii ni kwa sababu vyombo vingi havikujiandaa na ununuzi wa msimu wa mwaka huu na ule utaratibu wa mwaka huu. Tumeona pale ghala ya Benki Kuu ilikuwa inaingia Mtwara kila baada
ya siku moja. Kwa hiyo, nafikiri kwa sababu sasa hivi Tawi la Benki Kuu limezinduliwa Mtwara, yale ambayo yalikuwa yanatokea mwaka huu kwamba kila baada ya siku moja zinapelekwa fedha Mtwara, nafikiri msimu ujao hayatajitokeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kuna changamoto ya usafirishaji. Tumeona pale zikitokea kauli mbili; Watendaji wa Bandari wanasema Bandari ya Mtwara inaweza kusafirisha korosho lakini Mkoa wa Lindi wanasema kwamba Mtwara hawana uwezo wa kupeleka korosho zote, kwa hiyo, tusafirishe kwa barabara. Yote kwa yote, kuna changamoto pale zimejitokeza. Kwa hiyo, ni matarajio yangu kwamba Mamlaka ya Bandari, Wizara husika na Wizara ya Kilimo wataishughulikia hii changamoto ili mwakani korosho zote zisafirishwe kwa Bandari yetu ya Mtwara kwa sababu korosho zinaposafirishwa kwa Bandari ya Mtwara, tunawapa vijana wetu ajira, lakini vilevile tunadhibiti ununuzi wa korosho holela ule ambao unajulikana kwa jina la kangomba. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo tunatakiwa tulifanye katika mfumo wetu wa Stakabadhi Ghalani, tuongeze uwazi. Sasa hivi kuna malalamiko kwa wakulima kwamba mkulima anauza korosho yake kwenye mnada wa pili, lakini amelipwa kwa bei ya mnada wa tano. Kwa hiyo, nafikiri hili Wizara ya kilimo italifanyia kazi. Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, katika mfumo huu wa Stakabadhi Ghalani, kuna tozo moja. Kwanza tumshukuru na tumpongeze Mhesimiwa Waziri Mkuu, mwaka 2016 kwa usimamizi wake walifanikiwa kuondoa tozo tano kwenye zao la korosho. Kwa hiyo, kuna tozo moja ambayo inalalamikiwa sana na wakulima, tozo ya uchangiaji wa gunia. Ni matarajio yangu kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya kilimo na wadau watalishughulikia suala hili ili gunia zinunuliwe na Bodi ya Korosho au Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho ili wakulima wasichajiwe ile fedha ya kuchangia ununuzi wa gunia kila kilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niende ukurasa wa 36 ambao unahusu elimu na mimi nakubaliana kauli ya Waziri Mkuu kwamba uchumi wa viwanda lazima unahitaji rasilimali watu yenye weledi, lakini rasilimali watu yenye weledi inapatikana kukiwa na mfumo bora wa elimu. Lazima hapa
tukubaliane kwamba tunapozungumzia mfumo bora wa elimu au tunapozungumzia elimu bora, hatuwezi kusahau mahitaji na kero za walimu. Kwa hiyo, naomba sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano ijikite katika kuondoa changamoto zinazowakabili Walimu. Walimu bado wana malalamiko kwamba wana madai, bado hatujaandaa incetive package kwa Walimu wapewe motisha; lakini Walimu vile vile wanahitaji mafunzo kazini. Kwa hiyo, naomba Serikali chini ya Mheshimiwa Profesa Ndalichako na Mheshimiwa Simbachawene, basi walishughulikie hili suala la matatizo ya walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie mchango wangu kuhusu suala la maji. Kwanza naipongeza Wizara ya Maji kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya na katika Jimbo langu kuna harakati ambazo zinaonekana, za kuongeza kiwango cha upatikanaji wa maji kutoka asilimia 40 kwenda kwenye malengo yetu ya kufika asilimia 85, lakini bado kuna changamoto nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza kuna ule mradi ambao tunatarajia kupata mkopo kutoka Benki ya India, miradi 17 ambapo ni pamoja na mradi wa Muheza, ule mradi wa Makonde. Kwa kweli ni muda mrefu sasa hivi tunataka mradi huu uanze kutekelezwa. Kila siku
mnasema kwamba tunamalizia financial agreement, lakini sasa hivi natarajia Wizara ya Maji itaongeza speed ili mradi huu uanze kutekelezwa. Mradi huu ukianza kutekelezwa kwa miradi ile 17, tuna uhakika kwamba asilimia ya watu wetu ambao wanapata maji vijijini itaongezeka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, kwa sisi Wana- Mtwara kuna mradi wa kutoa maji Mto Ruvuma na kupeleka Manispaa ya Mtwara. Mradi huu ni tegemeo kwetu na utaongeza upatikanaji wa maji katika Jimbo langu la Nanyamba. Kwa hiyo, naomba pia na utekelezaji wa mradi huu usimamiwe kwa karibu na fedha zipatikane ili utekelezaji wake uanze mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja na yale yote ambayo yapo katika kitabu cha Waziri Mkuu yakitekelezwa, tuna uhakika kwamba nchi yetu tunakwenda kule ambako tunatarajia. Ahsante sana.